 Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza
 na Makamanda wa Polisi, Wanasheria wa Serikali,  Wafawidhi wa Mikoa na 
Wakuu wa upelelezi wa Mikoa na Vikosi kabla ya kufungua rasmi Kikao kazi
 cha Makamanda hao wa Polisi katika Ukumbi wa Dodoma Convention Center
Rais
 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza
 na Makamanda wa Polisi, Wanasheria wa Serikali,  Wafawidhi wa Mikoa na 
Wakuu wa upelelezi wa Mikoa na Vikosi kabla ya kufungua rasmi Kikao kazi
 cha Makamanda hao wa Polisi katika Ukumbi wa Dodoma Convention Center 
…………………………………………………………………………………………
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amelitaka Jeshi la Polisi nchini na 
Ofisi ya Mwendesha Mashitaka kujirekebisha kwa kutekeleza wajibu wao 
huku wakitanguliza maslahi ya taifa.
Rais Magufuli ametoa maagizo hayo
 leo tarehe 29 Aprili, 2016 wakati akifungua kikao cha kazi cha 
Makamanda wa polisi wa mikoa, Mawakili wafawidhi wa serikali  wa Mikoa 
na Wakuu wa upelelezi wa Mikoa na Vikosi, kinachofanyika kwa siku mbili 
katika ukumbi wa Mikutano wa Dodoma uliopo katika eneo la Tambukareli 
Mjini Dodoma.
Awali kabla ya kutoa hotuba yake 
Rais Magufuli aliwapa nafasi Makamanda na Mawakili Wafawidhi hao kutoa 
maoni yao juu ya changamoto zinazowakabili katika kutekeleza wajibu wa 
kufanya upepelezi na kuendesha mashitaka, hususani kujua sababu za 
kuchelewesha kesi za makosa ya jinai, ambapo wamedai ufinyu wa bajeti 
ndio sababu kubwa ya kucheleweshwa kwa kesi za hizo.
Kufuatia kutajwa kwa changamoto 
hiyo Rais Magufuli ameahidi kuhakikisha anawatafutia fedha kwa ajili ya 
kukabiliana nazo, lakini ametaka fedha zitakazotafutwa zitumike vizuri 
kwa kuwa taarifa zinaonesha Jeshi la Polisi limekuwa likihusishwa na 
matumizi mabaya ya fedha hali inayoongeza ukubwa wa matatizo 
yanayokwamisha utendaji wake wa kazi.
Ametolea mfano wa taarifa za 
matumizi mabaya ya fedha zinazotolewa kwa ajili ya kununulia vifaa na 
sare za askari, ama mikataba yenye mashaka inayotiwa saini kati ya 
Polisi na wawekezaji kuwa ni baadhi ya mambo yanayoongeza hali ngumu ya 
utendaji kazi kwa jeshi hilo.
“Oysterbay pale ni eneo 
ambalo ni very prime, kila mmoja anajua, mmeingia kwenye mikataba 
mnayoijua nyinyi, akapewa mtu anawajengea pale, sifahamu kama majengo 
hayo yanafaa. Palikuwa na ubaya gani eneo la Oysterbay likawa na hati, 
mkaitumia hiyo hati kwenda kukopa benki na kujenga nyumba hata za 
ghorofa 20 pale, mkaweka investment  na Polisi wenu wakakaa pale. 
Nimesema lazima nizungumze kwa uwazi, nisiposema kwa uwazi nitajisikia 
vibaya nikimaliza mkutano huu, nataka muelewe na muelewe ukweli direction  ninayoitaka mimi” Amesema Rais Magufuli
Aidha, Rais Magufuli ameitaka 
Ofisi ya mwendesha Mashitaka wa Serikali kujipanga kufanya kazi kwa 
ufanisi na ameelezea kusikitishwa kwake na vitendo vya serikali 
kushindwa katika kesi nyingi mahakamani licha ya kuwa na wanasheria 
mahiri.
“Niwaombe mawakili na polisi 
wanaohusika na upelelezi mtangulize maslai ya nchi mbele, kwa sababu 
kumekuwa na usemi kwa baadhi ya wapelelezi na mawakili wachache, nasema 
wachache, panapokuwa na kesi inayohusiana na pesa pesa, wana misemo yao 
wanasema dili limepatikana, na saa nyingine kesi inapopelekwa mahakamani
 wana-collude Mawakili wa serikali na mawakili wanaomtetea  mhalifu, na 
wanapo-collude siku zote serikali inashindwa. Unapoona hali hiyo ya kila
 siku serikali inashindwa, halafu siku hiyo unataka serikali ikuwezeshe,
 kwa vyovyote serikali inapata kigugumizi” amesisitiza Rais Magufuli.
Dkt. Magufuli pia amelitaka Jeshi
 la Polisi kujiepusha na kashfa ambazo zimekuwa zikisemwa dhidi yake, 
ikiwemo maafisa wa Polisi kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya na 
kuazimisha silaha kwa wahalifu wa ujambazi.
Hata hivyo Rais Magufuli 
amelipongeza Jeshi la Polisi na ofisi ya Mkurugenzi wa  Mashitaka kwa 
kazi kubwa wanayoifanya na ametaka apelekewe mpango wa mahitaji yao ili 
atafute namna ya kuimarisha vyombo hivyo.
Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dodoma
29 Aprili, 2016