Waziri
 wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akizungumza kwenye kikao
 na mabalozi kutoka Ujerumani na Denmark (hawapo pichani) hivi karibuni 
katika Ukumbi wa Wizara jijini Dar es Salaam.
Waziri
 wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo(Katikati) akiwa katika 
picha ya pamoja na Balozi wa Ujerumani, Egon Kochanke(Kulia) na Balozi 
wa Denmark, Einar Jensen(Kushoto).
Waziri
 wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo(Kulia) akijadiliana 
jambo na Balozi wa Denmark, Einar Jensen (Kushoto). Katikati ni Balozi 
wa Ujerumani, Egon Kochanke akiweka sahihi kwenye kitabu cha wageni 
ofisini kwa Waziri jijini Dar es Salaam hivi karibuni.
…………………………………………………………………………………………
- Kina thamani ya Dola za Marekani bilioni 1.5
- Kuzalisha tani milioni 1.35 kwa mwaka
Na Devota Myombe 
Waziri wa Nishati na Madini, 
Profesa Sospeter Muhongo amekutana na Balozi wa Ujerumani nchini 
Tanzania, Egon Kochanke pamoja na Balozi wa Denmark nchini, Einar Jensen
 kujadili ujenzi wa Kiwanda cha mbolea wilayani Kilwa.
Katika mkutano huo, ilielezwa 
kuwa matayarisho ya ujenzi wa kiwanda hicho cha mbolea chenye thamani ya
 Dola za Marekani bilioni 1.5 yanaendelea na kwamba kiwanda hicho 
kinatarajiwa kuzalisha tani milioni 1.35 za mbolea kwa mwaka.
Waziri Muhongo alisema ardhi kwa 
ajili ya ujenzi wa kiwanda hicho ipo na kuwa gesi asilia itakayotumika 
kiwandani hapo ipo ya kutosha.
Alisema kampuni mbalimbali kutoka
 ndani na nje ya nchi zitakuwa na hisa katika kiwanda hicho ambapo kwa 
upande wa Tanzania, alizitaja kampuni hizo kuwa ni Shirika la Maendeleo 
ya Petroli Tanzania (TPDC), Minjingu Mines pamoja na Shirika la Taifa la
 Hifadhi ya Jamii (NSSF).
Aidha, kwa upande wa kampuni za 
nje, Profesa Muhongo alizitaja kuwa ni Ferrostaal ya Ujerumani, Haldor 
Topsoe ya Denmark na Fauji kutoka nchini Pakistan.
Profesa Muhongo aliwahakikishia 
mabalozi hao pamoja na ujumbe wao kuwa ardhi kwa ajili ya uwekezaji wa 
kiwanda hicho ipo na kwamba gesi asilia itakayohitajika ipo ya kutosha 
na kuwa bado nafasi za uwekezaji zinapatikana. “Ardhi ipo, gesi ipo 
hivyo mnakaribishwa,” alisema Prof. Muhongo.
Naye Balozi wa Ujerumani nchini, 
Egon Kochanke alimshukuru Profesa Muhongo kwa kukubali kukutana na 
ujumbe huo kupokea maombi ya mpango wa ujenzi wa Kiwanda hicho cha 
mbolea ambapo alisema, hiyo ni njia mojawapo ya kuboresha uzalishaji 
Tanzania. “Nimefurahi sana kushiriki kikao hiki na nina kushukuru kwa 
kukubali kwako kupokea maombi haya,” alisema.
Kwa upande wake Balozi Einar 
Jensen alitumia nafasi hiyo kumshukuru Profesa Muhongo kwa jinsi 
alivyoupokea ujumbe huo na namna alivyoendesha majadiliano husika.
Kikao hicho pia kilihudhuriwa na baadhi ya watendaji wa Wizara pamoja na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati na Madini.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni