NECTA SASA KUFUNGA MITIHANI KWA KUTUMIA MASHINE.
Baraza la Mitihani la Tanzania 
(NECTA) limejipanga kuanza kufunga bahasha zenye karatasi za mitihani 
kwa kutumia mashine maalum ili kuondokana na hatari ya kuvuja kwa 
mitihani hiyo na gharama za ufungaji wa mitihani kwa kutumia mikono.
Hayo yamebainishwa na  Waziri wa 
Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako  wakati 
akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara yake kwa mwaka 
2016/2017, jana Bungeni Mjini Dodoma. 
Prof. Ndalichako alisema kuwa 
katika kuimarisha utendaji kazi wake NECTA itanunua mashine mbili za 
kufunga mitihani (Auto Poly Wrapping and Packing Machine) ili kuimarisha
 usalama wa mitihani kwa kupunguza watu wanaoshiriki kwenye maandalizi 
ya mitihani hiyo.
“Katika mwaka 2016/2017 Baraza 
litasimika mashine mbili za kufunga bahasha za mitihani hivyo kuondoa 
hatari zinazoweza kujitokeza kwa kuwa idadi ya watu wanaofanya kazi hiyo
 itapungua.” alisema Prof. Ndalichako.
Aidha, Prof. Ndalichako aliongeza
 kuwa Baraza litaboresha mfumo wake wa ukusanyaji na uchakati takwimu na
 kuweka Mfumo wa Kielektroniki wa kumtambua mwanafunzi kwa namba maalum 
tangu anapoandikishwa shuleni hadi atakapomaliza mzunguko wa masomo 
yake.
Alisema kuwa mfumo huo wa 
utambuzi utaunganishwa nchi nzima ili kuwezesha kufuatilia maendeleo ya 
mwanafunzi kwenye shule yoyote atakayoenda kusoma ndani ya nchi kwa kuwa
 namba hiyo atakayopewa na Baraza ataitumia hata kwenye shule nyingine 
atakazohamia.
“Wizara itaweka Mfumo wa 
Kielektroniki wa ukusanyaji taarifa za wanafunzi chini ya Baraza la 
Mitihani ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa hizo wakati wa mitihani 
na utaratibu huu utapunguza matumizi makubwa ya fedha kupitia mfumo wa 
TSM9.” alisema Prof. Ndalichako.
Pia alieleza kuwa katika 
kufanikisha Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN), mwaka wa fedha 
uliopita Mamlaka ya Elimu Tanzania imechapisha vitabu 558,720 vya jinsi 
ya kujibu mitihani ya Kidato cha Pili na Kidato cha Nne ili kuwawezesha 
wanafunzi watahiniwa kujibu maswali vizuri katika mitihani yao hatimaye 
kuongeza ufaulu.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni