WASOMI: JPM NA LOWASSA WAMEONYESHA KUWA MAZUNGUMZO YATALETA MUAFAKA.
Na Tiganya Vincent, MAELEZO- Dar es salaam
Wasomi na Wanazuoni mbalimbali 
wamepongeza hatua ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. 
John Pombe Magufuli na Waziri Mkuu zamani  Edward Lowassa kushikana 
mikono na kusalimiana wakati wa Jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya ndoa 
ya Rais Mstaafu Benjamin William Mkapa na Anna Mkapa.
Wanazuoni hao wametoa  kauli 
hiyo leo katika mahojiano maalum na Idara ya Habari iliyokuwa ikitaka 
kupata maoni yao kuhusu kitendo kilichoonyeshwa na viongozi hao kwa 
jamii.
Profesa Kitila Mkumbo wa Chuo 
Kikuu cha Dar es Salaam amesema kuwa hatua hiyo imeonyesha kuwa huo ndio
 Utanzania ulivyo wa kutofautiana bila kugombana.
Amesema kuwa kitendo hicho 
kimewaonyesha wananchi kuwa mazungumzo yana nafasi kubwa ya kuondoa 
tofauti zilizopo kuliko kutumia njia nyingine kama vile maandamano na 
mabavu katika kutafuta ufumbuzi wa baadhi ya matatizo.
“Kukutana kwa viongozi hao na 
kupeana mikono wakati wa kusalimiana kunakumbusha utamaduni wetu 
uliojingekea toka siku nyingi wa kutatua matatizo yetu kwa mazungumzo 
bila kugombana au kutumia mabavu,”alisema Profesa Mkumbo.
Kwa upande wa Profesa Joseph 
Semboja amesema kuwa amefurahishwa sana na kitendo kilichoonyeshwa na 
viongozi hao kwani kimeuonyesha ulimwengu kuwa Watanzania ni watu wenye 
 Amani na upendo.
Amesema kuwa hatua hiyo 
imeonyesha kuwa Watanzania wanaweza kuwa na tofauti lakini wakaendelea 
kuishi pamoja na kushirikiana katika mambo mbalimbali ya kijamii kwa 
ajili ya maendeleo yao na Taifa lao.
Profesa Semboja amewataka 
wananchi kujifunza kutokana na kitendo kilichoonyeshwa na viongozi hao 
ambao wameonyesha kuwa ni lazima wakae pamoja kwa ajili kushughulikia 
mambo muhimu ya maendeleo ya wananchi badala kuendeleza tofauti ambazo 
hazina manufaa kwa Watanzania.
Amesema kuwa ipo haja ya kwenda 
zaidi ya hapo kwa kuweka utaratibu wa kukaa pamoja na kujadiliana ili 
kutatua vyanzo vya migogoro kwa ajili ya mustakabali mzuri wa Taifa 
hili.
Profesa amesema kuwa sio sahihi 
kutumia mfumo wa jino kwa jino kwani utaratibu huo ndio unaoweza 
kusababisha kukua zaidi kwa migogoro na wakati mwingine unasababisha 
umaskini kwa wananchi na Taifa kwa ujumla kwani muda mwingi wananchi 
hawana muda wa kushiriki katika shughuli za maendeleo kwa sababu ya 
migogoro.
Naye Profesa Samwel Wangwe 
amesema kuwa hatua ya viongozi hao kukutana na kupeana mikonop ni ishara
 kwa Watanzania kujifunza kuwa mazungumzo yana nafasi kubwa katika 
kuleta muafaka mgogoro wowote kuliko kutunishiana misuli.
Amesema kuwa mazungumzo yana 
nguvu kubwa katika kultea upatanishi katika migogoro mbalimbali inatokea
 katika jamii kuliko kutumia njia nyingine ambazo zinaweza kusababisha 
vurugu na uharibifu wa mali za watu na upotevu wa maisha ya watu.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni