MKURUGENZI MKAZI WA BENKI YA DUNIA NCHINI ATEMBELEA OFISI YA TAIFA YA TAKWIMU
………………………………………………………………………………………………………..
Na Veronica Kazimoto
26 Mei, 2016.
BENKI ya Dunia imeahidi 
kuendelea kuisaidia Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kifedha ili iweze 
kutekeleza majukumu yake ya utoaji wa Takwimu Rasmi nchini.
Akizungumza leo alipotembelea 
Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia hapa 
nchini Ms. Bella Bird amesema kutokana na umuhimu wa takwimu katika 
kupanga na kupima matokeo ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya 
kimaendeleo, Benki ya Dunia itaendelea kuisaidia NBS ili iendelee 
kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na kutoa takwimu kwa wakati.
 “Ili Ofisi ya Taifa ya Takwimu
 iweze kutoa takwimu kwa wakati, inahitaji kuwekeza katika matumizi ya 
technolojia ya kisasa ya ukusanyaji wa takwimu, hivyo Benki ya Dunia 
itaendelea kutoa msaada wa kiufundi na kifedha ili kufikia malengo 
yaliyoainishwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu ya utoaji wa takwimu rasmi 
nchini”, amesema Ms. Bella Bird. 
Mkurugenzi huyo Mkazi 
amefafanua kuwa Benki ya Dunia inatambua umuhimu wa takwimu katika 
maendeleo ya nchi zote duniani ikiwemo Tanzania katika kupanga sera na 
kutekeleza miradi mbalimbali ya nchi husika.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu
 wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dkt. Albina Chuwa ameishukuru Benki ya 
Dunia kwa misaada mbalimbali ambayo imekuwa ikiisaidia Ofisi ya Taifa ya
 Takwimu ambayo imeongeza tija katika ukusanyaji na utoaji wa takwimu 
rasmi nchini.
“Napenda kuchukua fursa hii 
kuishukuru Benki ya Dunia kupitia ujio wako kuitembelea Ofisi ya Taifa 
ya Takwimu na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na ofisi hii 
ikiwa ni pamoja na ukusanyaji na utoaji wa takwimu rasmi hapa nchini,” 
amesema Dkt. Chuwa.
Dkt. Chuwa amesema Ofisi ya 
Taifa ya Takwimu imeendelea kupanua wigo wa uzalishaji wa takwimu nchini
 ikilinganishwa na karne zilizopita.
Benki ya Dunia inaisaidia Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa kutoa
 ushauri wa kitalaam pamoja na fedha kupitia Mpango Kabambe wa Kitaifa 
wa Kuboresha na Kuimarisha Takwimu nchini ambapo awamu ya kwanza 
itakamilika mwezi Juni, 2018.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni