Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Nape Nnauye akikabidhi Ipad
tano kwa mkuu wa wilaya ya Bukoba Bw.Jackson Msome kwa ajili ya
matumizi ya maafisa habari wa mkoa wa Kagera. Bwana Msome alikuwa
akimwakilisha Mkuu wa mkoa wa Kagera, Meja Jenerali mstaafu Salum
Mustafa kijuu.
……………………………………………………………………………………………………
Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO
Sekta ya
habari ni kiungo muhimu cha mawasiliano kati ya wananchi na serikali
yao. Ndiyo maana wanazuoni hupenda kusema kuwa habari ni muhimili wa nne
wa dola. Kwa kuzingatia umuhimu huo, katika kuchekecha huku na huko,
Mhe. Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John
Pombe Magufuli akamteua mtu mahiri kuongoza sekta hii, Mhe. Nape Moses
Nnauye.
Kwa uteuzi
huu ninadiriki kusema hatimaye Wizara imepata mtu sahihi na mchapakazi
anayeweza kwenda na kasi ya Mheshimiwa Rais Magufuli na ni dhahiri
kabisa kuwa kumpa Mhe. Nape ni kuthibitisha usemi wa wahenga usemao
upele umepata mkunaji.
Kwa jinsi
hii tuna kila sababu ya kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wa Mbingu na
Nchi kwa kutujalia kupata kiongozi wa nchi ambaye ni mchapakazi na
aliyejaliwa kipawa cha kuona mbali kwa kuwaweka viongozi wa chini yake
katika nafasi za uongozi wanazostahili.
Sekta ya
habari ni sekta nyeti na muhimu sana katika dunia hii kwa kua bila
kupashana habari na kujua kinachoendelea daima hakutakua na maendeleo
kwa hiyo, ni sekta inayohitaji kuangaliwa kwa jicho la tatu ili
kuhakikisha kwamba inachukuliwa uzito na inapewa kipaumbele kwa kupewa
vifaa na elimu ya kutosha ili kuepusha upotoshaji na kukosekana kwa
habari muhimu hasa za Serikali zinazotakiwa kuwafikia wananchi kwa muda
husika.
Tukiangalia
katika sekta ya habari, Mhe.Rais hakukosea kabisa kumuweka Waziri Mhe.
Nape kwa kuwa ameanza kuitumikia Wizara kwa kasi nzuri na ameonyesha nia
ya kuiboresha Wizara hasa kwa tasnia ya habari kwa kuanzia kwenye
wizara yake hadi katika ofisi za umma zilizoko mikoani ili kuhakikisha
wanahabari wote nchini wanatambua thamani ya kazi yao.
Kwa maneno yake aliyoyatoa Jijini Mbeya alipokua akigawa vitendea kazi vya kisasa kwa ajili ya mawasiliano yaani ipad
kwa maafisa mawasiliano wa mkoa huo alikaririwa akisema,”Nataka Wizara
ihamie mikoani” hii haimaanishi kuwa Wizara ihamie mikoani kama
alivyosema bali alimaanisha kiutendaji zaidi kuwa yale yote anayoyafanya
katika Wizara yake atahakikisha na maafisa wa mikoani pia wanafanyiwa
hivyo ikiwemo kugawiwa vitendea kazi pamoja na mambo mengine.
Katika kuhakikisha hilo, kwa upande wa sekta ya habari, Waziri Nape ameanza kwa kugawa ipad
kwa maafisa mawasiliano walioko mikoa ya pembezoni ambao wana upungufu
mkubwa wa vitendea kazi na kwa muda mrefu wameshindwa kuifanya kazi yao
kwa ufanisi kwa sababu ya uhaba wa vifaa vya kufanyia kazi hiyo.
Ipad
hizo zilizotolewa kama msaada kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo na kampuni ya Startimes ambayo imeahidi kuwa bega kwa bega na
Wizara hii katika kuisaidia ili kuongeza ufanisi hasa katika sekta hii
nyeti ya habari maana kwa maneno mengine tunaweza kusema sekta ya habari
ndio daraja linalounganisha serikali na wananchi.
Siku
aliyokabidhiwa ipad hizo Mhe. Nape alikaririwa akisema “Nawashukuru sana
Startimes kwa kutujali,ipad hizi tutaanza kuzigawa kwa maafisa habari
wa mikoa ya pembezoni kwa kuwa ndiko kuna uhaba mkubwa sana wa vifaa kwa
maafisa hao”alisema Mhe Nape.
Maneno haya
ya Mhe.Nape yanaungana na usemi wake wa kuifanya Wizara kuhamia mikoani
kwa maana ya kuwapa kipaumbele katika kuwapatia vitendea kazi ili nao
wasijione kuwa wametengwa au kutokuthaminiwa kama maafisa mawasiliano
wengine hasa walioko Dar es salaam na mikoa mingine iiliyoendelea. Maana
anaamini kuwa mikoani ndiko kuna wadau na ndiko ziliko shughuli nyingi
kwa kuwa watu wengi wenye uwezo wa kuzikuza tasnia anazozifuatilia wapo
mikoani.
Ni mengi
sana Mhe.Nape ameyaongea hasa kwenye ziara zake alizozifanya kwenye
baadhi ya mikoa kama Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi, Kigoma, Geita,
Simiyu,Dodoma, Kagera pamoja na Mwanza ambako alipita kugawa ipad na
kuangalia jinsi maafisa habari wanavyofanya kazi katika vituo vyao vya
kazi. Ziara hiyo pia inalenga katika kujua changamoto wanazokumbana nazo
ili kuweza kufanya kila kinachowezekana kuzitatua ili kufanya sekta hii
kufanya kazi ya kupeleka taarifa kwa wananchi kama inavyopaswa
kufanyika ili kuendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa
na Jemedari Mkuu Mhe. Rais John Pombe Magufuli.
Kiongozi
huyu ameongelea kuhusu Muswada wa Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari
ambao ulishirikisha wadau mbali mbali hasa wahariri pamoja na wamiliki
wa vyombo vya habari kutoa maoni yao ambayo kwa asilimia 99 maoni hayo
yamewekwa katika muswada huo.
“Muswada huo
umeshakamilika, uko tayari kufikishwa bungeni, pia nataka
niwathibitishie kuwa muswada huo utalinda maslahi ya waandishi wa habari
kuanzia mishahara yao, mikataba ya kazi zao pamoja na bima ya matatizo
wanayoyapata kwenye kazi zao lakini muswada huo utakua na sheria
zitakazobana ufundishwaji wa masomo ya habari ili tupate waandishi ambao
wamebobea katika fani hiyo” alisema Mhe. Nape.
Ndoto ya
changamoto zinazoikabili tasnia ya habari mikoani zinakaribia kuwa
historia kwa kuwa Waziri Nape amepanga kuleta teknolojia mpya na kuzitoa
zile zilizopitwa na wakati ili kuharakisha ufanisi wa utoaji wa
taarifa, kuweka busta kwa baadhi ya maeneo ili televisheni ya taifa
(TBC) iwe bora zaidi na kuongeza urefu wa minara ili matangazo yafike
mbali zaidi.
Waziri Nape
ameamua kuboresha urefu wa minara ili matangazo yafike mbali kwani mikoa
mingi ya pembezoni imepakana na nchi ambazo teknolojia zao za
mawasiliano ni kubwa kiasi kwamba wananchi wengi wa mipakani
wanasikiliza redio za nchi jirani na kuacha kusikiliza redio za hapa
nyumbani Tanzania.
Katika
harakati za kuboresha tasnia ya habari, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Amos
Makalla ameelezea changamoto na jinsi alivyopanga mikakati ya kusaidia
na kuiboresha tasnia hii mkoani kwake ambapo alikaririwa akisema “Mkoa
wangu unaomba kibali cha kuajiri maafisa habari ili kila Halmashauri iwe
na afisa habari wake pia naahidi kuendelea kutenga bajeti kwa ajili ya
kununua vitendea kazi vya maafisa hao”.
Wakati huo
huo, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa wito kwa wananchi
kuanzisha vituo vya utangazaji 19 katika Wilaya na Halmashauri
mbalimbali na wamewaomba wadau kutuma maombi kabla ya Aprili 29 mwaka
huu.
Akiongea
katika mkutano wa Mhe.Nape na wadau wake, Meneja wa Mamlaka ya
Mawasiliano Tanzania Nyanda za Juu Kusini, Mhandisi Lilian Mwangoka
alisema, “Mamlaka ya Mawasiliano ipo tayari kushirikiana na wananchi
kuongeza vituo vya utangazaji ili kuongeza idadi ya vituo na kuongeza
fursa katika ukusanyaji wa kodi”.
Aidha,
Waziri Nape amesisitiza suala la maafisa habari kupewa ruhusa ya
kushiriki katika vikao vya maamuzi ili wajue mambo yanayoendelea katika
ofisi zao kwani kufanya hivi kutasaidia maafisa habari kuacha kuwakimbia
waandishi wa habari na badala yake kuwapa taarifa kamili ili
wakawajulishe wananchi taarifa sahihi kuhusu Serikali yao.
Akiongea kwa
kujiamini Waziri Nape amehakikisha kuwa yote yatawezekana maana fedha
za kutatua kero hizo zitapatikana kwa kuwa Mhe.Rais tayari alifanya
maamuzi ya kuziamuru taasisi zote za Serikali zilizopewa huduma ya kutoa
matangazo yao kupitia Televisheni ya Taifa bila kulipa waanze kulipa
madeni yao mara moja kwa hiyo fedha hizo ndizo hasa zitatumika katika
kuboresha tasnia hii.
Sasa ni
wakati wa maafisa habari pamoja na waandishi wa habari wote nchini
kuunga mkono jitihada za waziri wetu kwa kufanya kazi za kukusanya na
kutawanya taarifa kwa ufanisi na usahihi wa hali ya juu ili kuifanya
jamii ielewe umuhimu wetu pamoja na kukuza uchumi wa nchi kupitia
taarifa tunazozitoa kwenye vyombo vya habari.
Wahenga
wanasema Taifa lisilo na taarifa haliwezi kukua kiuchumi, litadumaa.
Hivyo tumuunge mkono Mzalendo huyu ili kukuza na kuinua Tasnia ya Habari
na ionekane kweli kuwa muhimili wanne wa dola ambao unachangia kwa
kiasi kikubwa katika kuleta maendeleo.
i
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni