MAKALA KUHUSU FALSAFA, DHANA NA UMUHIMU WA MBIO ZA MWENGE WA UHURU
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA WAZIRI MKUU
SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVUFalsafa ya Mwenge wa Uhuru
Historia
 ya nchi yetu ni pana na ya kuvutia kwa namna ya pekee ukilinganisha na 
nchi nyingi za Afrika na Duniani kote. Upekee huu unatokana na uwezo wa 
kujenga hoja na uadilifu wa viongozi wetu, hasa mwasisi wa Taifa letu 
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alipochaguliwa kuwa mjumbe kwenye 
Baraza la kikoloni la kutunga Sheria (Tanganyika Legislative Council) 
mwaka 1958.
Kwa 
kuwa Mwalimu alikuwa na ndoto ya kuiona Tanganyika na Afrika iliyo huru,
 mwaka 1958 katika hotuba yake ya kwanza alitamka maneno ya kifalsafa 
kwa wajumbe na Spika wa Baraza la kikoloni la kutunga Sheria kwa kusema 
“Sisi tunataka Uhuru wa Tanganyika, Mkitupatia tutauwasha Mwenge wa 
Uhuru na kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, umulike ndani na nje na 
mipaka yetu, ulete tumaini pale ambapo hakuna matumaini, upendo mahali 
palipo na chuki na heshima palipojaa dharau”.
Falsafa
 hiyo ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ilikuwa ni kiashiria kikubwa 
kwa Waingereza kwamba watu wa Tanganyika wamechoka kutawaliwa. Siku 
Tanganyika ilipopata Uhuru tarehe 09 Desemba, 1961. Mwalimu Julius 
Kambarage Nyerere aliuwasha Mwenge wa Uhuru na akamkabidhi Luteni 
Alexander Ngwebe Nyirenda na kikosi cha Vijana wenzake wakaupeleka 
Mwenge wa Uhuru juu ya Mlima Kilimanjaro.
Mwalimu
 wakati akitoa hotuba ya siku ya Uhuru; aliwatangazia Watanganyika, 
Afrika na Dunia kwa ujumla kwa kusema 
                              “Sisi tumekwisha uwasha Mwenge wa Uhuru na
 kuuweka juu ya Mlima Kilimanjaro, umulike ndani na nje ya mipaka yetu, 
ulete matumaini pale ambapo hakuna  matumaini, ulete upendo mahali penye
 chuki na heshima mahali palipo jaa dharau”
Baada
  ya  Uhuru wa Tanganyika na kuwashwa kwa Mwenge wa Uhuru,  Mwalimu 
Julius Kambarage Nyerere na viongozi wenzake wa awamu ya kwanza 
walielekeza juhudi zao katika kuwaunganisha Watanzania na kuweka misingi
 imara ya kulijenga taifa huru la Tanganyika; kudumisha amani, upendo, 
umoja, mshikamano na kuweka sera za kukabili  maadui ujinga, umaskini na
 maradhi.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni