KONGAMANO LA KUBADILISHANA UZOEFU WA MAFUNZO YA TAALUMA UFARANSA NA TANZANIA LAFANYIKA
KONGAMANO kubwa la aina 
yake limefanyika mjini Dar es salaam ambapo washiriki walizungumzia 
namna ya kuendeleza rasilimali watu katika eneo la utaalamu na taaluma 
katika shughuli mbalimbali za uendelezaji wa makampuni na viwanda.
Kongamano hilo ambalo 
lilihudhuria na watu wenye kariba kubwa katika masuala ya viwanda na 
biashara akiwemo Dkt. Reginald Mengi ambaye ni Mwenyekiti wa makampuni 
ya IPP na Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF);na Balozi wa 
Ufaransa nchini Malika Berak liliangalia uhaba wa wataalamu na namna ya 
kuuondoa uhaba huo wakati taifa linaelekea katika uchumi wa kati 
unaotegemea viwanda.
Wengine waliokuwepo katika 
kongamano hilo Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) 
Dkt. Tonia Kandiero na maofisa wa serikali.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi 
ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida akikaribisha 
washiriki na wadau wengine alisema kwamba mafunzo hayo yaliyoratibiwa 
kwa pamoja katika wataalamu wa Ufaransa, ESRF na Benki ya Maendeleo ya 
Afrika yamelenga kudadavua tatizo lililopo na kulipatia ufumbuzi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi 
ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida (katikati) 
akisalimiana na mgeni rasmi Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi 
(TPSF), Dk. Reginald Mengi (kulia) alipowasili katika ofisi za ESRF 
jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Balozi wa Ufaransa nchini, Mh. Malika 
Berak.
(Picha na Modewjiblog)
Taasisi ya utoaji mafunzo ya 
Ufaransa ya AFPA ndiyo ilikuwa inaendesha mafunzo hayo wakibadilishana 
uzoefu na wadau wa Tanzania kutoka sekta binafsi.
Akifafanua zaidi Dkt. Kida 
alisema kwamba kongamano hilo limelenga zaidi katika kubadilishana 
uzoefu kuhusu changamoto zinazojitokeza na fursa zilizopo katika 
mafunzo, ukuzaji na uendelezaji taaluma.
Dkt. Kida alifurahishwa na 
mchanganyiko wa watu kutoka sekta binafsi waliofika katika kongamano 
hilo ambao aliamini kwamba wataelezea uzoefu wao katika kukabiliana na 
changamoto za taaluma katika makampuni yao.
Aidha alisema kwamba wadau hao 
wa Tanzania watapata uzoefu wa timu ya wataalamu wanne kutoka kwa wakala
 wa mafunzo ya taaluma nchini Ufaransa (AFPA) ambao wataeleza miaka 60 
ya uzoefu katika masuala ya mafunzo ya taaluma na uendelezaji wa 
utaalamu.
 Balozi wa 
Ufaransa nchini, Mh. Malika Berak (kushoto) akibadilishana mawazo na 
mgeni rasmi Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Dk. Reginald 
Mengi (kulia) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa 
Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida katika ofisi za ESRF jijini 
Dar es Salaam.
Alisema anaamini kwamba 
mchanganyiko huo wa wadau utasaidia katika kukabiliana na tatizo la 
taaluma katika soko la ajira la Tanzania.
Alisema mazungumzo hayo ni 
muhimu sana katika kuibua fursa hasa wakati taifa hili linajipanga 
kuelekea katika uchumi wa kati wa viwanda na bila wataalamu wenye 
taaluma zao makamapuni na viwanda vingi vitakuwa na shida kubwa.
Alisema changamoto kubwa 
inayokabili taifa la Tanzania kuelekea nchi ya viwanda kama ilivyo 
katika nchi nyingine zinazoendelea ni ukosefu wa taaluma na utaalamu.
“Ukosefu wa wafanyakazi wenye 
taaluma katika ngazi zote ni tatizo kubwa linalokabili harakati za 
kuelekea uchumi wa viwanda” alisema Dkt. Kida.
Anasema pamoja na matatizo hayo 
taasisi yake tayari imeshaanza kushughulikia shida hiyo ya taaluma 
nchini Tanzania kwa kuwa na makongamano mbalimbali makubwa 
yanayokutanisha wadau kuzungumzia hali hiyo.
Balozi wa Ufaransa nchini, Mh. 
Malika Berak (kulia) akisalimiana na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya 
Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Tonia Kandiero (kushoto) alipowasili 
ofisini kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Uchumi na 
Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida (katikati) kabla ya kuelekea kwenye 
ukumbi wa mikutano.
Alisema kwa mfano mwaka 2015 
iliendesha jukwaa la mafunzo ya ufundi (VTEC) Africa. Katika jukwaa hilo
 lililofanyika Machi 10 -12 mwaka huo walizungumzia mafunzo ya utaalamu 
wa gesi na mafuta kwa mataifa ya Afrika. Jukwaa hilo liliendeshwa kwa 
kushirikiana na kampuni ya Uingereza ya Getenergy.
Aidha Oktoba 9, 2015 iliendesha semina kuhusu uumbaji wa programu za mafunzo kwa aili ya kupata wataalamu wa gesi na mafuta.
Lakini, alisema, kuanzia Julai 
2014, ESRF imekuwa ikishirikiana na shirika la Maendeleo la Marekani 
(USAID) kutekeleza mpango wa miaka mitano wa mafunzo ya kinadharia na 
utaalamu yenye mfumo wa Ushiriki ambapo ESRF yenyewe hutoa msaada wa 
kitawala na lojistiki kwa wanafunzi ili waweze kwenda kuhudhuria mafunzo
 nje ya nchi.
Aidha ESRF imekuwa ikifanya 
tafiti mbalimbali na uchambuzi kuhusiana na uendelezaji wa taaluma 
nchini Tanzania na moja ya ya tafiti hiyo ni kudorora kwa ubora wa elimu
 Tanzania na namna ya kuzuia anguko hilo na kulibadili.
Mwaka 2014 na mwaka huu kuna 
mada inayozungumzia uendelezaji wa mafunzo ya taaluma na uwezo wa 
uzalishaji Tanzania.Mada hii ni sehemu ya taarifa ambazo zitapatikaa 
katika ripoti ya Maendeleo ya Binadamu ya mwaka 2017.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi 
ya Utafiti wa Uchumi na Kijamii (ESRF), Dkt. Tausi Kida (kulia) 
akiongozana na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) 
Dkt. Tonia Kandiero kuelekea kwenye ukumbi wa mikutano wa ESRF. Nyuma ni
 Balozi wa Ufaransa nchini, Mh. Malika Berak akibadilishana mawazo na 
mgeni rasmi Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Dk. Reginald 
Mengi pamoja na Mkurugenzi wa Ajira Ofisi ya Waziri Mkuu, Ally Msaki.
Continue reading →
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni