Serikali yakamata kilo 140 za dawa za kulevya nchini
Dar es Salaam.
Serikali imefanikiwa kukamata 
takribani kilo 139.69 za dawa za kulevya ikiwemo kilo 53.49 za Heroin, 
Cocaine kilo 86.2 kuanzia mwaka 2015 mpaka Aprili mwaka huu.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo 
vya habari kutoka Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya 
iliyotolewa na Mkuu wa Kitengo cha Elimu, Habari na Takwimu wa tume 
hiyo, Amani Msami, pia tume hiyo imekamata tani 97 za bangi na mirungi.
Alisema mbali na kukamata kilo 
hizo, takwimu zinaonesha kuwa watumiaji wa Heroin nchini wanakadiriwa 
kuwa kati ya 200,000 hadi 425,000 ambapo kati ya hao 30,000 hutumia dawa
 hizo kwa njia ya kujidunga sindano.
“Serikali imefanikiwa kukamata 
takribani kilo 53.49 Heroin, Cocaine kilo 86.2 kuanzia mwaka 2015 mpaka 
Aprili mwaka huu” alisema Msami na kuongeza kuwa:
“Watumiaji wa Heroin nchini 
wanakadiriwa kuwa kati ya 200,000 hadi 425,000 ambapo kati ya hao 30,000
 hutumia dawa hiyo kwa njia ya kujidunga”.
Msami alifafanua kuwa mbali na kukamata dawa hizo, tume hiyo ilikamata tani 81.3 za bangi na Mirungi tani 15.7.
Aliongeza kuwa mbali na hayo 
idadi ya watuhumiwa waliyokamatwa wakijihusisha na usafirishaji wa dawa 
za kulevya zikiwemo Bangi,Mirungi, Heroin na Cocaine walikuwa 14,503.
Hata hivyo, alisema takwimu hizo 
zinaonyesha jitihada za serikali katika kukabiliana na biashara ya dawa 
za kulevya nchini na si ukubwa wa usafirishaji wa Heroin na Cocaine 
nchini.
“Moja ya jitihada za Serikali 
katika kukabiliana na tatizo la dawa za kulevya ni kutungwa kwa Sheria 
ya kudhibiti na kupambana na Dawa za Kulevya Na.5 ya mwaka 2015.” 
Alisema Msami.
Alifafanua kuwa sheria hiyo 
imeweka adhabu kali kwa makosa ya kujihusisha na matumizi na biashara ya
 dawa ya kulevya ikiwemo kifungo cha maisha kwa yeyote atakayesafirisha 
dawa za kulevya.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni