Maandamano ya UKUTA hayawezi kufanyika
Maandamano ya UKUTA hayawezekani kwani hii ni ndoto ya mchana na hayana msingi wowote wala tija kwa wahusika hata kwa Taifa.
Hayo yalisemwa na Muhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Prof. Benson Bana katika mahojiano maalum.
“Wanaotaka kuandamana 
wanajidanganya na kuwalaghai wenzao kwani kufanya operesheni ni suala la
 dola na si la mtu au kikundi cha watu, hivyo maandamano hayo 
hayawezekani kabisa, alisema Prof. Bana.
Ameongeza kuwa wanaojiita UKUTA ni
 kwamba Mhe. Rais John Pombe Magufuli amewanyima ajenda kwani utendaji 
wake umezidi fahamu zao na kuwafanya waanze kutapatapa wasijue nini la 
kufanya.
Prof. Bana amesema kama viongozi 
wa UKUTA ni waungwana inabidi watamke wazi kuwa wametafakari na kuona 
kuwa maandamano hayana maana hivyo wameamua kuyasitisha nchi nzima.
Kuhusu utendaji wa Serikali ya 
Awamu ya Tano, Prof. Bana alisema ni Serikali yenye maamuzi ya uhakika 
na inayowajali watu wote bila kujali itikadi zao za vyama, dini wala 
makabila hivyo inabidi watanzania waipende na kuiheshimu.
“Rais Magufuli utendaji wake ni wa
 kuigwa na viongozi wengi Duniani kwani anafanya maamuzi ya uhakika 
ikiwemo kukuza uchumi kwa kukusanya kodi na kuziba mianya ya ubadhirifu 
wa mali ya umma, alisema Prof. Bana.
Pamoja na kuwa Rais Magufuli 
amekuwa madarakani kwa kipindi kifupi, viashiria vyote vinaonyesha kuwa 
ni kiongozi imara na shupavu kutokana na mambo makubwa ambayo ameyafanya
 kwa kipindi hiki kifupi. Katika kipindi hiki kumekuwepo na nidhamu 
katika utumishi wa umma, kodi inakusanywa kwa kiwango kikubwa na elimu 
ya msingi inatolewa bure kama Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala 
inavyosema, alisema Prof. Bana.
Aidha, Prof Bana amesema kuwa 
wanaomlaumu Mhe. Rais ni wale ambao hawajitambui na labda wanaona mianya
 ya ubadhirifu anayoendelea kuiziba, wao wanakosa mapato, vinginevyo 
Rais anafanya vizuri katika kuliongoza Taifa.
“Rais Magufuli yuko sahihi kwa 
jinsi anavyosimamia vipaumbele vya Serikali ikiwemo elimu bure, 
kukusanya kodi na kuzuia mianya ya rushwa pia dhamira ya kuifanya 
Tanzania kuwa na uchumi wa viwanda, alisema Prof. Bana.
Prof. Bana ameelezwa kusikitishwa 
kwake na watu wanaomkosea Rais heshima na kumwita “Dikteta 
Uchwara.”Amesema watu hawa inabidi wazalendo wakemee kabisa vitendo vya 
namna hii ambavyo ni utovu wa nidhamu kwa kiongozi.
Akizungumzia uamzi wa kuhamia 
Dodoma, Prof. Bana alisema kuwa ni uamzi wa busara kutekeleza azma ya 
Serikali ya miaka takribani arobaini iliyopita. Hivyo kuhamia Dodoma 
kutaufanya mji huo kuendelea zaidi kimiundombinu na kiuchumi.
Aliongeza kuwa mikoa ya jirani 
nayo itanufaika kiuchumi kwani itakuwa karibu na makao makuu ya nchi na 
pia kuhama huko kutatoa fursa kwa Dar es Salaam kukua zaidi kibiashara.
Prof. Bana ameitofautisha Serikali
 ya Awamu ya Tano na awamu nyingine nne zilizopita kwa kutokuwa na 
kigugumizi katika kufanya maamuzi yake ikiwemo hii ya kuhamia Dodoma, 
kuondoa wabadhirifu katika utumishi wa umma na kupunguza matumizi yasiyo
 ya lazima na fedha hizo kutumika kwa ajili ya miradi ya maendeleo kama 
afya, elimu na miundombinu.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni