WAZIRI MKUU AKAGUA UTENDAJI KAZI MABASI YA DART
…………………………………………………………………………………………………………………
*Ataka watu walipe tiketi rasmi, wafuate taratibu
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa 
amekagua utendaji kazi kwenye mabasi ya mwendokasi yanayotoa huduma 
katika Jiji la Dar es Salaam na kubaini changamoto kadhaa ambazo amesema
 zitarekebishwa kadri mradi unavyoendelea.
Waziri Mkuu ambaye alilipa nauli 
na kupanda basi namba 23 lenye usajili namba T125 DGW kuanzia kituo cha 
Ferry, Kivukoni, ametumia muda wa dakika 50 kufika Kimara mwisho kwa 
kutumia usafiri huo.
Waziri Mkuu alipanda basi hilo 
saa 3:30 asubuhi na lilianza safari saa 3:33 baada ya kusubiri wengine 
wapande. Kwa wastani ililtumia kati ya dakika mbili hadi tatu kutoka 
kituo kimoja hadi kingine. Basi hilo liliwasili Kimara Mwisho saa 4:23 
asubuhi.
Akizungumza na waandishi wa 
habari akiwa Kimara mwisho mara baada ya kumaliza ziara hiyo fupi ya 
ukaguzi leo (Ijumaa, Mei 27, 2016), Waziri Mkuu alisema aliamua kufanya 
ziara hiyo ya ghafla ili kuangalia matumizi ya njia za mabasi yakoje na 
pia kuona abiria wanaelewa vizuri namna ya kuitumia huduma hiyo.
Amesema ameridhishwa na mradi 
unavyofanya kazi ila ameelezwa kuna usumbufu kwenye mageti wakati abiria
 wanapotaka kuthibitisha tiketi zao hasa wakati wa asubuhi kunapokuwa na
 msongamano wa abiria. Pia alielezwa kwamba kuna baadhi ya abiria 
wanakuja na tiketi za jana yake jambo ambalo linaleta usumbufu kwa 
sababu hazitambuliki kwenye mfumo wao.
“Nimeridhishwa na uharaka wa njia
 kwa sababu na mimi mwenyewe nimetumia dakika 50 kufika hapa ingawa kuna
 maeneo nimeona kuna haja ya kuwa na taa maalum za kuzuia magari 
(special sensors) wakati mabasi yakipita ili kuepusha ajali,” alisema.
Aliyataja maeneo hayo kuwa ni 
kwenye makutano ya barabara ya Morogoro na mtaa wa Samora, Morogoro na 
Jamhuri na makutano ya Morogoro na Kisutu.
Waziri Mkuu aliwataka Watanzania 
waende na tiketi rasmi badala ya kutumia tiketi za jana kwa sababu 
kufanya hivyo ni makosa na  mtu anakuwa amedhamiria. “Hawa watachukuliwa
 hatua za kinidhamu. Mtu akija na tiketi ya jana akamatwe na kupelekwa 
polisi, huyu atakuwa amedhamiria,” alisema Waziri Mkuu wakati akiongea 
na mhudumu mmoja katika kituo cha Kimara Mwisho.
“Ninawasihi wananchi wanaotumia 
usafiri huu wajifunze kufuata utaratibu na kuwasisitizia kuwa kila 
abiria aje na tiketi ambayo ni rasmi,” alisema na kuongeza: “Haya mabasi
 nimebaini yako vizuri. Ninatoa msukumo kwa watumishi wa umma wapande 
mabasi haya ili kupunguza msongamnao wa magari barabarani.”
Katika kupiunguza baadhi ya 
changamoto, Waziri Mkuu alisema Serikali itasimamia uboreshaji wa 
ukataji tiketi ili kuondoa usumbufu kwa abiria. Pia alivionya vyombo vya
 moto viache kutumia njia maalum ya mabasi hayo.
Pia aliwataka polisi wanaofanya 
doria za usiku kupita kwenye fly-overs na kuwaondoa watu wanaolala 
kwenye maeneo kwani wanahatarisha usalama wa watu wanaotumia njia hizo. 
“Zile siyo sehemu za kulala, wanaofanya hivyo wanahatarisha usalama wa 
watumiaji wa njia hizo, kwa hiyo polisi wakiwakuta watu wa aina hiyo 
wawakamate mara moja,” alisema.
Kwa upande wake, Kamanda wa 
Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Mohammed Mpinga ambaye alifuatana 
na Waziri Mkuu kaktika ziara hiyo, alisema amepiga marufuku magari na 
pikipiki kutumia njia hiyo hata kama ni magari ya Serikali.
“Tulishapiga marufuku magari na 
pikipiki kutumia njia hiyo hata kama ni magari ya Serikali, ninawasihi 
madereva watambue hili na watii,” alisema.
Machi 22, mwaka huu Waziri Mkuu 
alitembelea soko la Feri kwa lengo la kuangalia mfumo wa majiko ya gesi 
sokoni hapo (kuzuia moshi) na kukagua ujenzi wa ukuta unaotenganisha 
soko hilo na mabasi yaendayo kasi.
Aprili 15, mwaka huu, Waziri Mkuu
 alifanya kikao na kuwaagiza wakuu wa taasisi zinazohusika na 
utekelezaji wa mradi huo kuhakikisha wanatoa elimu kwa umma ili 
kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza pindi majaribio yakianza.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni