MAJALIWA:VITA DHIDI YA RUSHWA SI NGUVU YA SODA
 WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema vita inayoendeshwa na Serikali ya 
awamu ya tano dhidi ya wala rushwa na wale wanaofanya ufisadi siyo nguvu
 ya soda kama wengi wanavyofikiri.
“Serikali ya awamu ya 
tano imedhamiria kupambana na wala rushwa na mafisadi. Wala hatutanii. 
Hawa tutacheza nao na wala wasidhani vita hii ni nguvu ya soda. 
Tutaendelea kuwasaka hadi tufike mwisho,” alisema Waziri Mkuu wakati 
akizungumza na Watanzania waishio Zambia katika mkutano uliofanyika 
kwenye Ubalozi wa Tanzania jijini Lusaka, Zambia juzi jioni (Jumanne, 
Mei 24, 2016).
“Hatutaki tabia 
iliyokuwepo ya mwananchi anakuja ofisini kutaka huduma lakini 
hasikilizwi hadi atoe chochote, sisi hiyo tabia hatutaki kuisikia 
kabisa. Tumedhamiria kurudisha heshima kwenye utumishi wa umma na 
nimeanza kupata faraja kwani sasa hivi (nimeambiwa) katika baadhi ya 
taasisi unasikia mtu akiulizwa una shida gani, nenda pale, jambo ambalo 
zamani halikuwepo,” alisema.
Alisema Serikali 
imeamua kupigia debe dhana ya utumishi wenye uadilifu kwa sababu huo ni 
utamaduni mpya. “Ni kipindi kigumu kidogo cha mabadiliko lakini 
tumesimamia mabadiliko haya na ndiyo maana watumishi wote 
tumewasisitizia kuwa suala la uaminifu, uadilifu na uwajibikaji ni 
muhimu,” alisema na kuongeza:
“Hatutamvumilia 
mtumishi yeyote ambaye hatakuwa tayari kuwatumikia Watanzania au 
atakayeendekeza uzembe lakini pia hatutamuonea mtu yeyote. Hapa 
tunasisitiza usawa na hatutaki kutengeneza gap kati ya mwananchi 
mtumishi na wa mwananchi wa kawaida, tunataka kila mwananchi aione 
Tanzania ni nchi yake na kila kinachozalishwa ni sehemu yake. Tukifika 
hapo, tunaamini kila mmoja ataweza kuisemea nchi yake.”
Akizungumzia kuhusu 
ubadhirifu wa fedha za umma, Waziri Mkuu alionya kwamba Serikali imelipa
 kipaumbele suala la uaminifu na uadilifu kwenye fedha za Serikali na 
kwamba haitakuwa tayari kuona fedha hizo zikifujwa.
“Hivi sasa Serikali 
imetenga fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo na fedha hizo 
zitaenda vijijini. Tunataka zikafanye kazi iliyokusudiwa, na wale 
wadokozi wajue kuwa wamekalia kaa la moto,” alisema huku akishangiliwa.
Alisema watumishi wa 
umma wana wajibu wa kusimamia kazi zilizopangwa na kuhakikisha miradi 
iliyolengwa inakamilika. “Kama fedha zimeletwa kujenga zahanati simamia 
zahanati ijengwe na ni lazima zahanati hiyo ionekane,” alisema.
Alisema bajeti ya mwaka
 huu imeongezeka kutoka sh. trilioni 21 hadi trilioni 29 lengo kuu 
likiwa ni kuleta maendeleo kwa wananchi. “Ndiyo maana tumepandisha 
bajeti ya maendeleo kutoka asilimia 27 hadi asilimia 40. Ole wake 
atakayepokea fedha hizi halafu zisifanye kazi yake, ukiipoteza wewe 
utafute njia ya kwenda,” alisema huku akishangiliwa.
Akifafanua zaidi, 
Waziri Mkuu alisema vita inayoendeshwa imelenga kuifanya Tanzania 
ibadilike na itoke kwenye uchumi wa chini na kuingia uchumi wa kati. 
“Swali la msingi ni je tunafikaje hapo? Jibu ni kupitia uzalishaji wa 
bidhaa viwandani,” alisema.
“Nyote ni  mashahidi wa
 jinsi ambavyo shilingi yetu imekuwa ikishuka thamani kulinganisha na 
dola ya Marekani. Tulitoka sh. 1,600/-, tukapanda hadi sh. 1,900/- na 
sasa tumefikia sh. 2,180/-. Hii ni kwa sababu tunaagiza zaidi bidhaa 
kutoka nje ya nchi badala ya kuzalisha, hatuwezi kuendelea hivi na ndiyo
 maana tumeamua kuwa nchi ya viwanda. Leteni mitaji nyumbani muwekeze,” 
alisisitiza.
Akijibu swali kuhusu 
Serikali kutafuta njia ya kutoa mikopo kwa Watanzania waishio nje ya 
nchi, Waziri Mkuu alisema mkopo ni mkataba kati ya taasisi ya kifedha na
 mkopaji kwa hiyo Serikali haiwezi kubeba dhamana hiyo. “Benki wanataka 
ijue taarifa zako mkopaji, wanataka wajua dhamana zako ni zipi, 
wajiridhishe na shughuli unazofanya. Je panakopesheka hapo?,” alihoji.
Hata hivyo, aliwaeleza 
kwamba wakitaka kuwekeza nyumbani wanaweza kupata mikopo kutoka benki ya
 maendeleo ya kilimo (TADB), Benki ya Rasilmali (TIB Corporate na TIB 
Development). “Hizi benki ni za wakulima na wajasiriamali, na zina 
masharti yake, kwa hiyo ni lazima wakakague eneo lako au mahali 
unapofanyia biashara au wakague leseni yako na ukweli wa maombi 
uliyopelekea. Sasa ukiwa Zambia watawezaje kukukopesha? Kwa hiyo ukitaka
 fedha uwe nyumbani,” alisema.
Akijibu swali ni vipi 
Serikali itawasaidia wanadiaspora kupiga kura kwenye uchaguzi mkuu 
wakiwa nje ya nchi, Waziri Mkuu alisema Serikali haijawahi kujaribu 
jambo hilo licha ya kuwa ilikwishapokea mapendekezo kadhaa kutoka nchi 
mbalimbali lakini kwa vile wameliuliza, yeye analibeba na kwenda 
kulifanyia kazi.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni