Jumatano, 3 Agosti 2016

MAKALA KUHUSU FALSAFA, DHANA NA UMUHIMU WA MBIO ZA MWENGE WA UHURU

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA WAZIRI MKUU
SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVUFalsafa ya Mwenge wa Uhuru
TZ
Historia ya nchi yetu ni pana na ya kuvutia kwa namna ya pekee ukilinganisha na nchi nyingi za Afrika na Duniani kote. Upekee huu unatokana na uwezo wa kujenga hoja na uadilifu wa viongozi wetu, hasa mwasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipochaguliwa kuwa mjumbe kwenye Baraza la kikoloni la kutunga Sheria (Tanganyika Legislative Council) mwaka 1958.
Kwa kuwa Mwalimu alikuwa na ndoto ya kuiona Tanganyika na Afrika iliyo huru, mwaka 1958 katika hotuba yake ya kwanza alitamka maneno ya kifalsafa kwa wajumbe na Spika wa Baraza la kikoloni la kutunga Sheria kwa kusema “Sisi tunataka Uhuru wa Tanganyika, Mkitupatia tutauwasha Mwenge wa Uhuru na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, umulike ndani na nje na mipaka yetu, ulete tumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo mahali palipo na chuki na heshima palipojaa dharau”.
1Maneno haya aliyarudia tena mwaka 1959 alipohutubia kikao cha 35 cha Baraza la Umoja wa Mataifa kama Mbunge mwakilishi pekee wa Tanganyika.
Falsafa hiyo ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ilikuwa ni kiashiria kikubwa kwa Waingereza kwamba watu wa Tanganyika wamechoka kutawaliwa. Siku Tanganyika ilipopata Uhuru tarehe 09 Desemba, 1961. Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliuwasha Mwenge wa Uhuru na akamkabidhi Luteni Alexander Ngwebe Nyirenda na kikosi cha Vijana wenzake wakaupeleka Mwenge wa Uhuru juu ya Mlima Kilimanjaro.
Mwalimu wakati akitoa hotuba ya siku ya Uhuru; aliwatangazia Watanganyika, Afrika na Dunia kwa ujumla kwa kusema                               “Sisi tumekwisha uwasha Mwenge wa Uhuru na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, umulike ndani na nje ya mipaka yetu, ulete matumaini pale ambapo hakuna  matumaini, ulete upendo mahali penye chuki na heshima mahali palipo jaa dharau”
2Luteni Alexander Nyirenda akipandisha Bendera na Mwenge wa uhuru juu ya mlima Kilimanjaro usiku wa kuamkia tarehe 9 december, 1961
Baada  ya  Uhuru wa Tanganyika na kuwashwa kwa Mwenge wa Uhuru,  Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na viongozi wenzake wa awamu ya kwanza walielekeza juhudi zao katika kuwaunganisha Watanzania na kuweka misingi imara ya kulijenga taifa huru la Tanganyika; kudumisha amani, upendo, umoja, mshikamano na kuweka sera za kukabili  maadui ujinga, umaskini na maradhi.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni