CCM YAOMBOLEZA VIFO VYA POLISI WALIOUAWA NA MAJAMBAZI, SENDEKA AIVAA CHADEMA, AMJIBU TUNDU LISU
Msemaji wa CCM, Christopher Ole
 Sendeka akizungumzaa Waandishi wa Habari, kufafanua masuala mbalimbali,
 katika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba Jijini Dar es Salaam.Ifuatayo ni Taarifa rasmi Kama ilivyosomwa na Sendeka wakati wa kikao hicho na waandishi wa Habari.
…………………………………………………………………
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
 Ndugu wanahabari,
Chama cha Mapinduzi (CCM) 
kimepokea kwa majonzi na masikitiko makubwa sana taarifa ya kushambuliwa
 na kuuawa kwa askari wa jeshi la Polisi wakiwa katika kutekeleza 
majukumu yao ya ulinzi eneo la Mbande, Temeke jijini Dar Es Salaam.
CCM tayari imemtumia salamu za 
rambirambi Mkuu wa Jeshi la Polisi IGP Ernest Mangu pamoja na familia za
 marehemu waliofikwa na umauti katika tukio hilo baya katika historia ya
 nchi yetu.
Tunalaani tukio hilo na kutoa wito
 kwa wananchi kuvipa ushirikiano wa kutosha vyombo vya dola ili 
kufanikisha wahusika wa tukio hilo kusakwa popote pale na kupatikana ili
 wafikishwe mbele ya vyombo vya sheria haraka.
Serikali ya Chama Cha Mapinduzi 
itaendelea  kuhakikisha amani ya Taifa letu inalindwa dhidi ya wachache 
wanaofurahia madhila kwa wananchi wetu. Wananchi wetu wanapenda, 
wamezoea na wanastahili amani. Ndio maana Tanzania imekuwa nchi ya 
kupigiwa mfano, ikionesha uongozi katika maeneo mengi. Tuendelee 
kuilinda taswira hii.
MAFANIKIO YA AWAMU YA TANO
Ndugu wanahabari,
CCM inachukua nafasi hii 
kumpongeza Rais Mhe Dkt John Pombe Magufuli na Serikali yake kwa 
mafanikio makubwa yaliyopatikana katika muda mfupi wa uongozi wake.
Rais Magufuli aliahidi mabadiliko.
 Tunampongeza kwa kusimamia vema utekelezaji wa ilani ya CCM. Katika 
muda mfupi wa miezi tisa tu, Rais Dk Magufuli amefanya mambo makubwa.
Sote tunafahamu kuwa Shirika letu 
la Ndege, ATCL, limekuwa linafanya kazi na ndege moja. Serikali ya Dk 
Magufuli imekwisha lipia ndege tatu za abiria toka Canada, ndege mbili 
zitaingiza nchini mwezi ujao.
Reli ya kati inajengwa kwa kiwango
 cha Standard Gauge. Meli katika ziwa viktoria inanunuliwa ktk bajeti ya
 mwaka huu. Elimu ya msingi na sekondari inatolewa bure. Wanafunzi wetu 
sasa wanakalia madawati na kujifunza vizuri zaidi. Barabara zimeendelea 
kujengwa. Makusanyo ya kodi yameongezeka. Huduma za jamii zinaendelea 
kuimarika. Lakini pia, nidhamu katika utumishi wa umma sasa imeimarika. 
Wananchi wanastahili huduma nzuri na kuthaminiwa na wafanyakazi wa Umma.
Mataifa mengi ya Afrika na nje ya 
Afrika yanaiga mbinu za Rais wetu katika kuleta mabadiliko nchini mwao. 
Hapa Kenya tu, Waziri mmoja wa Elimu anayesifika kwa utendaji kazi 
mzuri, anajiita “MAGUFULI.” Hata Australia, baadhi ya wananchi waliwahi 
kumtaka Waziri Mkuu wao afanye kazi kama Dk Magufuli.
Dk. Magufuli ameazimia kujenga 
uchumi wa viwanda. Ifikapo mwaka 2025, Tanzania itakuwa nchi yenye 
uchumi wa kati. Maisha ya wananchi wetu yataboreka. Vijana wetu wapate 
ajira katika viwanda, watauza malighali na mahitaji mbalimbali ya 
viwanda. Wakulima watapata masoko ya bidhaa zao katika viwanda hivyo. 
Kilimo kitaongezeka thamani kutokana na mahitaji mbalimbali ya viwanda 
vyetu.  Hatua za kuelekea huko tayari zimechukuliwa.
Wapo wachache wanaelekea kutafuta 
mbinu chafu za kuhujumu mafanikio haya, lakini hawatafanikiwa. 
Watanzania wamemchagua Dk Magufuli ili awaletee maendeleo.   
Serikali ya CCM, itawasaidia 
vijana wa Tanzania kuendesha uongozi wa Taifa lao. Kamwe tusikubali 
ndoto ya kuongoza mapinduzi haya makubwa kwa ajili ya Taifa na Bara letu
 ikapokonywa na watu wachache wasiokuwa na dira ya kuliletea maendeleo 
Taifa letu. Tuwapuuze.
UPINZANI KUSUSIA VIKAO VYA BUNGE
Ndugu Wanahabari,
Bunge kama ilivyo kwa mhimili 
mingine linaongozwa kwa katiba, sheria na kanuni katika mijadala na 
maamuzi yake. Kama Mbunge hajaridhika na maamuzi ya Spika, Naibu Spika 
au Mwenyeki wa kikao, kuna taratibu za kufuata. Utaratibu wa kikanuni ni
 kuulalamikia uamuzi huo kwa Katibu wa Bunge. Wakiwa wanafahamu taratibu
 za kikanuni, kama kawaida yao, WAPINZANI, waliamua kuzisigina na badala
 yake wakataka Naibu Spika aondolewe.
Hivyo wakaratibu kupigwa kura ya 
kutokuwa na imani na Naibu Spika. Ambapo suala hilo lilipelekwa kwenye 
Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge. Kutokana na kutokuwepo kwa
 Spika nchini, hoja hiyo haikufikia ukomo. Tunamshukuru Mungu afya ya 
Spika imeimarika. Sasa hoja hiyo huenda itafikishwa katika mkutano wa 
Bunge litakalokaa mwezi ujao.
Kana kwamba hiyo haitoshi, kama 
kawaida yao, hawakuwa na subira ya kufuata taratibu. Wakaamua kufanya 
kihoja. Wakaamua kutohudhuria vikao vyote vya Bunge vilivyokuwa 
vikiongozwa na Naibu Spika.
Na hata walipoingia Bungeni 
waliziba midomo yao na kuamua kutowasalimia wabunge wenzao wa CCM, 
kutopeana mikono na hata kutohudhuria misiba na sherehe zao. Vitendo 
vyao hivi ndivyo vimeasisi chuki ndani ya jamii yetu iliyozoea UPENDO, 
UDUGU, UMOJA NA MSHIKAMANO. Watanzania tunafahamika na tunaona fahari 
kuishi kama ndugu.
Baada ya kitendo hicho cha 
kuwasaliti wapigakura wao kulaaniwa kila kona ya nchi, sasa wamekubali 
kutumiwa kama vibaraka kuichafua taswira ya nchi yetu, nao kwa hila 
iliyo wazi, wamekubali kuwafitinisha watanzania kwa kuandaa maandamano 
ya nchi nzima, yasiyo na ukomo. Hatua hii ni uvunjaji wa katiba ya nchi,
 Sheria na inalenga kuvunja amani, utulivu na mshikamano wa watu wetu.
Ileleweke kwamba, wanachokifanya 
hawa CHADEMA ni kuchochea wananchi kwa makusudi kutotii maagizo halali 
ya vyombo vya dola na Serikali kwa visingizio mufilisi kuwa katika 
Katiba imewapa uhuru huo. Katika haitoi haki na uhuru usio na ukomo. 
Ibara ya 29 (5) inasema;
       “Ila watu wote waweze 
kufaidi haki na uhuru vinavyotajwa na katiba hii kila mtu ana wajibu wa 
kutenda na kuendesha shughuli zake kwa namna ambayo haitaingilia haki na
 uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma”
Baada ya kusema hayo, ninaomba 
CHADEMA wakumbuke na kutilia maanani kuwa kila haki ina wajibu na hakuna
 haki au uhuru usiokuwa na ukomo hususani pale inaposababisha kuingiliwa
 ama kukatizwa kwa haki na uhuru wa watu wengine. Rejea ibara ya 30 (1) 
na (2) ya Katiba.
Ndugu wahabahari,
Mwisho tunatoa pole kwa wenzetu wa
 CUF kutokana na mapambano huko kwao. Tumestushwa sana na yanayoendelea 
huko. CCM inawapa pole na tunawatakia maelewano ili waje tusaidiane 
kuwaletea watanzania maendeleo.
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni