 
MSHAMBULIZI wa Taifa Stars, Elius Maguli amekamilisha usajili wake 
kutoka Stand United ya Shinyanga kama mchezaji huru na kujiunga katika 
klabu ya Dhofar SC ya Oman Professional League.
Kila mmoja anakumbuka namna mchezaji huyo alivyopitia kipindi kigumu 
msimu wa 2014/15 akiwa na kikosi cha Simba SC ambacho kabla ya kuanza 
kwa msimu wa 2015/16 kocha aliyepita wa kikosi hicho, Dylan Kerr 
alitangaza kutomuhitaji na uongozi ukavunja mkataba wake akiwa bado na 
mwaka mmoja zaidi.
Kitendo cha kujiunga na kocha Mfaransa, Patrick Liewig katika timu ya
 Stand kabla ya kuanza kwa msimu uliopita hakikuonekana kuwastua wengi 
lakini game 9 za mwanzo wa msimu ziliambatana na magoli 9 kwa mchezaji 
huyo wa zamani wa Ruvu Shooting, pia alishinda tuzo ya mchezaji bora wa 
mwezi katika VPL na kujumuhishwa katika timu ya Taifa kwa mara ya kwanza
 baada ya miaka mitatu.
Kujiunga na Dhofar timu iliyomaliza katika nafasi ya tano katika ligi
 ya kulipwa mwaka mmoja uliopita ni hatua kubwa kwa mchezaji kijana kama
 Maguli ambaye ameondoka VPL akiwa amefunga jumla ya magoli 33 katika 
misimu yake mitatu aliyocheza kama mchezaji wa vilabu vya Shooting, 
Simba na Stand United.
Ameruka vikwazo vingi katika ‘soka lenye fitna’ na matatizo mengi ya 
watendaji. Mfano, katika misimu yake miwili ya mwisho VPL (Simba na 
Stand) timu hizo zote mbili zimejaa migogoro ya kiutendaji kati ya 
viongozi na wachezaji au viongozi kwa viongozi.
Katika mazingira hayo si rahisi kwa mchezaji kutimiza malengo yake na
 inapotokea nafasi kama hii ya Maguli-Kusajiliwa moja kwa moja na timu 
ya kulipwa ukiwa U25 ni jambo la kumshukuru Mungu na pengine ni sehemu 
ya kufanya kazi nzuri zaidi kwa jitihada ili kuthibitisha kwa wale 
waliokusaini kuwa hawakufanya makosa.
Maguli ni mshambuliaji wa kikosi cha kwanza katika timu ya Taifa ya 
Tanzania kwa mwaka mmoja sasa akicheza sambamba na Thomas Ulimwengu na 
Mbwana Samatta katika safu ya mashambulizi kwa maana hiyo, kocha Charles
 Mkwassa ataendelea kufurahia vijana wake watatu wakiwa ng’ambo ya nchi 
kuendeleza vipaji vyao na kudumisha viwango vyao vya kiuchezaji.
Kama Hamis Mroki anayecheza Thailand, huyu ni nahodha wa kikosi cha 
vijana kilichokuwa kikiwajumuhisha kina Ulimwengu, Himid Mao na wengine 
ni zao la TSA, Samatta, Tom, Maguli, Mrisho Ngassa watatupiwa jicho la 3
 bila shaka timu ya Taifa Stars itaimarika licha ya kwamba bado hatuna 
ligi makini ya ndani.
Dhofar ni timu iliyoanzishwa miaka 44 iliyopita, na Oman kuna 
mishahara mikubwa hadi kufikia dola 30,000 kwa mchezaji wa kiwango cha 
Maguli. Mchezaji wa kikosi cha kwanza wa timu ya Taifa. Sasa mastaa 
watatu wa Stars katika kikosi cha mashambulizi wapo ng’ambo. Kila la 
heri Elius Maguli.
Kwa ukaribu zaidi, tafadhali unaweza ku-LIKE PAGE yangu BSports. Utapata Updates za michuano mbalimbali.