SERIKALI YATANGAZA KIAMA CHA WAUZA DAWA NA VIPODOZI HATARI MITANDAONI
——————————
Serikali kupitia Mamlaka ya 
Chakula na Dawa (TFDA) imesema hivi karibuni itaanza msako mkali wa 
kuwatafuta na kuwakamata wauzaji wa dawa zinazokatazwa pamoja na 
vipodozi vikali ambao wanajitangaza kupitia mitandao mbalimbali ya 
kijamii.
Hayo yamesemwa na Meneja 
Mawasiliano na Uhusiano wa Umma kutoka TFDA Bi. Gaudensia Simwanza 
wakati wa mahojiano na mwandishi wa habari hii kuhusu kuibuka kwa watu 
wanaotangaza  biashara ya dawa na vipodozi ambavyo Serikali imevipiga 
marufuku.
Akitaja bidhaa hizo Bi. Simwanza 
alisema ni pamoja na dawa za kuongeza ukubwa wa viungo vya mwili, 
kupunguza uzito wa mwili na vipodozi vyenye kemikali za kuchubua ngozi 
bidhaa ambazo zinasababisha madhara makubwa kwa binadamu ikiwemo ugonjwa
 wa Saratani.
“Kumezuka wafanyabiashara holela 
wanaotumia mitandao ya kijamii kama vile Instagram, Facebook, Whatsup 
Groups na kwengineko  kutangaza biashara ya dawa na vipodozi vyenye 
kemikali hatari ambavyo vimepigwa marufuku na TFDA hivyo wanaohusika 
wajiandae, hivi karibuni tutaanza kuwashughulikia.” Alisema Simwanza.
Alibainisha kuwa bidhaa hizo 
nyingi hazijathibitishwa na kupewa kibali na TFDA hivyo wauzaji 
wanakiuka Sheria ya Chakula, Dawa na Vipodozi Sura ya 219 inayowataka 
wafanyabiashara wote wa bidhaa hizo kuzisajili kabla hazijaenda kwa 
 mtumiaji na kutofanya hivyo ni kwenda kinyume na Sheria.
Alieleza kuwa TFDA kwa 
kushirikiana na Jeshi la Polisi wameandaa mkakati madhubuti wa 
kuhakikisha wanawabaini na kuwakamata wafanyabiashara wote wanaouza dawa
 na vipodozi hivyo kupitia mitandao na kuwachukulia hatua ikiwemo 
kuwafikisha mahakamani au kuwatoza faini.
“Wengi wa wafanyabiashara hao 
hawaweki anuani za maeneo wanayopatikana na hawana maduka rasmi bali 
huweka namba za simu za mkononi lakini kwa kutumia vyombo vya dola 
tutawabaini tu na kuwatia mbaroni.” Alisisitiza Simwanza.
Kwa upande wake Meneja Mawasiliano
 wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Bw. Innocent Mungy 
amewatahadharisha watumiaji wa huduma za mawasiliano hasa matangazo ya 
biashara kuwa makini na matangazo hayo kwani baadhi ya wafanyabiashara 
hizo wanaweza kuwa ni watu wenye nia mbaya.
Hivi karibuni kumeibuka wimbi la 
wafanyabiashara wa dawa mbalimbali pamoja na vipodozi ambao 
wanajitangaza kupitia mitandao ya kijamii na kuna baadhi ya watu 
wananunua bidhaa hizo bila ya kuhakikisha usalama wake jambo ambalo ni 
hatari kwa afya zao.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni