WAZIRI MBARAWA AFUNGUA KOZI MPYA YA MAFUNZO YA WAKUFUNZI WA MARUBANI
Rubani Focus Mmbaga kutoka Chuo 
cha Taifa cha Usafirishaji (NIT), akitoa maelezo ya namna ndege 
inavyoendeshwa kwa kutumia kifaa maalum cha mafunzo ya urubani 
(simulator) kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame
 Mbarawa wakati wa uzinduzi wa mafunzo ya wakufunzi wa marubani 
uliofanyika jijini Dar es salaam.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na 
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akiendesha ndege kwa kutumia kifaa 
maalum cha kufundishia marubani (simulator) kwenye chumba cha mafunzo 
kwenye Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT).
Mkuu wa chuo cha Taifa cha 
Usafirishaji Profesa Zacharia Mganilwa akizungumza na wadau wa sekta ya 
usafiri wa anga (hawapo pichani) katika uzinduzi wa mafunzo ya wakufunzi
 wa marubani uliofanyika jijini Dar es salaam.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na 
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akifafanua jambo kwa wadau wa sekta 
ya usafiri wa anga (hawapo pichani) katika uzinduzi wa mafunzo ya 
wakufunzi wa marubani uliofanyika jijini Dar es salaam.
wadau wa sekta ya usafiri wa anga 
wakimsikiliza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame 
Mbarawa katika uzinduzi wa mafunzo ya wakufunzi wa marubani uliofanyika 
jijini Dar es salaam.
Picha na Wizara ya  Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
…………………………………………………………………
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na 
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amekitaka Chuo cha Taifa cha 
Usafirishaji (NIT), kuhakikisha kinatoa marubani waliobobea katika 
masuala ya usafirishaji wa anga na wenye uadilifu katika taaluma hiyo.
Akizungumza jijini Dar es Salaam 
wakati wa uzinduzi wa mafunzo ya wakufunzi wa kozi za Urubani Chuoni 
hapo, Waziri Prof. Mbarawa amesema kuwa Sekta ya anga ina changamoto ya 
upungufu wa marubani pamoja na uadilifu kwenye sekta hiyo, hivyo 
ameutaka uongozi wa chuo kutoa mafunzo ambayo yatabeba taaluma iliyo 
bora na yenye uadilifu.
“Tunataka kuijenga Air Tanzania 
mpya ambayo ilijengwa kwa misingi ya uadilifu, na  serikali ipo tayari 
kukijengea uwezo chuo hiki ili kitowe marubani waadilifu watakaoweza 
kufufua shirikia letu la ndege”, amesema Waziri Mbarawa.
Profesa Mbarawa amefafanua kuwa 
suala la uadilifu ni la muhimu, hivyo ameutaka uongozi wa Chuo na 
wakufunzi wake kuwa mfano kwa kuonyesha uadilifu ili wanafunzi 
watakaofuzu wawe na tija na uzalendo.
Aidha, amesema kuwa Serikali ina 
mpango wa kukiongezea uwezo chuo kwani lengo ni  kuzalisha wataalamu wa 
usafiri wa anga  ndani ya nchi na si kutegemea nchi nyingine.
“Tunataka marubani waweze kupata 
mafunzo ndani ya Tanzania na ikitokea wameenda nje ya nchi basi iwe 
nikwaajili ya mafunzo maalumu tu” amesisitiza Profesa Mbarawa.
Waziri Profesa Mbarawa amesema 
kuwa kwa kutambua changamoto zilizopo kwenye sekta ya anga, Serikali 
imejipanga kuboresha sekta hiyo kwa kuongeza idadi ya ndege za abiria 
ambapo mbili zimekwisha nunuliwa na mbili nyingine zipo kwenye mchakato 
wakununuliwa ili kuongeza ufanisi wa shirika la ndege nchini.
Amewataka watanzania kuiamini 
Serikali yao kutokana na uamuzi wa ununuzi wa  ndege mpya aina ya 
Bombadiat Q400 kwani Tanzania si ya kwanza kuzitumia bali kuna nchi 
nyingi  zinazotumia ndege hizo ikiwemo Afrika ya kusini, Malawi, Rwanda,
 Ethiopia na Austria.
Kwa upande wake Mkuu wa chuo hicho
 Profesa Zacharia Mganilwa ameiomba serikali kuangalia jinsi ya kuongeza
 mikopo kwa wanafunzi wanaochukua kozi hiyo  kutokana na umuhimu wake 
kwa jamii na Taifa kwa ujumla ili kuwezesha watanzania wengi kupata 
fursa ya mafunzo hayo.
Aidha, uongozi wa chuo hicho 
umeishukuru serikali kwa mpango wake wa uwekezaji mkubwa katika sekta ya
 usafiri wa anga ili iweze kukuza na kuleta ushindani wa usafiri huo 
nchini.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni