SIKU YA VIPIMO DUNIANI: VIJANA WA KITANZANIA WATAKIWA KUCHANGAMKIA FURSA YA MAFUNZO KATIKA FANI YA VIPIMO
Mkuu
 wa Chuo cha Elimu ya Biashara kampasi ya Dar es salaam Prof. Emanuel 
Mjema (kulia) akiangalia moja ya mashine ya kisasa inayotumika 
kufundishia wanafunzi wa Fani ya Mizani na Vipimo ndani ya karakana ya 
chuo hicho leo jijini Dar es salaam wakati wa maadhimisho ya Siku ya 
Vipimo Duniani yaliyoongozwa na kauli mbiu isemayo Vipimo katika dunia 
inayobadilika.\
Mkufunzi
 wa Mizani na Vipimo wa Chuo cha Elimu ya Biashara kampasi Dar es salaam
 Ishigita Shunashu akitoa ufafanuzi kwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza 
wanaosomea fani hiyo leo jijini Dar es salaam wakati wa maadhimisho ya 
Siku ya Vipimo duniani.
Baadhi
 ya wanafunzi wa kike wa mwaka wa kwanza katika Fani ya Mizani na Vipimo
 katika Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es salaam (CBE). wakiangalia moja
 mashine ya kujifunzia masomo hayo iliyofungwa ndani ya Karakana ya 
Idara ya Vipimo na Mizani.
Mkufunzi
 katika Idara ya Mizani na Vipimo ya Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es 
salaam (CBE) Bi. Rabia Katula akitoa ufafanuzi kuhusu namna 
wanavyowajengea wanafunzi wa kuhakiki ubora wa mizani  na kushughulikia 
matatizo mbalimbali ya mizani.
Mkuu
 wa Chuo cha Elimu ya Biashara kampasi ya Dar es salaam Prof. Emanuel 
Mjema (wa tatu kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Wakufunzi
 wa chuo hicho, Idara ya Vipimo na Mizani.
Mkuu
 wa Chuo cha Elimu ya Biashara kampasi ya Dar es salaam Prof. Emanuel 
Mjema (wa tatu kutoka kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi
 wa mwaka wa kwanza wanaosomea shahada ya mizani na Vipimo.
Vijana wa kitanzania wametakiwa 
kuchangamkia fursa za mafunzo katika fani ya vipimo na uendeshaji wa 
mitambo mbalimbali ili Tanzania mpya ya viwanda iweze kujengwa na 
wataalam wazawa kutoka ndani ya nchi.
Kauli hiyo imetolewa leo jijini 
Dar es salaam na Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es salaam Prof. 
Emanuel Mjema alipotembelea maonesho ya vitendo yaliyoandaliwa na walimu
 na wanafunzi wa chuo hicho yaliyohusisha matumizi ya vifaa na 
teknolojia ya kisasa  ya Mizani na Vipimo.
Amesema Tanzania inahitaji 
wataalamu wengi wa vipimo kutokana na mahitaji makubwa yaliyopo kuanzia 
ngazi ya kijiji hadi taifa katika sekta ya Mafuta kwenye makampuni 
yanayouza mafuta, mafundi wa pampu za mafuta pia kwenye mitambo ya Gesi 
na kuongeza kuwa mahitaji wa wataalam hao kwa sasa ni makubwa kuliko 
idadi ya wataalam wanaozalishwa kwa mwaka.
Ameeleza kuwa sekta ya vipimo 
duniani kote ni sekta mtambuka kwa kuwa inagusa maeneo mbalimbali ya 
maisha ya mwanadamu na huchangia kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa maendeleo 
katika maeneo mbalimbali ikiwemo mazingira,teknoloji, Gesi, ubunifu 
ambayo yote yana vipimo vyake.
Amesema kuwa CBE kama chuo 
kinachofundisha fani ya Mizani na Vipimo nchini kimeungana na taasisi 
nyingine za elimu duniani kuadhimisha Siku ya Vipimo duniani ambayo 
mwaka huu inaongozwa na kauli mbiu isemayo Vipimo katika ulimwengu 
unaobadilika kuweka msisitizo katika ufundishaji unaokwenda sambamba na 
mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia yanayotokea duniani  ili kukidhi 
mahitaji ya soko.
Amesema Siku hiyo iliasisiwa 
mwaka 1870 kwa lengo la kuweka viwango kwenye upimaji wa kutumia Mita na
 kuongeza kuwa kuanzia wakati huo siku hiyo imekuwa ikiadhimishwa 
duniani kote.
Amefafanua kuwa chuo cha CBE 
kimedhimisha siku hiyo kwa kuwa ni chuo pekee kinachotoa taaluma ya 
elimu na watalaam wa Vipimo Afrika Mashariki, Kati na Kusini na 
kubainisha kuwa nchini Tanzania taasisi za Serikali ikiwemo Wakala ya 
Vipimo ambayo watalaam wake wengi wamefunzwa katika chuo hicho.
Prof. Mjema amesisitiza kuwa 
suala la vipimo linagusa maisha ya kila siku ya wananchi kutokana na 
umuhimu na kuzitaja sekta kama vile viwanda, madini na uchimbaji wa 
Mafuta na Gesi haziwezi kufanikiwa bila kuwa na watalaam vipimo.
Ili kuhakikisha sekta ya vipimo 
na Mizani katika chuo hicho inakwenda  na mabadiliko yanayotokea duniani
 chuo hicho kimekuwa kikibadilisha mbinu za kufundishia wanafunzi na 
kuandaa mitaala mipya ili kukidhi mabadiliko hayo.
Aidha, amesema wao kama watalaam 
wa vipimo wanasimamia na kutoa ushauri kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo
 kupiga vita ufungashaji wa mazao kwa kutumia vifungashio vilivyozidi 
maarufu kama Lumbesa ambayo vinamnyonya mkulima na kusababisha apate 
kiwango kisichoendana fedha na wingi wa mazao yake.
Amefafanua kuwa katika 
kukabiliana na changamoto  ya mabadiliko inayotokana na uvumbuzi wa Gesi
 na Mafuta nchini Tanzania  CBE ilianzisha mitaala ya ufundishaji wa 
nishati hizo kuwajengea uwezo wanafunzi wanaodahiliwa ili waweze 
kumiliki uchumi na kusimamia rasilimali za taifa kwa manufaa ya 
watanzania.
Prof. Mjema ameeleza kuwa licha 
ya vifaa vya kisasa vya kufundishia kupatikana gharama kubwa,chuo hicho 
imeendelea kufanya maboresho ya ndani kununua teknolojia mpya za kisasa 
zinazotumia mfumo wa digitali ili kuwawezesha wanafunzi kutumia mitambo 
mipya.
Amesisitiza kuwa CBE imeendelea 
na program mbalimbali za kuwajengea uwezo wakufunzi wake kwa kuwasomesha
 ndani na nje ya nchi ili waweze kutoa elimu yenye ubora na viwango 
vinavyokubalika.
“Ni kweli dunia imebadilika na 
teknolojia imebadilika sana tofauti na miaka ya nyuma, ili kuendana na 
mabadiliko haya tumebaresha mbinu zetu za ufundishaji ili wahitimu wetu 
waweze kumudu mahitaji ya soko kwa kukidhi viwango vya ndani na nje ya 
nchi kwa kuwa suala la vipimo halina mipaka” Amesisitiza Prof. Mjema.
Kwa upande wake Mkufunzi wa Chuo 
hicho Bw. Boniface Nyamweru amesema kuwa mafunzo anayoyatoa kwa 
wanafunzi wake yanalenga kuwajengea ujuzi na uwezo wa kubuni na 
kuanzisha vifaa vyao wenyewe vinavyoweza kutumika kwenye masuala ya 
Mizani na Vipimo.
Amesema kuwa yeye kama mtalaam wa
 masuala ya Mizani na Vipimo anawafundisha wanafunzi wake namna ya 
kushughulikia masuala mbalimbali yanayohusiana na ufundi kwenye  Mizani,
 kufanya ukaguzi wa Mizani na Mita za kupimia vimiminika mbalimbali kama
 mafuta ili kuhakikisha kuwa Sekta ya Mizani na vipimo nchini inapata 
wataalam wa kutosha wenye ujuzi.
“Mpaka sasa tunao wataalam wa 
ndani wazawa ambao tumewajengea uwezo wa kukabiliana na changamoto 
mbalimbali za kiufundi , wengi wao tumewafundisha sisi hapa chuoni na 
wana uwezo wa kufanya ukaguzi na uhakiki wa Mizani na vifaa mbalimbali 
vya Vipimo katika viwango na ubora unaotakiwa” Amesisitiza.
Kuhusu matumizi ya huduma ya 
Mizani na vipimo nchini yanaendeshwa kwa mujibu wa sheria huku 
akifafanua kuwa vipimo vinavyofanyika nchini ikiwemo matumizi ya mita ya
 kupimia mafuta (Flow Meter) eneo la bandari ya Dar es salaam 
vimeruhusiwa kisheria.
Faudhia Nchila mmoja wa wanafunzi
 wa mwaka wa kwanza wanaosomea fani ya Mizani na Vipimo katika chuo 
hicho amesema kuwa sekta ya Vipimo na Mizani ina mchango mkubwa katika 
maendeleo ya nchi kwa kuwa inagusa shughuli za kila siku za maisha ya 
wananchi.
Amesema vipimo vinagusa sekta ya 
ujenzi, maji, vifaa, teknolojia na shughuli mbalimbali za ufundi katika 
maeneo mbalimbali nchini huku akisisitiza kuwa mahitaji ya wataalam wa 
vipimo nchini kwa sasa ni makubwa kutokana na mchango wake katika 
maendeleo ya nchi na kutoa wito kwa vijana wengi zaidi kujiunga na 
masomo hayo.
Naye Dunstan Binamu mwanafunzi wa
 mwaka wa kwanza anayesomea masuala ya sheria katika fani ya Mizani na 
Vipimo akieleza mchango wa fani anayoisomea katika maendelea ya nchi 
amesema kuwa inalenga kulinda Haki ya mlaji katika kwa kuhakikisha 
masuala vipimo na mizani  yanafanyika katika viwango vilivyowekwa.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni