SEKTA YA KILIMO YAZIDI KUAJIRI WANAWAKE NA VIJANA NCHINI
Dar es Salaam
SERIKALI imesema sekta ya 
kilimo inaendelea kuwa sekta muhimu katika uchumi wa Tanzania kwa 
asilimia 25% ya pato la taifa na kuajiri asilimia 75% ya watanzania  
wakiwemo wanawake na vijana.
Hayo yamesemwa leo na Mkuu wa 
Kitengo cha Mawasiliano katika Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mifugo 
na Uvuvi, Richard Kasuga wakati wa uzinduzi wa mchezo wa redio uitwao 
KUMEKUCHA unaotarajia kuonyesha mchango wa wanawake na vijana katika 
kutokomeza tatizo la uhaba wa chakula nchini.
Kasuga  amesema kuwa 
igizo hilo la mchezo wa redio, litaakisi umuhimu wa ushirikishwaji wa 
wanawake na vijana katika kukuza sekta ya kilimo na kutoa ujumbe kwa 
vijana kuona umuhimu wa kilimo hasa kilimo cha biashara.
“Sheria na tamaduni zilizopo 
zinakwaza juhudi za mwanamke kupata fursa za kiuchumi kwa sababu hawana 
haki ya kumiliki ardhi au vifaa vya kilimo, vyanzo endelevu vya maji, 
ukosefu wa mikopo ambayo wanahitaji ili kufanikisha juhudi zao”alisema 
Kasuga.
Kwa upande wake mwakilishi 
kutoka shirika la msaada la Marekani (USAID) Randy Chester alisema kuwa 
mchezo wa KUMEKUCHA umeandaliwa na taasisi ya Africa Lead kwa 
kushirikiana na Media for Development International (MFDI) na 
kufadhiliwa na USAID kwa lengo la kupunguza uhaba wa vyakula vyenye 
virutubisho hapa Tanzania.
Mchezo wa KUMEKUCHA ni mchezo 
wa redio wa kila wiki ambao unaangazia maisha, vikwazo na fursa za 
wakulima Tanzania na utaanza kurushwa hewani kuanzia Julai 25, 2016 
kupitia Redio Free Afrika, Redio Abood FM, Redio Ebony FM na Redio Bomba
 FM.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni