TTCL YAZINDUA NEMBO MPYA NA HUDUMA YA 4G LTE
Waziri
 wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akizungumza 
na wafanyakazi wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), na wadau wa Sekta ya 
Mawasiliano (hawapo pichani), wakati uzinduzi wa nembo mpya ya kampuni 
hiyo na huduma ya 4G LTE jijini Dar es Salaam.
Mjumbe
 wa Bodi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), Bi. Edwina Lupembe 
akifafanua jambo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa 
Makame Mbarawa, katika hafla ya uzinduzi wa nembo mpya ya kampuni hiyo 
na huduma ya 4G LTE
Afisa
 Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), Dkt. Kamugisha 
Kazaura akielezea mafanikio ya TTCL kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na 
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (hayupo pichani), katika hafla ya 
uzinduzi wa nembo mpya ya kampuni hiyo na huduma ya 4G LTE jijini Dar es
 Salaam.
Waziri
 wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akizindua 
nembo mpya ya Kampuni ya Simu ya Tanzania (TTCL), jijini Dar es Salam.
Waziri
 wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akijadiliana 
jambo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), Dkt. 
Kamugisha Kazaura, wakati wa halfla ya uzinduzi wa nembo mpya ya kampuni
 hiyo na huduma ya 4G LTE jijini Dar es Salaam.
Baadhi
 ya Wafanyakazi wa Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), wakifatilia sherehe 
za uzinduzi wa nembo mpya ya kampuni hiyo na huduma ya 4G LTE jijini Dar
 es Salaam.
…………………………………………………………………………………
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na 
Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amewataka wafanyakazi wa Kampuni ya 
Simu ya (TTCL), kuwa wabunifu ili kuhimili ushindani wa soko katika 
sekta ya mawasiliano na hivyo kuiwezesha kampuni hiyo kupata faida.
Akizungumza wakati akizindua 
nembo mpya ya kampuni ya TTCL na huduma ya 4G LTE inayowezesha huduma ya
 mawasiliano ya sauti na data kwa haraka Prof. Mbarawa amesema huu ni 
wakati wa kubadili mtazamo na kufanya kazi kisasa ili kuvutia wananchi 
kutumia huduma za TTCL.
“TTCL lazima mubadilike ili 
muweze kuendana na kasi ya mabadiliko ya sayansi na teknolojia na hivyo 
kumudu ushindani uliopo sasa katika sekta ya mawasiliano”, amesema 
Waziri Prof. Mbarawa.
Amewataka TTCL kuhakikisha kituo mahiri cha kutunzia taarifa (Data Centre), kinaanza mapema mwezi Juni ili kuwezesha wadau wengi kunufaika na kituo hicho.
Prof. Mbarawa amesema Serikali 
inaunga mkono TTCL na imetenga masafa ya 800 MHZ ambayo yataiwezesha 
TTCL kushindana na makampuni mengine ya watoa huduma ya mawasiliano na 
kuwaunganisha wateja wengi kutumia huduma za mawasiliano na data.
“Uzinduzi wa nembo mpya ya TTCL 
na huduma ya masafa ya 4G LTE uendane na ubunifu kwa wafanyakazi ili 
muwavutie watumiaji wengi wa simu na hivyo kupata soko kubwa na kuifanya
 TTCL kuchangia kikamilifu pato la taifa”, amesisitiza Waziri Mbarawa.
Prof. Mbarawa amesema mawasiliano
 ni kiungo muhimu cha kufanikisha ukuaji wa sekta za kilimo, taasisi za 
fedha, uwekezaji, ujasiliamali na utendaji kazi wa Serikali na sekta 
binafsi hivyo ubunifu katika utendaji utaiwezesha TTCL mpya kufikia 
malengo yaliyokusudiwa.
Katika hatua nyingine Prof. 
Mbarawa amewataka wananchi kuzingatia maelekezo wanayopatiwa na Mamlaka 
ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), kuhusu namna ya kuzitambua simu na vifaa
 feki na hatua za kufuata ili ifikapo Juni 16 zoezi la kuzifunga simu 
feki litakapotekelezwa wasiathirike.
Kwa upande wake Mwakilishi wa 
Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL Bi. Edwina Lupembe amesisitiza kwamba TTCL 
imejipanga kuboresha huduma za fedha ili kuwezesha watumiaji wengi wa 
kampuni hiyo kunufaika na huduma ya kutuma na kupokea fedha.
“Tumekamilisha mradi mkubwa wa 
kusimika mitambo ya GSM, UMTS na LTE ambayo itakuwa na uwezo wa kutoa 
huduma ya mawasiliano 2G, 3G na 4G”, amesema Bi. Lupembe
Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa TTCL 
Dkt. Kamugisha Kazaura amemhakikishia Waziri Mbarawa kuwa mabadiliko ya 
muonekano wa TTCL yataendana na mtazamo mpya wa wafanyakazi wenye lengo 
la kuiwezesha kampuni hiyo kuwa ya kisasa hapa nchini.
Amesema TTCL imejipanga kuboresha
 simu za mezani, mkononi, na huduma za intaneti ya haraka ili iweze 
kupata wateja wengi na hivyo kuongeza mapato yake.
“Teknolojia ya 2G GSM, 3G UMTS na
 LTE imeongeza nguvu kwa kampuni yetu kuleta ushindani katika soko la 
mawasiliano na zitaendelea kuongeza ufanisi na ubunifu wa huduma zetu 
kwa bei nafuu”, amesisitiza Dkt. Kazaura.
Tayari huduma ya 4G LTE inapatikana katika maeneo mengi ya Ilala, Temeke na Kinondoni jijini Dar es Salaam.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni