SERIKALI YAANDAA MPANGO KABAMBE WA MIPANGO MIJI (MASTER PLANS) ILI KUONDOA MIGOGORO YA ARDHI
By Newsroom on May 26, 2016  
       
       
       
         
       
       
        
Serikali kupitia Wizara ya Ardhi,
 Nyumba na Maendeleo ya Makazi inaandaa Mpango Kabambe wa Mipango Miji 
(Master Plan) utakaoainisha matumizi bora ya ardhi na kuondoa migogoro 
ya ardhi nchini.
Kauli hiyo ilitolewa jana Bungeni
 Mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi  
Mhe. Angelina Mabula  wakati akijibu maswali ya wabunge kuhusu mpango wa
 Serikali kumaliza migogoro ya ardhi kwenye maeneo mbalimbali nchini.
Mhe. Mabula alieleza kuwa Wizara 
yake inashirikiana na  Halmashauri za Wilaya na Miji 18 kwenye program 
ya Urban Local Government Supporting Programme (ULGSP) katika kuandaa 
Mipango Miji hiyo.
Pia Mhe. Mabula alibainisha kuwa 
Wizara inaandaa na kukamilisha programu ya kupanga, kupima na 
kumilikisha kila kipande cha ardhi Tanzania itakayotekelezwa kwa kipindi
 cha miaka kumi kuanzia 2015 hadi 2025.
“Serikali imekuwa ikiziagiza 
Halmashauri kutenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya upimaji kwa 
kuwa inatambua umuhimu wa kupima viwanja na mashamba ili kuwa na 
matumizi bora ya ardhi yetu” alisema Mabula.
Aidha, Mabula aliongeza kuwa 
Serikali kupitia Mradi wa Benki ya Dunia ipo katika mchakato wa kununua 
vifaa vya upimaji ambavyo vitasambazwa katika kanda 8 za Wizara ya Ardhi
 ili Halmashauri zote zilizopo ndani ya kanda hizo ziweze kunufaika.
Alieleza kuwa makadirio ya awali 
ya gharama za mradi huo ni Dola za Kimarekani Milioni 4 ambapo Dola 
Milioni 2 zitatumika kwenye upimaji na Dola Milioni 2 zitatumika kwa 
ajili ya ununuzi wa Vifaa.
Katika kupunguza na kutatua 
migogoro ya ardhi iliyopo sasa, Mabula alisema kuwa Wizara ya Ardhi 
imeandaa kitabu cha orodha ya migogoro nchi nzima kinachoainisha vyanzo 
vya migogoro hiyo ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.
Hali kadhalika, Mabula alisema 
kuwa Wizara imesambaza Sera na Sheria za Ardhi hasa kwenye maeneo yenye 
migogoro, wameimairisha mfumo wa kielektroniki  katika kutunza 
kumbukumbu, na kuboresha ofisi za Kanda ili kusogeza huduma za ardhi 
karibu na wananchi.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni