WAZIRI MKUU AKARIBISHA WAWEKEZAJI KUTOKA JAPAN
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
akizungumza na Rais na Ofisa mtendaji Mkuu wa kampuni ya Sumitomo 
Corporation ya Japan, Bw. Kunihuru Nakamura  katika Mkutano wa TICAD 6 
uliofanyika Nairobi Kenya, Agosti 28, 2016. (Pivha na Ofisi ya Waziri 
Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisalimiana na Rais na Ofisa 
mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Sumimoto Corporation ya Japan katika mkutano
 wa TICAD 6 uliofanyika jijini Nairobi Agosti 28,2016. (Picha na ofisi 
ya Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
akiwa katika picha ya pamoja na Rais na Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni 
ya Sumimoto ya Japan, Bw. Kanihuru Nakamura  (kushoto kwake) baada ya 
mazungumzo yao jijini Nairobi Agosti 28, 2016. Kushoto ni Naibu Katibu 
Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Profesa James Mdoe na Kulia ni 
Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Dkt.Adelhelm 
Meru.  Wanne kushoto ni Balozi wa Tanzania nchini Japan, Mathias 
Chikawe. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majliwa akisalimiana na Balozi wa Umoja
 wa Mataifa anayeshughulikia  Masuala ya Wakimbizi, Fillipo Grand kabla 
ya mazungumzo yao jijini Nairobi, Agosti  28, 2016. (Picha na Ofisi ya 
Waziri Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
akikabidhiwa kitabu chenye picha ramani na taarifa za jiji la Yokohama 
nchini Japan na Meya wa jiji hilo, Bi. Fumiko Hayashi baada ya 
mazungumzo yao jijini Nairobi Agosti 28, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri
 Mkuu)
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa TANTRADE, Bw. Edwin 
Rutageruka (kushoto) wakati alipotembelea banda la Tanzania katika 
maonyesho yaliyokwenda sambamba na mkutano wa TICAD 6 jijini Nairobi 
Agosti 28, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
 akimsikiliza , Bw. Lameck Borega (kushoto) ambaye ni Meneja wa 
Uwekezaji kutoka EPZA, Mabibo jijini Dar es salaam wakati alipotembelea 
banda la Tanzania katika maonyesho yaliyokwenda sambamba na mkutano wa 
TICAD 6 jijini Nairobi Agosti 28, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
akitazama pipili iliyosindikwa na kupewa jina la AKABANGA wakati 
alipotembelea banda la Rwanda katika  maonyesho yaliyokwenda sambamba na
 mkutano wa TICAD 6 jijini Nairobi Agosti 28, 2016. (Picha na Ofisi ya 
Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
akizungumza na washiriki wa maonyesho kutoka Senegal wakati 
alipotembelea bada lao kwenye  maonyesho yaliyokwenda sambamba na 
mkutano wa TICAD 6 jijini Nairobi Agosti 28, 2016. (Picha na Ofisi ya 
Waziri Mkuu)
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa 
 akitazama nguo za batik wakati alipotembelea banda la Tanzania kwenye  
 maonyesho yaliyokwenda sambamba na mkutano wa TICAD 6 jijini Nairobi 
Agosti 28, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
…………………………………………………………………………………
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa 
amewakaribisha wawekezaji kutoka Japan na kusema kwamba kufanyika kwa 
Mkutano wa Sita wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Bara la Afrika
 (TICAD VI) jijini Nairobi kumetoa fursa kwa Tanzania na nchi nyingine 
kukutana na wafanyabiashara wakubwa wenye nia ya kuwekeza barani humo.
Ametoa kauli hiyo jana (Jumapili, 
Agosti 28, 2016) alipokutana faragha kwa nyakati tofauti na viongozi wa 
makampuni makubwa ya Japan ambao walikuwa wakihudhuria mkutano huo 
uliofanyika katika kituo cha Mikutano ya Kimataifa cha Jomo Kenyatta 
(JICC) jijini Nairobi, Kenya.
Mkutano wa sita wa TICAD ambao 
umemalizika jana, ulilenga kuiwezesha Afrika katika sekta ya uchumi na 
uwekezaji. Ili kufikia lengo hilo, mkutano huo umewashirikisha wadau wa 
sekta binafsi zikiwemo kampuni binafsi zaidi ya 300 kutoka Japan.
Katika mazungumzo yake na Waziri 
Mkuu, Rais wa kampuni ya Sumitomo, Bw. Kuniharu Nakahura, alisema 
kampuni hiyo imeanza utekelezaji wa mradi wa Kinyerezi II wa kuzalisha 
umeme wa MW240 kutoka gesi asilia (Gas Fired Combined Cycle Gas Power Plant). Mradi huo ulioanza kutekelezwa Machi 2016, unatarajiwa kukamilika ndani ya miaka mitatu.
Bw. Nakahura ambaye pia ni Afisa 
Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, alisema kampuni yao inajishughulisha 
zaidi na utengenezaji wa bidhaa za vyuma, kemikali, ujenzi wa 
miundominu, na usafirishaji.
Naye Makamu wa Rais wa kampuni ya 
Toyota Tshuso, Bw. Yasuhiko Yokoi alikutana na Waziri Mkuu na kumweleza 
jinsi kampuni hiyo kubwa duniani inavyoweza kushiriki na kuchangia 
maendeleo nchini Tanzania.
Alisema kampuni yao 
inajishugulisha zaidi na masuala ya miundombinu ikiwemo kuzalisha 
mitambo ya umeme na mitambo ya bandari. Pia inazalisha bidhaa za kilimo 
(matrekta, mashine za viwanda vya mbolea na nguo, ujenzi wa maghala ya 
nafaka), mitambo ya nguvu za umeme wa joto-ardhi na uzalishaji wa magari
 ya aina mbalimbali.
“Kwa mfano hapa Kenya, tumeweza 
kutengeneza mitambo midogo ya kisasa ambayo inazalisha mbolea tofauti 
kulingana na hali halisi ya udongo wa mahali husika. Huwezi kuzalisha 
mbolea ya aina moja na kuamua kuisambaza kwa nchini nzima. Tunapima 
udongo wa sehemu moja na kuzalisha mbolea inayofaa kwa udongo ule,” 
alisema.
Naye Rais wa kampuni ya Marubeni, 
Bw. Fumiya Kokubu alimweleza Waziri Mkuu kwamba maeneo ambayo wangependa
 kuwekeza ni kwenye viwanda vya nguo, mbolea, saruji, uzalishaji wa 
sukari, umeme wa gesi na hasa miradi ya LNG.
Kwa upande wake, Waziri Mkuu 
aliwahakikishia wawekezaji hao kuwa Serikali iko tayari kushirikiana nao
 na akawashauri watume timu za maafisa wao ili wakutanishwe na wadau wa 
sekta husika.
Alisisitiza kuwa Tanzania hivi 
sasa imedhamiria kuwa nchi ya uchumi wa viwanda na kwa sababu hiyo 
inahitaji kuwa na nishati ya kutosha ili iweze kumudu kuendeleza sekta 
hiyo. “Serikali ya awamu ya tano imeamua kujenga uchumi wa viwanda, 
tunahitaji kujenga viwanda vya kutosha ili tuweze kusindika mazao ya 
wakulima ambao wanafikia asilimia 80 ya Watanzania wote. Tunahitaji 
masoko ya uhakika kwajili ya mazao wanayozalisha,” alisema.
Akiwa kwenye mkutano huo, Waziri 
Mkuu pia alikutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Umoja wa Mataifa 
anayeshughulikia masuala ya wakimbizi, Bw. Filippo Grandi; Meya wa Jiji 
la Yokohama, Bibi Fumiko Hayashi; na Makamu wa Rais wa Kwanza wa Sudan, 
Jenerali Bakri Hassan Saleh.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu 
alitembelea Maonesho ya Biashara ya Afrika na Japan (Africa-Japan Expo 
2016) ambapo Mamlaka ya Kuendeleza Biashara Tanzania (TANTRADE) na wadau
 wengine kama Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Mamlaka ya Kukuza 
Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Mamlaka ya 
Ukanda Maalumu wa Uwekezaji (EPZA) walishiriki.
Akiwa huko alitembelea pia mabanda
 ya Uganda, Rwanda, Sénégal, Kenya, Japan na UN Habitat. Pia alitembelea
 banda la wajasiriamali wa nguo kutoka Tanzania ambao walishiriki 
maonyesho hayo yaliyofanyika kwenye viwanja vya Kituo cha Mikutano ya 
Kimataifa cha Jomo Kenyatta (JICC) jijini Nairobi, Kenya.
Waziri Mkuu alirejea jijini Dar es Salaam jana usiku.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni