RAIS FIFA GIANNI INFANTINO AIPONGEZA YOUNG AFRICANS
Rais
 wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Gianni Infantino, 
ameipongeza timu ya soka Young Africans ya Dar es Salaam, kutwaa ubingwa
 wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara 2015/16.
Young Africans imetwaa ubingwa huo
 kwa msimu wa pili mfululizo, lakini ikiwa ni mara ya 26 tangu kuanza 
kwa Ligi Kuu Bara mwaka 1965.
Katika salamu zake, kupitia barua 
yake ya Mei 18, 2016 kwa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), 
Jamal Emil Malinzi, Infantino ameelezea ubingwa wa Young Africans kwamba
 umetokana na kazi kubwa inayofanywa na uongozi wa timu hiyo, makocha, 
wachezaji pamoja na mashabiki.
“Yanga ndiyo mabingwa wa Tanzania.
 Napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza Young Africans na timu nzima 
isiyoshindika kwa mafanikio haya makubwa. Taji la Young Africans ni 
matokeo ya mshikamano ulioko ndani ya Young Africans,” amesema Infantino
 katika barua hiyo yenye kichwa cha habari kinachosema: Salamu za 
Pongezi kwa Young Africans.
Amesema pongezi zake ziende kwa 
uongozi wa klabu, makocha na benchi nzima la ufundi, wachezaji, 
madaktari pamoja na mashabiki wote wa Young Africans.
“Kwa niaba ya familia ya soka, 
napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru Young Africans na Shirikisho la 
Soka Tanzania (TFF) kwa jinsi mnavyopeleka ujumbe chanya wa soka kwa 
jamii ya michezo,” alisema Infantino katika barua hiyo iliyotua TFF Mei 
21, mwaka huu.
Tayari Rais wa TFF, Jamal Malinzi 
alikwisha kuipongeza Yanga ambayo imepewa Kombe na medali kwa wachezaji 
24, viongozi saba wa benchi la ufundi na viongozi wanne wa Kamati ya 
Utendaji na kwa sasa wanasubiri zawadi ya fedha Sh 81,345,723.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni