Alhamisi, 28 Aprili 2016

Sio kila homa ni malaria, nenda ukapime

UMMWaziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akipima afya yake kujua kama ana vimelea vya ugonjwa wa malaria baada ya kutoa tamko la maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani mjini Dododma Aprili 25 mwaka huu.
……………………………………………………………………………………………
Na Eleuteri Mangi-MAELEZO, Dodoma.
La mgambo likialia kuna jambo, safari ya kujenga taifa bora na imara katika sekta ya afya ni jukumu la watu wa taifa husika kuanzaia na mtu mmoja mmoja.
Katika kuhakikisha watu wanajenga afya njema itakayowawezesha kuwa uchumi imara, ni jukumu la taifa hilo na kila mtu kutumia nguvu zake katika kujenga uchumi imara wenye kusimamiwa na afya bora ambayo ni ni msingi maendeleo.
Katika hali ya kawaida, mtu anayefanya kazi za mbalimbali za kijamii, kiuchumi na kisaiasa ni lazima awe na afya bora na njema, kwa maneno mengine ni lazima awe mzima.  
Siku ya Malaria Duniani inayoadhimishwa kila mwaka Aprili 25, ni moja ya siku adhimu inayopaswa kuzingatiwa na kutiliwa maanani.
Maadhimisho hayo yalianza kuadhimishwa tangu mwaka 2001 inatoa nafasi kwa Wataalamu wa Afya na Wananchi kwa jumla kuchambua kwa kina utekelezaji wa mapambano dhidi ya Ugonjwa wa Malaria kwa kila mwaka.
Siku hiyo inatoa nafasi ya kuangalia tulikotoka, tulipo na tunakokwenda katika suala zima la kufanikisha mapambano dhidi ya malaria.
Jitihada hizo hufanywa ulimwenguni kote kutokana na kutambua kuwa Malaria haina mipaka hivyo mikakati ya kupambana na ugonjwa huo inahitaji ushiriki wa Wadau wote si tu katika Bara la Afrika peke yake, bali Ulimwenguni kote.
Kila mpenda maendeleo anatambua namna Ugonjwa wa Malaria unavyoendelea kuwa tishio kwa maisha ya Watanzania kwa miaka mingi sasa.
Taarifa za Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsia, Wazee na Watoto zinaonyesha kuwa, Ugonjwa wa Malaria unaongoza kuwa na wagonjwa wengi wa Nje (OPD) katika hospitali nyingi hapa nchini pamoja na wagonjwa wa malaria wanaolazwa katika Hospitali katika hospitali mbalimbali. Pia ugonjwa wa malaria unaongoza kwa vifo vyote vinavyotokea katika Vituo vya Tiba.
Mwanga bora wa kutatua tatizo hili nchini umeanza kuonekana ambao ni dalili njema ya kulitoa taifa kwenye janga na hatari za ugonjwa wa malaria hatua ambayo itasaidia kupungua kwa kiasi kikubwa ugonjwa huo nchini.
Kutokana na Ripoti ya Utafiti wa viashiria vya VVU/UKIMWI na malaria inaonekana kupungua kwa asilimia 50 kutoka asilimia 18 kwa mwaka 2007/2008 hadi asilimia 10 mwaka 2011/2012.
Pamoja na kupungua kwa maambukizi ya malaria, takwimu zinaonesha kuwa ugonjwa huo bado ni tatizo kubwa katika vijijini ikilinganishwa na maeneo ya mjini ambapo maambukizi ya maeneo ya vijijini ni asilimia 10.7 na mjini ni aslimia 3.4
Kupungua kwa maambukizi ya ugonjwa wa malaria nchini, Watanzania wana kila sababu ya kujipongeza na kumshukuru kila mdau aliyeyechangia kwa namna moja au nyingine katika jitihada za kutokomeza ugonjwa huo.
Juhudi hizo zinatoa msukumo kwa Watanzania kutambua kuwa bado kuna kazi ya kufanya ambapo lengo la taifa ni kuhakikisha maambukizi ya ugonjwa wa malaria yanapungua  hadi asilimia 5 mwaka 2016 na asilimia 1 ifikapo mwaka 2020.
Hatua hiyo inawezekana kufikiwa na taifa ikiwa kila mtu anawajibika kwa nafasi yake kushiriki katika kupambana na vita dhidi ya malaria.
Ukiona vya elea ujue vimeundwa, hatua ambazo zimesababisha kupungua kwa maambukizi ya ugonjwa huo zinatokana na juhudi mbalimbali zinazosimamiwa vema na viongozi wenye dhamira ya dhati ya kupambana na adui wa taifa ambaye maradhi.
Rais Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Kikwete wakati wa uongozi wake na hata baadha ya muda wake wa uongozi amekuwa msari wa mbele katika kupambana na adui wa taifa ambaye miongoni wao ni ugonjwa malaria.
Jitihada zake za kupambana na malaria ndani na nje ya nchi zimeonesha tija na zimezaa matunda na kupelekea kutunukiwa tuzo iliyotukuka ya “White House Summit Award” mapema Aprili mwa huu ndio maana waswahili husema “Chanda chema huvikwa pete”.
Je? Mimi na wewe, tumejifunza nini katika kupambana na ugonjwa wa malaria? Tambua zama zimebadilika, si kila homa ni malaria, chukua hatua nenda kituo cha afya kilicho karibu nawe uweze kupima afya yako badala ya kuanza kutumia dawa bila kufanya vipimo.
Vipimo ndio iwe mwalimu na mwongozo wa kujua mtu anasumbuliwa na ugongwa gani ndipo aweze kutumia dawa sahihi za kupambana na adui anayemsumbua.
Hadi sasa nchini, Serikali inapaswa kupongezwa kwa kuanzisha utaratibu kabambe wa kupambana na ugonjwa wa malaria ambapo watu watakaoenda kupima ugonjwa huo katika zahanati, vituo vya afya na hospitali mbalimbali za umma wanakiwa kupima bure na mara baada ya wakigundulika kuwa wana ugonjwa wa malaria wanapswa kupewa dawa za kutibu ya ugonjwa huo bure.
Hatua hiyo njema ni na ya kupongezwa na kila mpenda na mthamini uhai,   Waziri mwenye dhamana ya afya nchini chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu alipokuwa akitoa tamko la maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani mjini Dododma amesisitiza kuwa huduma ya vipimo na matibabu ya ugonjwa wa malaria itakuwa intolewa bure isipokuwa malipo ya kumuona daktari ndio yanapaswa kulipwa.
Kwa hatua hiyo itaifikisha Tanzania kujiridhisha na usemi wa “Tanzania bila malaria inawezekana” maana wananchi sasa wamepunguziwa mzigo mkubwa uliokuwa ukiwasumbua kwa muda mrefu na kuwafanya watu wengi kupoteza maisha kabla hata ya kufikishwa vituo vya afya kutokana na kukosa fedha za kupata matibabu.
Hatua hiyo ya taifa ya kupambana na malaria ni njia na mwanga bora kwa kuwa na watu wenye afya njema ambao watakuwa mstari wa mbele katika kujenga na kuhakikisha nchi inafikia uchumi wa kati ifikapo 2025.
Akitoa tamko katika kilele cha maadhimisho ya siku ya malaria duniani mjini Dodoma, Waziri Ummy alisema kuwa Watanzania ni lazima kutambua maadhimisho hayo ya Malaria nchini yapaswa kuwa chachu ya wananchi kupima na kuthibitisha kama wana vimelea vya malaria kabla ya kuanza kutumia dawa.
Waziri Ummy aliongeza kuwa pale mtu anapogundulika kuwa ana malaria, anapaswa kuhakikisha anatumia dawa na kumaliza kozi nzima kulingana na maelekezo ya daktari.
Katika kuhakikisha taifa linapambana na ugojwa wa malaria, Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti wa Mbu Waenezo Malaria Charles Damas anabainisha umuhimu wa jamii kushiriki kikamilifu katika kuharibu mazalia ya mbu kwa kufukia madimbwi ya maji, kusafisha mifereji na kuweka mazingira safi ili kuondoa maji yanayotuama hatua ambayo itachangia kupunguza maambukizi ya malaria.
Ni dhahiri Tanzania sio kisiwa, imeendele kuwa na mahusiano mazuri na mataifa rafiki pamoja na wadau wengine wa maendeleo katika kupambana na ugonjwa wa malaria nchini.
Wadau ambao wapo mtari wa mbele katika mapambano ya malaria ni pamoja na Mfuko wa Dunia wa kushughulikia ugonjwa wa UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria, Mfuko wa Rais wa Marekani wa Kushughulikia Malaria (PMI), Shirika la Misaada la Uingereza (DFID), Shirika la Maendeleo la Uswisi (SDC), Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika la UNITAID,Taasisi zisizo za Kiserikali, Sekta Binafsi kupitia Mpango wa malaria Safe na Taasisi za Utafiti za NIMRI na Ifakara.
Katika kupambana na adui maradhi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, alitoa mwongozo wa Serikali yake kupitia hotuba yake ya kufungua rasmi Bunge jipya la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,mjini Dodoma Novemba 20, 2015 ambapo alibainisha dhamira ya dhati katika masuala ya afya.
Rais Dkt. Magufuli anasema “Dhamira ya kujenga uchumi wa kisasa na suala la kupambana na umasikini linakwenda sambamba na kuwa na wananchi wenye afya bora. Kwa kutambua ukweli huu na mahitaji ya huduma bora za wananchi wetu Serikali ya Awamu ya Tano itahakikisha kwamba wananchi wanapata huduma bora za afya”.
Dhamira hiyo ya Serikali ni kuimarisha huduma za afya sehemu ambapo huduma hizo zipo na kuanzisha pale ambapo hazipo ikiwa na lengo la kuhakikisha kila kijiji kinakuwa na Zahanati, kila Kata inakuwa na Kituo cha Afya, kila wilaya inakuwa na Hospitali, na kila Mkoa unakuwa na hospitali ya Rufaa.
Ni dhahiri nia ya Serikali ya kuboresha huduma za afya nchini itasaidia kuongeza utaalamu katika sekta ya afya kwa kuwapatia mafunzo watumishi wake ndani na nje ya nchi, kuzipatia vifaa bora na vya kisasa hospitali, vituo vya afya na zahanati zilizopo nchini.
Lengo hilo la Serikali kuchukua hatua hizo itasaidia kuwezesha upatikanaji wa huduma mahsusi hapa nchini na hivyo kutolazimika kupeleka wagonjwa kutibiwa nchi za nje.
Ili kufanikisha hayo, Rais alisema kuwa Serikali yake itaendelea kuongeza bajeti ya dawa na kuboresha mfumo wa upatikanaji wa dawa hizo ili kuhakikisha zinapatikana katika hospitali, vituo vya afya na zahanati na kuhamasisha wananchi wajiunge na Bima ya Afya ili kuwa na uhakika wa kupata huduma za afya mahali popote nchini na wakati wowote.
Alipokuwa akitoa tamko hilo siku ya maadhimisho ya Siku ya Malaria Duniani, Waziri Ummy aliongoza kupimwa kujua kama ana vimelea vya malaria ambapo waaandishi wa habari ambao walihudhuria wakati tamko hilo kutolea mjini Dododma waliungana naye kujua hali ya afya zao.
Ili kutokomeza ugonjwa wa malaria nchini, kila mtu anapaswa kuzingatia kupima ili kujua uwepo wa vimelea vya malaria kabla ya kutumia dawa, kumaliza kozi ya dawa kulingana na maelekezo ya daktari na mtoa huduma, kutumia vyandarua vyenye viaatilifu kila siku wakati wa kulala pamoja na kuzingatia usafi wa mazingira kuzuia mazalia ya mbu katika maeneo yanayozunguka nyumba zao.
Jukumu la kupambana na malaria sio la mtu moja, halmashauri  zao zinapaswa kuboresha takwimu zao ili kujua ukubwa wa tatizo la malaria katika halmashauri zao na kuweka bajeti kwenye mipango yao ya halmashauri (CCHP) kwa ajili ya udhibiti wa mbu.
Majukumu mengine ya halmashauri ni kuhakikisha miongozo ya uchunguzi na tiba ya malaria inazingatiwa katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya vya umma na vya sekta binafsi pamoja na kufanya ufuatiliaji katika vituo vya kutolea huduma vya umma na vya sekta binafsi ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.
Juhudi hizo kupambana na ugonjwa wa malaria sio za kuachiwa Serikali tu, kila mtu awajibike na atambue kuwa zama zimebadilika, “Sio kila homa ni malaria, nenda ukapime” na “lala kwenye chandarua kila siku” kujikinga na malaria.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni