Misaada huwa haitozwi kodi – TRA
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) 
imetoa ufafanuzi juu ya utozwaji wa kodi za misaada inayotolewa na 
wadhamini kusaidia Sekta ya Maendeleo ya Michezo Nchini.
Ufafanuzi huo umetolewa leo na 
Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi, Richard Kayombo kutokana 
na habari iliyochapishwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari kuhusu 
Serikali kukosa mabilioni ya fedha kwa sababu ya kutokukusanya kodi ya 
fedha zinazotolewa na wadhamini kwenda kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu 
Tanzania (TFF).
“Fedha zinazotolewa kama msaada 
kutoka kwa wadhamini huwa hazikatwi kodi lakini TRA hupata mapato yake 
kutokana na matumizi ya fedha hizo hasa pale wahusika wanapozitumia 
katika shughuli za kiuchumi”,alisema Kayombo.
Kayombo ametaja baadhi ya shughuli
 za kiuchumi zinazoweza kuwaingizia mapato kutoka kwenye misaada hiyo 
kuwa ni; kodi za waajiriwa wakiwemo makocha na wachezaji, makusanyo ya 
uwanjani ,kupewa huduma za kitaalam pamoja na majengo ya kupangisha au 
kupanga.
Amefafanua kuwa kama Shirikisho la
 Mpira wa Miguu Nchini  (TFF) linakodisha jengo basi fedha wanazopata 
lazima walipe kodi ya asilimia 10 kutoka kwenye fedha hizo na kama wao 
ndio wamekodi jengo kwa ajili ya matumizi yao wanatakiwa kutoa kodi ya 
asilimia 5.
Kwa upande wa kodi kutoka kwa 
waajiriwa, Mamlaka hiyo inaendelea kutoa elimu kwa vilabu vya michezo 
kuwa michezo ni ajira kama ajira zingine hivyo mishahara yao inatakiwa 
kukatwa kodi kulingana na kiasi wanacholipwa.
Zoezi la kuwatoza kodi makocha na wachezaji limeanza rasmi mwaka huu.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni