Serikali yawaunganisha watafuta kazi 20,000 na waajiri
Frank Mvungi-Maelezo
Serikali imefanikiwa 
kuwaunganisha Watanzania wanaotafuta kazi wapatao 20,000 ikiwa ni moja 
ya hatua ya kupunguza tatizo la ajira nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Msemai wa Wakala wa Huduma za Ajira nchini (TaESA) Bi Jamila Mbarouk wakati wa mkutano na vyombo vya habari leo jijini Dar es salaam.
Akizungumzia watafuta kazi 
waliongushwa tangu kuanzishwa kwa wakala huo Jamila alisema kuwa wengi 
waliounganishwa walikuwa wahasibu, Makatibu muhtasi, wataalamu wa huduma
 za jamii.
 “Jukumu letu letu ni 
kuwaunganisha watafuta kazi na waajiri ndani na nje ya nchi ili waweze 
kupata huduma hii kwa urahisi kwa kuzingatia sheria na kanuni za Ajira 
hapa nchini” alisisitiza Jamila.
Katika kupanua huduma ili 
kuwafikia watanzania walio wengi Jamila amebainisha kuwa (TaESA) 
imefungua ofisi za Kanda katika Mikoa ya Dodoma,Mwanza, na Arusha .
Mafanikio Mengine ni wakala 
kuendesha mafunzo ya kuwajengea uwezo watafuta kazi 3185 ili kuweza 
kuhimili ushindani na changamoto za soko la ajira.
Mafunzo hayo yametolewa 
mbalimbali ikiwemo chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Chuo cha Usimamizi 
wa Fedha (IFM), Taasisi ya Uhasibu (TIA), Chuo cha Ardhi na Taasisi ya 
Teknplojia Dar es salaam (DIT).
Akieleza Umuhimu wa mafunzo 
hayo Jamila amesema kuwa yanalenga kuwajengea uwezo watafuta kazi ili 
waweze kuandika barua za maombi ya ajira kwa ufasaha, kuandaa wasifu 
binafsi (CV) na kuwajengea uwezo wa namna ya kufanya mahojiano kwa 
ufanisi kwa kuzingatia mbinu za kisasa.
Kwa upande wake Afisa Kazi wa 
TaEsa Bw. Amani Kasale amesema kuwa baadhi ya watafuta kazi wamekuwa na 
kasumba ya kuchagua maeneo ya kufanyia kazi hasa yale yaliyopo katika 
miji mikuu hali inayozorotesha juhudi za Serikali kuwaunganisha watafuta
 kazi na waajiri katika maeneo mbalimbali hapa nchini na nje ya nchi.
Akifafanua Kasale alisema kuwa 
huduma ya kuwaunganisha watafuta kazi na waajiri inatolewa bure kwa 
watanzania wote wanaotafuta ajira kwa kuzingatia sheria na Kanuni za 
ajira hapa nchini.
Pia Kasale alitoa wito kwa 
vijana wote wanaotafuta ajira kuachana na kasumba ya kuchagua maeneo ya 
kufanya kazi hasa yale yaliyo katika miji mikuu na kutumia fursa 
zilizopo maeneo ya pembezoni.
Wakala wa huduma za Ajira 
Tanzania TaESA Ulianzishwa kwa sheria ya wakala Na. 30 ya mwaka 1997 
ikiwa na lengo la kuunganisha watafuta kazi na waajiri wenye fursa za 
ajira ndani na nje ya nchi.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni