Umoja wa Wanawake Viongozi wa Vyama vya Siasa Tanzania wapinga maandamano ya kuvunja amani
Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake 
Viongozi wa Vyama vya Siasa Tanzania (UWASATA), Cecilia Augustino 
akifafanua jambo wakati alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar 
es Salaam leo, kupinga maandamano ya UKUTA. Kulia ni Katibu wa umoja huo
 Mwajuma Naty na Makamu Mwenyekiti Zaitun Hokororo.
Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa 
Wanawake Viongozi wa Vyama vya Siasa Tanzania (UWASATA), Zaitun Hokororo
 akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.Kulia ni 
Mwenyekiti Cecilia Augustino, Katibu Mwajuma Naty na Mjumbe Ziada 
Athumani.
……………………………………………………………………………..
Hussein Makame-MAELEZO
Umoja wa Wanawake Viongozi wa 
Vyama vya Siasa Tanzania (UWASATA), umepinga maandamano yasiyo na ukomo 
yaliyotanganzwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kwa kuwa 
hayana tija kwa wananchi na Tifa kwa ujumla.
Akizungumza na waandishi wa habari
 jijini Dar es Salaam leo, Mwenyekiti wa umoja huo Cecilia Augustino, 
alisema maandamano hayo yanaashiria uvunjifu wa amani ambayo ni urithi 
wa Taifa la Tanzania.
Alisema wamefikisha tamko lao kwa 
Msajili wa Vyama vya Siasa Jaji Francis Mutungi na kumtaka msajili 
kutoacha chokochocko hizo ziendelee kwani zitasababisha kutoweka kwa 
amani nchini.
“Sisi wanawake viongozi wa vyama 
vya Siasa Tanzania tunapinga azimio la maandamano yasiyo na kikomo 
yanayoandaliwa na chama cha Chadema, hakika maandamano hayo hayana tija 
kwa wananchi na Taifa kwa ujumla” alisema Hokororo na kuongeza:
“Mheshimiwa Msajili, chokochocko 
hizi zinazofanywa na baadhi ya viongozi wa kisiasa zikiachwa tu bila ya 
kukemewa tunaamini tunu yetu ya amani ambayo ni urithi wetu tulioachiwa 
na waasisi wetu itatoweka”
Aliongeza kuwa hatma ya maandamano
 hayo ni kuingia kwenye machafuko na hatimaye mauaji na mateso kwa 
wanawake, watoto na walemavu, mambo ambayo hawatakubali yatokee.
Alibainisha kuwa wanawake viongozi
 wa vyama vya siasa wanaamini kuwa siasa ni kushindana kwa hoja na si 
uvunjifu wa sheria kwa njia ya maandamano yasiyo na tija kwa wananchi na
 Taifa.
Aliliomba Baraza la Vyama vya 
Siasa kuhakikisha linawajibika katika kulinda demokrasia, amani na 
ustawi wa jamii nzima ya Watanzania.
Katika hatua nyingine, umoja huo 
unaojumuisha wanawake viongozi wa vyama 22 vya siasa nchini, umeomba 
kufanya kongamano la amani lenye lengo la kuhamasisha amani na utulivu 
nchini.
Hivyo, Hokororo aliwaomba viongozi
 wakuu wa nchi kuanzia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu 
wa Rais, Waziri Mkuu, wadau wa amani na mashirika binafsi kushirikiana 
na umoja huo kufanikisha kongamano hilo.
“Hakika tunaumia wanasiasa 
wanapokuwa chanzo cha migogoro na vurugu kwa Taifa letu.Hivyo tunamuomba
 Rais wetu tunajua ni msikivu  aweze kuona namna nzuri ya kutafuta 
suluhu ya mgogoro huu wa kisiasa” alisema Mwenyekiti Cecilia Hokororo.
Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji 
Francis Mutungi, tayari ameitisha Baraza la Vyama vya Siasa Agost 31, 
mwaka huu ili kutoa fursa kwa pande vyama husika kukaa meza moja na 
kujadili tofauti zilizopo na kuzipatia ufumbuzi.
Naye Makamu Mwenyekiti wa umoja 
huo Ziada Athumani alisema wanaunga mkono hatua hiyo kwani ndio njia 
muwafaka ya pande husika ili kufikia muwafaka kwa njia ya amani.
Katika mkutano huo na waandishi wa
 habari, wanawake viongozi wa vyama vya siasa waliwakilishwa na wenzao 
kutoka vyama vya Demokrasi Makini, ADA TADEA na Chama cha Umoja wa 
Demokrasi ya Vyama Vingi (UMD).
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni