Wanufaika wa Mikopo ya Elimu Juu watakiwa kurejesha mikopo waliyopewa.
Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma
Wanufaika wa Mikopo ya Elimu ya 
Juu ambao tayari wapo katika ajira wametakiwa kurejesha marejesho ya 
mikopo waliyopewa kutokana na mfuko wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu 
(HESLB) kutegemea fedha hizo kuendelea kuwakopesha wanafunzi wengine.
Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa 
ameyasema hayo leo Bungeni, Mjini Dodoma alipokuwa akiwasilisha hotuba 
ya kuhitimisha mkutano wa tatu wa Bunge la kumi na moja.
“Uwezo wa Bodi ya mikopo ya Elimu
 ya Juu kuwahudumia walengwa unajengwa na fedha zinazotengwa kila mwaka 
katika mipango na Bajeti pamoja na marejesho ya mikopo iliyoiva kutoka 
kwa wanufaika,” alisisitiza Mhe. Majaliwa.
Aliendelea  kusema kuwa Serikali 
inaendelea kufanya maboresho ya kimfumo na kisheria ili kuimarisha 
urejeshwaji wa mikopo. Aidha amewaagiza waajiri wote Nchini kutekeleza 
wajibu wao wa kuingiza makato ya marejesho wa mikopo ya wanufaika kwa 
wakati na kwa viwango vinavyotakiwa baada ya kuwasiliana na Bodi ya 
Mikopo.
Vile vile Mhe. Majaliwa amesema 
kuwa Serikali inaendelea kuimarisha mfumo wa utoaji wa mikopo kwa 
wanafunzi wa elimu ya juu sambamba na kushughulikia changamoto 
mbalimbali zilizopo katika Bodi ya mikopo ili kuhakikisha utoaji wa 
mikopo unafanyika kwa ufanisi.
Pia Serikali inategemea kubadilisha utaratibu wa kutoa mikopo ili kuwafikia
 wanafunzi wote wenye uhitaji zaidi wakiwemo yatima na wenye uwezo mdogo
 kiuchumi bila kujali aina gani ya program wanazozisomea.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni