SERIKALI KUTOA MAFUNZO MAALUM YA ELIMU YA FEDHA KWA WANANCHI
By Newsroom on May 20, 2016
Wizara ya Fedha na Mipango 
imesema kuwa  iko tayari kutoa mafunzo maalum ya elimu ya fedha kwa 
wananchi wote wakiwemo wakinamama kuhusu ili kuleta uelewa mpana wa 
upatikanaji wa huduma za fedha na taratibu zinazohusu mikopo.
Kauli hiyo imetolewa leo mijini
 Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kachwamba Kajaji
 wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Anna Lupembe 
aliyetaka kujua mipango ya Serikali ya kupeleka huduma za kibenki 
vijijini ili wanawake waweze kupata mikopo.
Aidha, alisema kuwa Wizara ya 
Fedha na Mipango kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imehakikisha kuwa 
huduma za kibenki zinawafikia wananchi wengi ili kurahisisha shughuli 
zao mbalimbali za kiuchumi katika maeneo ya mjini na vijiji.
Alisema kuwa baadhi ya Benki 
zimeanzisha huduma za Kibenki kupitia mawakala, na huduma za kifedha 
kupitia simu za mikononi ambazo zimewasaidia wananchi kwenye sehemu 
ambako hakuna matawi ya Benki.
Mhe. Dkt.Kajaji aliongeza kuwa 
 Wizara ya Fedha na Mipango kupitia Benki Kuu inaendelea kuweka 
mazingira wezeshi ili kusaidia nguvu za wananchi na sekta binafsi 
kuanzisha benki au taasisi za fedha.
Alitoa wito kwa wananchi 
kutumia fursa ya mazingira mazuri ya uwekezaji yaliyopo hapa nchini 
kuzishawishi Benki kuanzisha huduma za kibenki katika maeneo yao.
Mhe. Dkt.Kajaji alisema kuwa 
Wizara ya Fedha na Mipango itaendelea kushawishi Benki nchini kupanua 
shughuli zao ili ziwafikie wananchi wengi hasa wale wa vijijini wakiwemo
 akina mama.
Aidha, Naibu Waziri huyo 
alisema kuwa Serikali kwa kushirikiana na BOT iko tayari kutoa mafunzo 
maalum ya elimu ya fedha kwa wananchi wote wakiwemo wakinamama kuhusu 
utumiaji wa huduma za kifedha ili kuleta uelewa mpana wa upatikanaji wa 
huduma za fedha na mikopo.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni