Serikali kuanza kupima utendaji kazi kwa Taasisi za Umma
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO – Dar es Salaam
Serikali imejipanga kuanzisha 
mikataba ya utendaji kazi kwa Taasisi za Umma katika mwaka ujao wa fedha
 kwa ajili ya kuhakikisha watumishi hawafanyi kazi kwa mazoea.
Kauli hiyo imetolewa jana Jijini 
Dar es Salaam na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi 
wa Umma na Utawala Bora Mhe. Angela Kairuki alipokuwa akifanya mahojiano
 kwenye kipindi kinachorushwa na TBC1 cha ‘TUNATEKELEZA’ kinachoelezea 
utekelezaji wa mipango na mikakati iliyowekwa na Wizara yake katika 
kipindi cha Uongozi wa Awamu ya Tano.
Mhe. Kairuki amesema kuwa kwa 
kawaida Watumishi wa Umma hupimwa utendaji kazi wao kwa kujaza fomu za 
wazi zijulikanazo kama ‘OPRAS’ lakini upimwaji huo hauonyeshi utendaji 
wa Taasisi nzima,  hivyo ili kufahamu mipango na malengo ya Taasisi ni 
lazima kuwe na upimaji wa utendaji kazi wa Taasisi nzima.
“Sisi kama Ofisi ya Rais, Utumishi
 wa Umma tumeona kuna haja ya kuwa na mikataba ya kupima utendaji kazi 
wa Taasisi husika ,tumeshakamilisha maandalizi na kila kitu kikienda 
salama mwaka ujao wa fedha tutaanza zoezi hili”, alisema Mhe. Kairuki.
Waziri huyo ameongeza kuwa zoezi 
hilo limeshindikana kuanza mwaka huu wa fedha kwa kuwa bado maandalizi 
yake hayajakamilika na kuongeza kuwa taasisi zote zinatakiwa kupewa 
mafunzo kabla ya kusaini mikataba hiyo.
Amefafanua kuwa Serikali itaingia 
makubaliano kwa taasisi husika kwa kufuata ngazi za uongozi kuanzia kwa 
Mkuu wa Taasisi hadi kwa kiongozi wa juu kabisa wa Wizara husika.
Aidha, Mhe. Kairuki amewakumbusha 
Watumishi wa Umma kuwa kuvujisha nyaraka za Serikali ni kosa la jinai 
hivyo kila mtumishi anatakiwa kuzingatia kanuni za kudumu za Utumishi wa
 Umma ili kuhakikisha wanafanya kazi kwa nidhamu na uwajibikaji wa hali 
ya juu.
“Sheria ya Usalama wa Taifa na 
Sheria inayosimamia masuala ya kumbukumbu za nyaraka Serikalini inasema 
wazi kuwa ni kosa la jinai kuvujisha nyaraka za Serikali kwahiyo natumia
 fursa hii kukemea mtu yeyote mwenye tabia hiyo kwa sababu hatua kali 
zitachukuliwa dhidi yake”, alimalizia Mhe. Kairuki.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni