STDFAA wamuomba Nape kuharakisha Sera ya filamu
Katibu wa Chama cha Waigizaji cha 
Mkoa wa Kinondoni (STDFAA) , Jafari Makatu akiongea na waandishi wa 
habari (hawapo pichani) leo Jijini Dar es Salaam juu ya changamoto 
zinazowakabili katika tasnia ya filamu nchini, kulia ni Mwenyekiti wa 
chama hicho, Ali Baucha na kushoto ni Mdhamini wa Chama hicho, Ahmed 
Olotu.
……………………………………………………………………………
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO
Chama cha Waigizaji cha Mkoa wa 
Kinondoni (STDFAA) wamemuomba Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na 
Michezo, Mhe Nape Nnauye kuiharakisha Sera ya filamu ili iwasaidie 
katika mambo mbalimbali hususani ya kisheria.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es 
Salaam na Katibu wa Chama hicho, Jafari Makatu alipokuwa akiongea na 
waandishi wa habari kwa ajili ya kutoa pongezi kwa Serikali ya Awamu ya 
Tano pamoja na kuzungumzia changamoto zinazowakabili katika tasnia ya 
filamu nchini.
Makatu amesema kuwa Sheria ya 
Filamu ni muhimu katika tasnia hiyo hivyo ikiharakishwa itasaidia wadau 
wa tasnia hiyo kufanya kazi kwa uwazi na usalama wa hali ya juu kwa kuwa
 watakua wanalindwa na sheria.
“Tunamuomba Waziri wetu Mhe. Nape 
atuharakishie Sera ya Filamu kwa sababu sheria hiyo itatusaidia 
kuoanisha mambo mbalimbali ya kisheria kuanzia kwenye uandaaji wa kazi 
zetu hivyo, kupelekea kufanya kazi kwa  ufanisi na kutoa kazi bora 
zaidi”. Alisema Makatu.
Ameongeza kuwa sheria hiyo pia 
itawasaidia katika suala zima la Haki miliki na Haki shiriki, malipo 
stahiki kwa kila kazi, masoko, madaraja ya waigizaji na wadau wote wa 
tasnia ya filamu pamoja na ulazima wa kila msanii kujiunga katika vyama 
husika vitakavyowasaidia katika mambo mbalimbali.
Aidha, Katibu huyo ameiomba 
Serikali kuwekeza kwenye sanaa ili kuwawezesha kuifanya kazi hiyo kwa 
ufanisi na kuchangia katika Pato la Taifa pia amemuomba Mhe.Nape 
kuwatafutia eneo maalum la ardhi ambalo litawasaidia katika kufanyia 
shuhuli zao za kurekodi filamu.
Ametoa rai kwa wasanii kujiunga 
katika vyama mbalimbali vinavyowahusu ili kuleta umoja, mshikamano na 
tija katika kazi za sanaa,amesisitiza wasanii kujiunga na Bima za Afya.
Naye Mdhamini wa Chama hicho, 
Ahmed Olotu amewaomba waandishi wa habari kutumia kalamu zao katika 
kuwasaidia wasanii kupambana na wauzaji  wa filamu feki kwa kuwa 
wanarudisha nyuma maendeleo ya wasanii na kupunguza pato la Taifa.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni