TBC yafanikiwa kufanya upembezi yakinifu wa kufunga mitambo ya FM eneo la Mbambabay.
SHIRIKA la 
Utangazaji la Taifa (TBC) limefanya upembuzi yakinifu wa kufunga mitambo
 ya FM yenye uwezo wa Kilowati moja katika eneo la Mbambabay Wilayani 
Nyasa Ili kuongeza usikivu wa Redio za TBC.
Kauli hiyo 
imetolewa leo Bungeni Dodoma na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na 
Michezo, Mhe. Nape Nnauye wakati akijibu swali la Mbunge wa Mbinga 
Vijijini, Mhe. Martin Msuha aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa 
kuongeza uwezo wa kurusha matangazo ya Kituo cha TBC Songea ili wananchi
 wa tarafa hizo wapate habari kupitia TBC.
Mhe. Nape ameeleza kuwa Matangazo ya Redio ya Taifa kupitia mtambo wa masafa ya kati yaani ‘’Medium Wave’’
 wenye nguvu ya Kilowati 100 yalikuwa yakisikika vizuri katika Wilaya 
mbalimbali za Mkoa wa Ruvuma wakati mtambo huo ulipokuwa ukifanya kazi.
‘’Tangu mwezi 
Julai, 2013 mtambo huo haufanyi kazi kutokana na uchakavu na hivyo 
kuathiri usikivu wa matangazo ya TBC katika maeneo kadhaa”, alisema Mhe.
 Nape.
Alisema kwamba,
 kwa kutambua umuhimu wa Wananchi katika kupata matangazzo, TBC 
ililazimika kuhamisha mitambo yake miwili ya Redio yenye uwezo wa 
Kilowati moja kwa kila moja iliyokuwa imefungwa eneo la Mshangano, 
Songea na kuifunga eneo la juu la mlima wa Matogoro-Songea ili usikivu 
Wake usambae katika eneo kubwa zaidi.
‘’Baada ya kufunga mitambo hiyo, matangazo ya TBC Songea yameboreshwa”, aliongeza Mhe. Nape.
Ameongeza kuwa 
katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2016/17 Wizara yake imetenga fedha za 
maendeleo kwa ajili ya kufunga mtambo eneo la Mbambabay.
‘’Kazi hiyo ya 
uboreshaji wa matangazo katika eneo Hilo itaanza mara tu fedha za 
kununua na kufunga mitambo hiyo zitakapotolewa”, alisema Mhe. Nape.
Aidha, alisema 
kwamba kutokana na uwezo mdogo wa mitambo ya FM inayotumika kwa sasa, 
mawimbi yake ya sauti hayafiki mbali sana ukilinganisha na yale ya 
mitambo ya ‘’Medium Wave’’ iliyokuwa ikitumika awali ambayo yanafika eneo kubwa zaidi la Mkoa wa Ruvuma zikiwemo Tarafa za Hagati, Mbuji na Mkumbi.
‘’Kukabiliana 
na changamoto za usikivu hafifu katika maeneo kadhaa Mkoani Ruvuma, TBC 
imeshafanya upembuzi yakinifu wa kufunga mitambo ya FM yenye uwezo wa 
Kilowati moja katika eneo la Mbambabay Wilayani Nyasa Ili kuongeza 
usikivu wa Redio za TBC,”alisema Mhe. Nape.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni