Waziri Mkuu awataka wabunge wa upinzani kurejea Bungeni
Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma
Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa 
leo, Bungeni Mjini Dodoma amewataka wabunge wa upinzani ambao wamesusia 
vikao vya Bunge tangu Mei 30 kuingia Bungeni na kuacha kususia vikao vya
 Bunge kwani hakuna tija kwa Taifa.
Mhe. Majaliwa ameyasema hayo alipokuwa akitoa hutuba ya kuhitimisha mkutano wa tatu wa Bunge la kumi na moja.
“kitendo cha baadhi ya 
waheshimiwa wabunge kususia vikao vya Bunge hakitoi picha nzuri kwa 
wananchi waliotuchagua kuwasilisha matatizo yao katika Bunge hili, hivyo
 natoa rai kwa waheshimiwa wabunge hao kutafakari upya uamuzi wao na 
niwasihi kwa busara zao waingie ili kwa pamoja na kwa ushirikiano tuweze
 kutoa ushauri kwa Serikali,” alisema Mhe. Majaliwa.
Aidha Mhe. Majaliwa alitoa 
ufafanuzi juu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977
 ambayo imetoa haki na kinga kwa waheshimiwa wabunge ili kujadili na 
kuhoji utendaji wa Serikali kwa uhuru bila mashaka yoyote ya kuweza 
kushitakiwa wanapotimiza wajibu wao wakiwa Bungeni.
Aliendelea kwa kusema kuwa kinga 
ya aina hiyo haijatolewa kwa mwananchi yeyote yule Nchini ila kwa 
Wabunge, hivyo basi hakuna mbunge aliyefungwa mdomo labda aamue 
kujifunga mdomo yeye mwenyewe.
Mhe. Majaliwa amesema kuwa Bunge 
linaongozwa na Katiba, Sheria na Kanuni za Kudumu za Bunge, hivyo ni 
vyema zikafuatwa kuondoa manung’uniko yasiyo ya lazima na endapo kuna 
utata katika jambo lolote ndani ya Bunge zipo taratibu zilizowekwa na 
kanuni za kufuata ili kupata ufumbuzi na si kwa kususa kuingia Bungeni 
kwani hakuna tija kwa Taifa.
Wabunge wa upinzani wamesusia 
vikao vya Bunge tangu Mei 30, 2016 mpaka leo Juni 30 ambapo Bunge 
limehitimishwa. Aidha wabunge hao wamekuwa wakiingia Bungeni kila 
asubuhi na jioni kisha kutoka mara tu Naibu Spika Mhe. Dkt. Tulia Ackson
 anapomaliza kusoma Dua maalum la kuliombea Bunge na Taifa.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni