Waganga wa tiba asili watakiwa kujisajili
—————————-
Waganga wa tiba asili ambao 
wamekuwa wakitoa huduma ya tiba pasipo kujisajili wametakiwa kujisajili 
Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala ili waweze kutambulika kisheria.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya
 Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Hamis Kigwangalla ameyasema hayo 
leo, Bungeni Mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge 
Viti Maalum Mhe. Zainabu Mussa Bakar juu ya udanganyifu unaofanywa na 
waganga wa tiba asili wa kutoa dawa feki kwa wagonjwa.
“Waganga wa tiba asili wapo 
kisheria, ni kweli wapo wanaotoa dawa feki, na wengi wao ni wale ambao 
hawajasajiliwa, hivyo tumewaagiza kujisajili ili tuweze kuwatumbua na 
dawa zao ziweze kuhakikiwa na kusajiliwa kwa ajili ya matumizi ya 
binadamu,” alifanunua Mhe. Kigwangalla.
Mhe. Kigwangalla amesema kuwa, 
mganga yoyote atakaye kiuka agizo hilo la kujisajili basi hatua kali 
zitachukuliwa dhidi yake. Aidha, amesema Wizara iko makini na 
ufuatiliaji wa dawa feki nchini kwani wanapopata fununu ya uwepo wa dawa
 feki hutuma kikosi kuchunguza na ikibainika kuwa dawa ni feki basi 
hatua kali huchukuliwa kwa muhusika.
Aliendelea kwa kusema kuwa, ili 
kudhibiti uingizwaji wa dawa feki nchini Wizara hiyo hufanya uhakiki wa 
muda mrefu kuchunguza iwapo dawa inayopendekeza kuingia nchini siyo feki
 na inafaa kwa matumizi ya binadamu, ikiwa dawa haina madhara yoyote 
basi inasajiliwa kwa ajili ya kuingia sokoni.
Vilevile Mhe. Kigwangalla amesema 
kuwa, Wizara imewaagiza waganga wa tiba asili kufunga dawa zao kwa 
kutumia vifungashio maalum vya madawa ambavyo vitasaidia dawa hizo 
kuendelea kuwa salama kwa mtumiaji kwa kipindi kilichopangwa kutumika.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni