Waziri Nape Nnauye awataka Watanzania kuwapa Moyo Wanamichezo nchini.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa
 na Michezo, Mhe. Nape Nnauye (Mb) (kulia) akimkabidhi cheti Mwanariadha
 Alphonce Simbu baada ya kuibuka mshindi wa nafasi ya tano katika 
Mashindano ya Olimpiki yaliyomalizika hivi karibuni mjini Rio, Brazil.
Waziri wa Habari, 
Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye (Mb) (kulia) akimkabidhi 
King’amuzi cha Kampuni ya DSTV Mwanariadha Alphonce Simbu baada ya 
kuibuka mshindi wa nafasi ya tano katika Mashindano ya Olimpiki 
yaliyomalizika hivi karibuni mjini Rio, Brazil.

Rais wa Shirikisho la 
Riadha Tanzania (RT) Bw. Anthony Mtaka akiongea na baadhi ya Viongozi, 
wageni waalikwa pamoja na Wanamichezo (hawapo pichani) walioshiriki 
katika Mashindano ya Michezo ya Olimpiki yaliyomalizika hivi karibuni 
mjini Rio, Brazil.
Mwenyekiti wa Kamati 
ya Olimpiki (TOC) Bw. Filbert Bayi akiongea na baadhi ya Viongozi, 
wageni waalikwa pamoja na Wanamichezo (hawapo pichani) walioshiriki 
katika Mashindano ya Michezo ya Olimpiki yaliyomalizika hivi karibuni 
mjini Rio, Brazil.
PICHA ZOTE NA BENEDICT LIWENGA-WHUSM.
…………………………………………………………………………….
Na Benedict Liwenga-WHUSM.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape 
Nnauye amewataka Watanzania kujifunza kuwatia moyo Wanamichezo 
wanaposhiriki katika michezo mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Wito huo ameutoa jana Jijini Dar es Salaam wakati wa Hafla 
ya kuwapongeza na kupokea bendera ya Taifa toka kwa Wanamichezo ambao 
walishiriki katika Mashindano ya Olimpiki yaliyomalizika hivi karibuni 
mjini Rio, nchini Brazil.
Mhe. Nnauye alisema kwamba, Watanzania ni vizuri 
wakajifunza kusema maneno mazuri kwa wanamichezo pindi wanaporejea toka 
katika Mashindano mbalimbali ili kuwapa moyo wa kuendelea kufanya vizuri
 wanamichezo hao huku akisisitiza kuwa, ni vema ukosoaji ukaendana na 
ushauri mzuri wenye kujenga badala ya kulaumu.
 Aliongeza kuwa, Wanahabari nchini wanapaswa kuandika 
mazuri yanayofanywa na wanamichezo kwani yana manufaa kwa Taifa badala 
ya kutafuta maneno yasiyo na tija ya kukosoa mara kwa mara kwani kuna 
wavunja moyo wanamichezo.
“Tukijifunza kuandika na kusema mabaya tu ya kuvunja moyo 
kwa wanamichezo wetu hii sio sawa sawa, tujifunze kuwatia moyo, na hii 
ni hatua ya kwanza na wito wangu kwa Watanzania wote”, alisema Mhe. 
Nnauye
Alisisitiza kwamba, Watanzania wanapaswa kujifunza 
kujivunia vitu vya kwao kwa njia hiyo itakuwa ikiongeza hamasa kwa 
wanamichezo katika kujituma kwa manufaa yao na ya Taifa.
Aidha, alisisitiza kuwepo na maandalizi ya mapema kwa 
Wanamichezo nchini ili waweze kufanya vizuri zaidi huku akishauri 
uwekezaji wa kutosha katika sekta hiyo na kuyataka Makampuni kuwa na 
tabia ya kuwatumia Wanamichezo nchini katika kutangaza utalii wa nchi.
Ametoa wito kwa Viongozi wazembe ambao watashindwa kufikia 
malengo mazuri katika tasnia hiyo ni bora wakaachia ngazi zao ili kuwapa
 nafasi watu wengine wenye uwezo kutekeleza kazi hiyo.
“Nadhani sasa tuanze kukabana kwenye Vyama, ukichaguliwa na
 kukawa na mashindano kama haya, ukashindwa kupeleka hata mchezaji 
mmoja, kazi yako ya kwanza nadhani ni kijiuzulu”, alisema Mhe. Nnauye.
Awali akitoa taarifa ya Wanamichezo walioshiriki katika 
Mashindano hayo, Rais wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) Bw. Gulam 
Rashid alisema kwamba, Tanzania ilishiriki mashindano hayo ikiwa na 
Wanamichezo saba, walimu wa tatu wa michezO ya kuogelea, Judo na riadha 
ambapo kati yao wachezaji wa nne walipata nafasi ya upendeleo (Universality).
Alifafanua kuwa, wachezaji wa nne waliofanikiwa kupata 
nafasi ya upendeleo ni wale ambao walishiriki katika michezo mbalimbali 
katika kusaka viwango, lakini kwa bahati mbaya hawakuweza kufikia 
viwango vinavyowaruhusu wao kushiriki katika mashindano hayo, hivyo 
kulingana na Sera na itikadi za Olimpiki zilitaka kila nchi Duniani 
ambayo ni Mwanachama wa Mashindano hayo kutoa watu wake, hivyo walitoa 
nafasi hiyo kwa wale waliokosa kufikia viwango kuweza kushiriki.
“Nchi ambayo haikuwa na wachezaji waliofikia viwango vya 
Olimpiki walipewa nafasi ya upendeleo kwa wanamichezo kuweza kushiriki 
na kwa Tanzania tulikuwa na Waogeleaji wa tatu, mchezaji wa Judo na 
mchezaji wa kike wa mbio (Marathon) kwa hiyo, huo ndiyo upendeleo ambao 
wengi hawauelewi ni upendeleo upi”, alisema Bw. Gulam.
Aidha, katika hafla hiyo, mbali na kukabidhiwa Bendera ya 
Taifa toka kwa kikosi hicho cha Wanamichezo walioshiriki katika Olimpiki
 2016mjini Rio-Brazil, Mhe. Nnauye kwa niaba ya Makampuni ya TTCL na 
DSTV-Multi Choice aliwapatia zawadi mbalimbali washiriki hao zikiwemo 
fedha taslimu ambapo kwa nafasi ya kipekee Mwanariadha Alphonce Simbu 
ambaye aliibuka katika nafasi ya tano katika Mashindano hayo amepatiwa 
Mkataba wa mwaka mmoja wa kuwa Balozi wa DSTV ambapo kila mwezi atakuwa 
akilipwa kiasi cha Shilingi milioni moja pamoja na king’amuzi maalum, 
huku washiriki wengine wakipewa ving’amuzi na fedha.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni