Mitihani ya Taifa Darasa la 4 na Kidato cha 2 kufanyika kama kawaida
Na: Lilian Lundo – MAELEZO
Wizara ya Elimu, Sayansi na 
Teknolojia inaukumbusha Umma kuwa mitihani ya Taifa ya Darasa la 4 na 
Kidato cha 2 itaendelea kuwepo na mwaka huu itafanyika kama kawaida.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo 
Dkt. Leonard Akwilapo ameyasema hayo leo, jijini Dar es Salaam alipokuwa
 akikanusha taarifa za kutokuwepo kwa mitihani hiyo kwa mwaka 2016.
“Napenda niukumbushe Umma kuwa 
mitihani hii ni muhimu sana katika ufuatiliji wa maendeleo ya wanafunzi 
wetu. Kwa hiyo mitihani yote miwili itaendelea kuwepo na mwaka huu 
itafanyika kama kawaida. Kama kuna watu wanawaambia kuwa haitafanyika 
wawapuuze kabisa,” alifafanua Dkt. Akwilapo
Dkt. Akwilapo aliendelea kwa 
kusema kuwa, mitihani hiyo ina umuhimu mkubwa katika kupima maendeleo ya
 mwanafunzi kwa lengo la kufanya maendeleo ya kitaaluma. Aidha kwa 
wanafunzi ambao watakuwa hawajafikia viwango vya ufaulu vilivyowekwa 
watatakiwa kukariri darasa au kidato.
Amebainisha kuwa Baraza la 
Mitihani ndilo lenye jukumu la kushughulikia maandalizi ya mitihani hiyo
 ikiwa ni pamoja na utungaji, uchapaji, ufungaji na usafirishaji hadi 
ngazi ya Mkoa na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa 
(OR-TAMISEMI) ikiwa na majukumu ya kuhakikisha kuwa uendeshaji na 
usahihishaji wa mitihani hiyo unafanyika kikamilifu.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni