Viwanda visivyo endelezwa kurudishwa kwa watanzania
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe. Charles Mwijage 
—————————————————
Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma
Viwanda vilivyobinafsishwa na Serikali ambavyo haviendelezwi kutwaliwa ili kutolewa kwa wawekezaji wenye uwezo wa kuviendesha. 
Waziri wa Viwanda, Biashara na 
Uwekezaji Mhe. Charles Mwijage ameyasema hayo leo mjini Dodoma alipokuwa
 akijibu swali la Mbunge wa Tabora Mjini Mhe. Emmanuel Mwakasaka 
aliyetaka kujua hatua zinazochukuliwa juu ya mwekezaji wa kiwanda cha 
nyuzi Tabora kwa kushindwa kuendeleza kiwanda hicho.
“Wizara kwa kushirikiana na Ofisi 
ya Msajili wa Hazina inaendelea na tathmini ya viwanda vyote 
vilivyobinafsishwa na Serikali kikiwemo kiwanda cha nyuzi cha Tabora ili
 kujiridhisha kama wawekezaji wa viwanda hivyo wanatimiza matakwa ya 
mkataba na Serikali,” alifafanua Mhe. Mwijage.
Aliendelea kwa kusema kuwa, ikiwa 
viwanda hivyo vitabainika kubadilishwa matumizi yake au kutoendelezwa 
basi Serikali itavirudisha kwa watanzani ili viweze kuendelezwa.
Aidha Mhe. Mwijage amesema kuwa, 
kwa sasa mwitikio wa kuviendeleza viwanda ambavyo vilikuwa havizalishi 
ni mzuri kwani viwanda vingi vimeanza kufanya kazi lakini kwa wale ambao
 watashindwa kabisa  kuviendeleza basi viwanda hivyo vitarejeshwa kwa 
watanzania.
Vile vile Mhe. Mwijage amesema 
kuwa dhana ya Serikali ya awamu ya Tano ya kujenga uchumi wa viwanda 
inaenda pamoja na kurejesha Serikalini viwanda vyote vilivyobinafsishwa 
lakini haviendelezwi ili vitolewe kwa wawekezaji wengine. 
Sambamba na hayo Mhe. Mwijage 
amesema kuwa kufufua viwanda, hasa viwanda vya nguo ni pamoja na 
wakulima wa pamba kulima zao hilo kwa wingi kwa ajili ya uchakataji 
pamoja na kudhoofisha uingizaji wa nguo za mitumba nchini.
Wizara hiyo inaendelea na 
kushawishi wawekezaji mbalimbali ili kujenga viwanda vingi iwezekavyo 
kwa ajili ya uchakataji wa mazao yanayolimwa nchini pamoja na mifugo.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni