MHE. AUGUSTINO MREMA AWATAKA WATANZANIA KUYAPUUZA MAANDAMANO YA CHADEMA SEPTEMBA MOSI MWAKA HUU
Na Ismail Ngayonga-MAELEZO
Dar es Salaam
WAZIRI wa zamani wa mambo ya 
ndani ya nchi, Augustino Mrema amewataka Watanzania kuyapuuza 
 maandamano ya Septemba Mosi mwaka huu yaliyoandaliwa na Chama cha 
Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na badala waendelee na shughuli za 
ujenzi wa Taifa.
Mrema alisema hakuna haja ya 
kufanya maandamano Septemba Mosi kwani hayana faida yoyote kwa taifa 
badala yake wananchi wa kawaida ndio watakaoathirika.
Akizungumza katika mahojiano 
maalum na mwandishi wa habari hii leo Jijini Dar es Salaam, Mhe. Mrema 
ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Misamaha kwa Wafungwa 
(Parole) alisema mikutano ya hadhara na maandamano yasiyokwisha kila 
kukicha yatasababisha wananchi wasifanye kazi.
Nchi yetu ni maskini hivyo 
tunahitaji wananchi wafanye kazi kwa bidii” alisema Mrema. Alisema iwapo
 CHADEMA  wataona wameonewa ni vyema  watumie njia za mazungumzo au 
ikibidi kwenda mahakamani badala ya kufanya maandamano ambayo yanaweza 
kusababisha vurugu na kuharibu amani na utulivu wa nchi.
Aliwataka Watanzania kukumbuka 
maandamano ya mwaka 2001 yaliyoitishwa na Chama cha Wananchi (CUF) huko 
Zanzibar ambapo watu kadhaa waliuwawa na mamia kukimbilia uhamishoni 
nchini Kenya na Somalia.
Akizungumzia kuhusu utendaji 
kazi wa Serikali ya Awamu, Mhe. Mrema alimpogeza Rais Dkt. John Pombe 
Magufuli kwa hatua yake ya kurejesha maadili na miiko ya utumishi kwa 
watumishi wa umma nchini hali iliyosaidia kurejesha uwajibikaji wa 
Serikali kwa wananchi.
Mrema alisema tangu kuingia 
madarakani kwa Serikali ya Awamu Tano, kumekuwepo na mabadiliko kwa 
watendaji wa umma katika ngazi mbalimbali za kimamlaka ukitofautisha na 
miaka ya nyuma ambapo baadhi ya watendaji walikuwa wakifanya kazi kwa 
mazoea.
“Viongozi wengi wa umma walikuwa
 wakifanya kazi kwa mazoea bila kujali wajibu wao na wala hakukuwa na 
uwajibikaji cha kusikitisha mamlaka husika zilikuwa haziwachukulii hatua
 za kinidhamu, hivyo viongozi wa umma badala ya kuwatumikia wananchi 
wakawa wanatumikia matumbo yao” alisema Mrema.
Mrema alisema Rais Magufuli 
ameanza kutekeleza kwa vitendo ahadi yake aliyoitoa kwa wananchi ya 
kuwaondoa madarakani viongozi wazembe na wasiowajibika na wasiokuwa na 
uwezo wa kufanya kazi katika kuwatumia wananchi.
Aliongeza kuwa Serikali ya Awamu
 ya Tano inastahili pongezi kwa hatua inazochukua katika mapambano dhidi
 ya vitendo vya rushwa na ufisadi ikiwemo uanzishwaji wa Mahakama ya 
Mafisadi nchini, kwani hakuna maendeleo yatakayoweza kupatikana katika 
nchi pasipo na kupiga vita rushwa.
Mrema alisema ni wajibu wa kila 
mwananchi kuichukia rushwa kwa vitendo ikiwemo kuwafichua hadharani 
kikundi cha watu kinachojihusisha na rushwa kwani kwa kufanya hivyo 
kutasaidia Tanzania kupiga hatua kubwa za maendeleo. 
“Kama mnavyokumbuka mimi 
nilifukuzwa kazi serikalini kwa sababu ya kupinga ufisadi ambao kwa 
wakati ule ulikuwa umekithiri serikali, ivyo nilichokuwa nikikipigania 
mimi ndicho anachifanya Rais Magufuli” alisema Rais Magufuli.
Akizungumzia kuhusu hatua ya 
Serikali ya Awamu ya Tano kuhamishia shughuli zake Mjini Dodoma, Mrema 
alipongeza uamuzi huo kwani kiulinzi na kiusalama Dodoma ni pazuri zaidi
 kuliko Dar es Saalam kwani ni katikati ya nchi.
“Dodoma panafaa sana kiulinzi na
 usalama kwa kuwa ni vigumu kwa adui watoke baharini wafike hadi Dodoma 
kabla hawajathibitiwa” alisema Mrema.
“Kuhusu ubora wa miundombinu ya 
Mkoa wa Dodoma Mrema alisema Mkoa huo unafikika kirahisi zaidi kwa 
wananchi waishio mikoa ya pembezoni na mipakani kufika Dodoma kuliko 
ilivyo Dar es salaam ambayo iko Mashariki kabisa ya nchi”  alisema 
Mrema. 
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni