UGONJWA WA KIPINDUPINDU BADO UPO JIJINI DAR ES SALAAM
Waziri wa Afya, Maendeleo ya 
Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amesema ugonjwa wa 
kipindupindu bado upo jijini Dar es Salaam baada ya wagonjwa wapya wanne
 kugundulika katika Manispaa ya Temeke jijini hapa.
Waziri Ummy ameyasema hayo leo 
ofisini kwake jijini Dar es Salaam, wakati akitoa taarifa kwa waandishi 
wa habari juu ya magonjwa ya milipuko na magonjwa mengine nchini.
Alisema mwenendo wa ugonjwa huo 
kuanzia Julai 2016 ulikuwa wa kuridhisha kwani wagonjwa walipungua hadi 
kufikia 173 kwa mwezi bila kifo kutoka wagonjwa 555 walioripotiwa mwezi 
Juni 2016 na vifo vya watu saba.
“Mkoa wa Morogoro ni mkoa pekee 
umekuwa ukiripoti wagonjwa wa kipindupindu kwa kipindi kirefu hadi 
sasa.Vilivile mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa haujaripoti wagonjwa tangu 
Mei 19, 2016 ila wiki iliyopita siku ya Jumamosi waliripotiwa  wagonjwa 
wapya wanne katika wilaya ya Temeke” alisema Waziri Ummy.
Alisema katika kipindi cha wiki 
iliyopita idadi ya wagonjwa wa kipindupindu imeongezeka hadi wagonjwa 41
 kutoka wagonjwa 30 wa wiki iliyotangulia ingawa hakuna aliyepoteza 
maisha.
“Hivyo kuna dalili za kuwepo tena
 ongezeko la ugonjwa wa kipindupindu jambo ambalo linafanyiwa kazi kwa 
haraka sana na Wizara yangu” alisema.
Alifafanua kuwa Wizara yake 
imeelekeza nguvu kubwa kuendelea kuudhibiti ugonjwa huo hapa Dar es 
Salaam na huko mkoani Morogoro na inafuatilia ugonjwa wa kuharisha 
katika mikoa mingine ili kubaini kama kuna mgonjwa yeyote wa 
kipindupindu na kuudhibiti mapema.
Aliongeza kuwa kikosi kazi cha 
Taifa kinaainisha maeneo makuu ya kuyafanyia kazi mkoani Morogoro ambapo
 yatajumuisha elimu kwa jamii, uvumbuzi wa namna gani ya kupatikana maji
 safi na salama na matumizi vya vyoo bora.
Mbali na kueleza mikakati hiyo, 
Waziri Ummy alisisitiza mikoa na halmashauri zote nchini kuendelea kutoa
 taarifa sahihi na kwa wakati kuhusu ugonjwa huo ili kuweza kuudhibiti 
endapo utabainika kuwepo sehemu yoyote nchini.
Alisema timu ya wataalamu kutoka 
ngazi ya Taifa ilifanya tathmini mnamo Juni, 2016 na kubaini upungufu 
katika utoaji taarifa katika baadhi ya mikoa na hivyo Wizara yake 
inashirikiana na TAMISEMI kuhakikisha inafanyia kazi mapendekezo 
yaliyotolewa.
Ugonjwa wa kipindupindu ulianza 
nchini tarehe 15 Agost mwaka 2015 na hadi kufikia tarehe 31 Julai, 2016 
watu 22,375 wameugua na kati yao wagonjwa 345 walipoteza maisha.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni