TUZILINDE HAKI ZA BINADAMU.
Tanzania
imechukua hatua kadhaa za kulinda na kuhifadhi haki za binadamu nchini.
Hatua hizo zinajumuisha kuridhia mikataba kadhaa muhimu ya Kimataifa na
Kikanda ya haki za binadamu, kuingiza baadhi yake kwenye sheria za nchi
na kuanzisha Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB).
Aidha, Serikali imeendelea kuimarisha Mahakama, Bunge na Vyombo vyote vinavyosimamia utekelezaji wa Sheria nchini.
Kwa mujibu
wa mapendekezo ya Azimio la Vienna la mwaka 1993 na Programu yake ya
utekelezaji, kila serikali ulimwenguni inapaswa kuandaa Mpango Kazi wa
Kitaifa wa Haki za Binadamu, ambapo kwa upande wa Serikali ya Tanzania
iliamua kuanzisha mchakato huu.
Mnamo mwaka
2009, THBUB iliongoza warsha ya Kitaifa ya Mashauriano yenye lengo la
kuandaa Mpango Kazi wa Kitaifa wa Haki za Binadamu ambapo warsha hiyo
ilijumuisha wajumbe mbalimbali kutoka Serikalini, Wanataaluma, Asasi za
Kiraia pamoja na Ofisi ya Umoja wa Mataifa (UN).
Mpango Kazi
huu unajumuisha mapendekezo mengi ya kimataifa na unatoa mwongozo wa
utekelezaji ulio wazi kwa Wizara mbalimbali katika kukuza haki za
binadamu nchini. Unaelezea malengo ya jumla na hatu za msingi
zinazopaswa kuchukuliwa huku ukibainisha Wizara zinazohusika.
Aidha,
Mpango huu unajumuisha Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini (M&E) wenye
viashiria vinavyopimika, ambao pia unaimarisha utekelezaji wa Mpango
Kazi.
Mpango Kazi
huu utaimarisha haki za binadamu nchini Tanzania kupitia baadhi ya
malengo yakiwemo kufanya tathmini kuhusu masuala ya haki za binadamu na
kuandaa mikakati ya kukuza utoaji elimu ya haki za binadamu na kuongeza
uelewa kwa Watanzania wote.
Halikadhalika,
Mpango umebainisha haki 23 zilizoko katika makundi manne ya kimada kama
maeneo ya kipaumbele katika kuimarisha ukuzaji na ulinzi wa haki za
binadamu nchini. Haki na makundi hayo yanajumuisha Haki za kiraia na
Kisiasa, Haki za kiuchumi, Kijamii na Kiutamaduni, Makundi yenye
Mahitaji Maalumu, Kuimarisha Taasisi na Msuala yaliyopo ambapo Tume ya
Haki za Binadamu na Utawala Bora ikisaidiwa na Wizara ya Katiba na
Sheria pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali itafuatilia
utekelezaji wa Mpango huo.
Pamoja na
hayo, haki za binadamu nchini zina changamoto kadha wa kadha zikiwemo;
Uelewa mdogo wa haki za binadamu nchini ambapo bado ni mdogo haswa
katika maeneo ya vijijini ikilinganishwa na maeneo ya mjini na hali hii
inaathiri kiwango cha utoaji taarifa za uvunjifu wa haki za binadamu,
utoaji taarifa wa vyombo vya habari na uwezo wa asasi za kiraia kwa
ujumla.
Changamoto
nyingine ni tabia ya ubaguzi ya baadhi ya watu wanaotoa huduma, Ukatili
dhidi ya wanawake, hatari kwa watu wenye ulemavu wa ngozi na nyinginezo.
Ili
kushughulikia changamoto hizi, Mpango Kazi wa Kitaifa wa miaka mitano wa
Haki za Binadamu 2013-2017 uliozinduliwa Desemba 10, 2013 unaainisha
hatua za kiutendaji zitakazoiwezesha Serikali ya Tanzania kutekeleza
Mikataba ya Kimataifa ya Haki za Binadamu na kuhakikisha kuwa haki za
binadamu zinaheshimiwa nchini kote.
Wakati
Tanzania inaelekea kufanyiwa Tathmini ya Awamu ya Pili na Nchi wanachama
wa Umoja wa Mataifa (UN) juu ya utekelezaji wa haki za binadamu, Asasi
za Kiraia pamoja na Taasisi za kutetea haki za binadamu nchini
zimeendelea kujadili kuhusiana na haki hizo ambapo Waandishi wa Habari
nchini wanaaswa pia kujikita katika kuhabarisha umma kuhusiana na
masuala ya haki hizo hususani masuala ya mauaji ya watu wenye ualbino,
mauaji ya vikongwe, ukatili dhidi ya watoto, pamoja na adhabu ya vifo.
Miongoni mwa
masuala hayo ndiyo yanakamilisha idadi ya mapendekezo 46 yaliyobakia
kusainiwa na Tanzania ambapo Mshauri wa masuala ya haki za binadamu
kutoka Ofisi ya Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, Bi. Chitralekha Massey
anaeleza kuwa, ni vema Tanzania ikakubalina na mapendekezo
yanayohusiana na masuala ya haki za binadamu yanayoendana na Dunia kwa
ajili ya ulinzi wa haki hizo.
“Sisi kama
Umoja wa Mataifa tunapenda kuona Tanzania inafanya uamuzi utakaosaidia
kuboreshwa kwa haki za binadamu nchini kwani ni wakati sasa wa jamii
kusema kwa uwazi kuwa mapendekezo hayo yatakuwa yenye manufaa kwao”,
alisema Massey.
Katika
mkutano na waandishi wa habari uliofanyika hivi karibuni mkoani
Morogoro, masuala ya haki za binadamu yanazungumzwa kwa upana lengo
likiwa ni kuwajengea wanahabari uelewa wa kutosha kuhusiana na masuala
ya haki hizo ili wao waweze pia kuhabarisha umma.
Kamishna wa
Haki za Binadamu na Utawala Bora, Bi. Salma Ally Hassan anatoa rai kwa
waaandishi wa habari huku akiwasisitizia kuwa hawanabudi kujitahidi
kuandika habari kuhusu haki za binadamu kwani kwa kufanya hivyo watakuwa
wameisaidia jamii kupata uelewa wa masuala hayo.
Bi. Salma
alisema kuwa, baadhi ya wanajamii wamekuwa hawazitambui baadhi ya haki
zao hali iliyopelekea kukithiri kwa vitendo vya uvunjifu wa amani
yakiwemo matukio ya mauaji ya watu wenye ualbino, vikongwe pamoja na
ukatili kwa watoto nchini.
Aliongeza
kuwa, baadhi ya watu nchini wamekuwa wakijichukulia sheria mkononi kwa
kuua watu ovyo ambapo watu wenye kuyasemea hayo ni Vyombo vya Habari
lengo likiwa ni kukemea hali hiyo ili vitendo hivyo visiendelee tena
katika jamii.
“Uvunjaji wa
haki za binadamu unafanywa na watu waliomo katika jamii zetu, kwa
mfano, mauaji ya Watu wenye Ualbino, mauaji ya Vikongwe, pale sio
Serikali inakua imevunja haki za binadamu, bali ni watu katika jamii”,
alisema Bi. Salma.
Aidha,
katika warsha hiyo, moja ya mada zilizojadiliwa ni namna gani Vyombo vya
Habari, jamii pamoja na Serikali vinakuwa na jukumu la kulinda haki za
binadamu na kuendelea kukemea matukio yanayovunja amani katika jamii.
Ikumbukwe
kuwa, tarehe 9 Mei, 2016 Tanzania inatarajiwa kufanyiwa tathmini ya pili
juu ya hali ya haki za binadamu nchini na Nchi Wanachama wa Umoja wa
Mataifa ambapo tayari Asasi za Kiraia na Watetezi wa haki za binadamu
wamekwisha wasilisha mapendekezo yao kwa Wawakilishi wa nchi wanachama
wa umoja huo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni