Ijumaa, 20 Mei 2016

MKUU WA WILAYA WETE PEMBA ALAANI VITENDO VYA HUJUMA MALI ZA WANANCHI KWA MISINGI YA KISIASA

????????????????????????????????????
 
SERIKALI ya Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba  imelaani  vikali  vitendo vya hujuma vinavyofanywa na baadhi ya wananchi kwa kuhujumu mali za wengine kwa misingi ya kisiasa .
Akizungumza kwa nyakati tofauti baada ya kutembelea maeneo yaliyohujumiwa , Mkuu wa Wilaya ya Wete Rashid Hadid Rashid amevitaka vyombo vya ulinzi kuhakikisha wanaohusika wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria .
Amesema serikali haitavifumbia macho vitendo hivyo ambavyo vinaweza kusababisha kutoweka kwa amani na utulivu uliopo hapa nchini .
Maeneo ambayo yamehujumiwa ni pamoja na bonde la Chwangayo na Mburani Shehia ya  Mtambwe kaskazini pamoja na Shehia ya Pembani ambapo  wakulima wamepata hasara kubwa kutokana na hujuma hizo.
“Serikali ya Wilaya inakilaani vikali kitendo hichi cha kuhujumu mali za wananchi kutokana na misingi ya kisiasa , tunaahidi kuwasaka wahusika wote na tutawafikisha mahakamani ”alieza Mkuu wa Wilaya .
Katika bonde hilo jumla ya mikarafuu 16 ya daraja la pili ambayo ilikuwa tayari kuzaa pamopja na nusu ya shamba la muhogo limehujumiwa na watu wasiojulikana.
Mmoja wa wakulima katika bonde hilo Bakar Mwitani Sheha amesema kuwa uharibifu katika shamba lake ameubaini baada ya kufika katika aneo hilo kwa ajili ya kupata mahitaji ya chakula.
Alisema baada ya kubaini hali hiyo , alitoa taarifa Ofisi ya sheha , Ofisi ya Wilaya pamoja na kutoa taarifa katika vyombo vya ulinzi kwa hatua zaidi .
Maeneo mengine ni shamba la mwakilishi wa jimbo la Mtambwe Bi Khadija Omar Kibano na Saleh Khamis Ahmed  ambao mashamba yao ya mpunga yamefyekwa pamoja na Said Khamis Mohammed na Mariam Suleiman Makame  walioharibiwa vipando vya mihogo , migomba , viazi , kubomolea nyumba yake pamoja na kuibwa mali ghafi katika kiwanda cha uchongaji huko Pembeni
Naye  Said Khamis Mohamed wa Shehia ya Pembeni anayemiliki kiwanda cha kuchonga ambaye amebomolewa baadhi ya kuta za nyumba yake , kung’olewa vipando katika Shamba lake pamoja na kuchukuliwa samani (funiture) zake alisema vitendo hivyo vimeathiri biashara yake .
Alisema kwamba tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa nane za usiku baada ya kutoka tangazo kupitia mskitini lililowataka wananchi wote wa Shehia hiyo kukutana , na baada ya hapo kundi la watu walivamia na kutekeleza hujuma hizo .
“Nikiwa nyumbani nilisikia  tangazo likiwataka wananhi wote wa Shehia kukutana sokoni , na baada ya muda nilivamiwa na kundi la watu na kuanza kuchuma machungwa na kisha kuutaka mchungwa , kuvunja baadhi ya kuta katika nyumba yangu pamoja na kung’owa vipando katika shamba langu ”alifahamisha.
Akitoa tathmini ya hasara iliyotokea katika maeneo hayo , Afisa maendeleo ya Kilimo Wilaya ya Wete Makame Hamas Said alisema ni shilingi milioni 7,439,500 /= .
Hadi sasa hakuna mwananchi aliyekamatwa na vyombo vya ulinzi akihusishwa na vitendo hivyo ambapo jeshi la Polisi limeahidi kuwasaka na kuwafikisha mbele ya mikono ya sheria.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni