Vyuo vikuu vyatakiwa kuunga mkono Serikali katika kujenga Tanzania ya Viwanda
……………………………………..
Waziri wa Elimu, Sayansi na 
Teknolojia Mhe. Prof. Joyce Ndalichako  amevitaka vyuo vikuu Tanzania 
kuunga mkono serikali ya Awamu ya Tano juu ya uanzishwaji wa viwanda 
kuelekea uchumi wa kati.
Prof. Ndalichako ameyasema hayo 
leo katika viwanja vya Karimjee Jijini Dar es Salaam alipokuwa akifungua
 maonyesho ya kumi na moja ya Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia 
yatakayofanyika kwa siku tatu kuanzia leo Julai 20 mpaka Julai 22 mwaka 
huu.
“Vyuo vikuu vinatakiwa kuangalia 
sera za nchi na mwelekeo wa Taifa kuelekea kukuza uchumi wa viwanda kwa 
kuhakikisha wanatoa wataalamu ambao watashiriki katika uchumi wa viwanda
 ambavyo vitaanzishwa nchini,” alifafanua Prof. Ndalichako
Prof. Ndalichako aliendelea kwa 
kusema kuwa Serikali iko katika mkakati wa kuboresha vyuo vya ufundi kwa
 kuanzia na vyuo vitatu vya ufundi vya Dar es Salaam, Arusha na Mbeya 
ili kuboresha mafunzo wanayoyatoa kuendana na uhitaji uliopo katika 
uanzishwaji wa viwanda.
Mbali na hayo, Wizara ya Elimu, 
Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi inashirikiana na Wizara ya 
Viwanda, Biashara na Uwekezaji katika uanzishwaji wa mafunzo katika 
sekta adimu ikiwemo gesi kwa ajili ya kupata wataalamu watakaoajiriwa 
katika viwanda vitakavyo anzishwa. 
Vile vile wanafunzi wanaotarajia 
kujiunga na vyuo vikuu hupewa maelekezo ya namna ya kuomba vyuo kupitia 
Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) pamoja na Baraza la Taifa la Elimu ya 
Ufundi (NACTE) katika maonyesho hayo.
Maonyesho ya Elimu ya Juu, Sayansi
 na Teknolojia hufanyika kila mwaka yakiwa na Lengo la kutoa elimu kwa 
wazazi na wanafunzi wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu hapa nchi waweze
 kujua kozi zinazotolewa katika vyuo hivyo pamoja na maelezo ya kozi 
hizo.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni