RC MKOANI PWANI HANA GARI ALAZIMIKA KUTUMIA LA DC KISARAWE
MKUU wa mkoa wa Pwani pamoja na 
katibu tawala wa mkoa huo hawana usafiri wa uhakika katika kutekeleza 
majukumu yao ya kazi hali ambayo inasababisha mkuu wa mkoa huo kutumia 
gari la mkuu wa wilaya ya Kisarawe ambae bado hajaripoti kazini.
Aidha baadhi ya wakuu wa wilaya 
magari yao ni mabovu ikiwemo gari la mkuu wa wilaya ya Kibaha huku 
maafisa tarafa 26 kati ya 27 waliopo mkoani hapo wanakabiliwa na tatizo 
la kukosa pikipiki wanazotumia kwenye kazi zao.
Akizungumzia changamoto 
zinazoikabili sekretarieti ya mkoa huo,mkuu wa mkoa wa Pwani,mhandisi 
Evarist Ndikilo alisema analazimika kutumia gari la mkuu wa wilaya ya 
Kisarawe kwasasa.
Alielezea kuwa anatumia gari hiyo
 kutokana na mkuu huyo wa wilaya bado hajamwapisha kutokana na kutoa 
udhuru maalum na endapo mkuu huyo wa wilaya ataanza kazi yeye atakuwa 
hana gari la kutumia.
Mbali na hayo ,mhandisi Ndikilo 
alisema wanakabiliwa na changamoto nyingine ya uhaba wa fedha za 
matumizi ya kawaida (OC)ambapo uhaba huo unatokana na kushuka kwa ukomo 
wa bajeti  mwaka hadi mwaka hususan katika mwaka wa fedha 2015/2016 
ulishuka kwa asilimia 40 ikilinganisha na ukomo wa fedha katika kipindi 
cha nyuma.
Alisema fedha pia za matumizi ya 
kawaida zinazopokelewa kila mwezi ni pungufu tofauti na kiasi cha fedha 
iliyopangwa hivyo kuathiri sekretarieti ya mkoa katika kutekeleza 
majukumu yake.
“Changamoto hii ni kubwa ambayo 
inasababisha kuzalisha changamoto nyingine ikiwemo madeni ya watumishi 
ambayo hadi sasa yamefikia mil.152”
“Watumishi hawapati stahiki zao 
kwa wakati na mazingira ya kazi yakikabiliwa na changamoto mbalimbali 
hivyo watumishi wengine wanaamua kuhama na kwenda kufanya kazi kwingine 
ambapo wanafikiri wataweza kutumiwa vizuri na kupata maslahi 
mazuri”alisema mhandisi Ndikilo.
Akizungumzia juu ya upungufu wa 
vitendea kazi alisema pikipiki kwa maafisa tarafa ni tatizo jingine 
ambalo linahitaji kushughulikiwa.
Mhandisi Ndikilo alieleza ni tarafa moja ya Kaskazini Mafia iliyo nzima kati ya maafisa tarafa 27 waliopo mkoani Pwani.
Alisema kuwa maafisa tarafa hao 
ni mkono wa kulia wa wakurugenzi na wakuu wa wilaya ndio wanaochapa kazi
 katika pande hizo lakini hawana usafiri wa uhakika.
Alisema sekretarieti ya mkoa 
,wataalamu na maafisa tarafa hushindwa kutembelea mamlaka za serikali za
 mtaa na maeneo mbalimbali kwa lengo la kufuatilia miradi  na shughuli 
zinazopaswa kufuatilia na hata wakitembelea inakuwa sio kwa kiwango 
kinachotakiwa .
Mhandisi Ndikilo alisema zipo 
hatua wanazozichukua ikiwa ni sanjali na kufikisha changamoto hizo 
katika wizara na idara husika ili ziweze kutafutiwa ufumbuzi.
Hatua nyingine ni madeni ya 
watumishi kufikishwa hazina ili yaweze kulipwa licha pamoja na 
kuwasilisha taarifa hizo lakini hazina bado haijalipa kwa wakati.
Hata hivyo Mhandisi Ndikilo 
alielezea kwamba baadhi ya maafisa tarafa hawana ofisi za kudumu 
wanalazimika kutumia ofisi ambazo hazina hadhi huku kukiwa hakuna huduma
 muhimu za maji na umeme.
Mkuu huyo wa mkoa alisema ofisi ya mkoa imeshajenga ofisi 6 kati ya 27 zinazohitaji kwa maafisa tarafa hao.
Mhandisi Ndikilo aliiomba ofisi 
ya rais ,utumishi wa umma kuangalia kwa ukaribu matatizo hayo ili 
kuyatafutia ufumbuzi kwani ni moja ya sababu zinazokwamisha utekelezaji 
wa ufuatiliaji na jitihada za kuinua maendeleo ya mkoa kwa haraka.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni