ZIARA YA WAZIRI NAPE NA RIPOTI KAMILI YA TFF
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye 
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Jamal Malinzi.
………………………………………………………………………..
Ripoti ya mwenendo wa mpira wa 
miguu Tanzania na mipango yake inayofanywa na Shirikisho la Mpira wa 
Miguu Tanzania (TFF), imemfurahisha Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa 
na Michezo, Nape Nnauye hivyo moja kwa moja akaupongeza uongozi wa Rais 
Jamal Malinzi akisema unafanya kazi kubwa.
Kutokana na ripoti hiyo, Nape 
ambaye ni Mbunge wa Mtama mkoani Lindi, aliridhia wadau wa mpira wa 
miguu kusapoti timu za taifa hususani Serengeti Boys – timu ya taifa ya 
vijana wenye umri chini ya miaka 17 ambayo kwa sasa imepiga kambi 
Shelisheli kujiandaa kuivaa Congo-Brazzaville Jumapili ijayo.
Serengeti Boys inawania kucheza 
Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana wenye umri katika fainali 
zitakazofanyika Antananarivo, Madagascar sawa na timu ya taifa ya soka 
la ufukweni ambayo inatarajiwa kusafiri kwenda Abidjan, Ivory Coast 
kucheza mchezo wa pili wa kuwania kufuzu fainali za Kombe la Mataifa ya 
Afrika kwa mchezo huo.
Timu nyingine ya taifa ni ile ya 
wanawake ya Tanzania Bara maaarufu kwa jina la ‘Kilimanjaro Queens’ 
ambayo kwa sasa iko Uganda kuwania taji la Chalenji ikishirikisha timu 
za taifa za Afrika Mashariki katika michuano ya inayotarajiwa kufanyika 
jijini Jinja kwa siku tisa kuanzia Septemba 11, mwaka huu.
Nape amefurahishwa na mipango ya 
TFF baada ya kupeleka timu zote kushiriki michuano mbalimbali kwa 
vipindi mbalimbali na kwamba Serikali itasapoti lakini hapo baadaye 
baada ya kufuata taratibu mbalimbali baada ya Rais Malinzi kumfafanualia
 kuwa gharama za kuendesha mpira kwa mwaka zinafika shilingi bilioni 15,
 na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) huchangia asilimia 
tatu (3) tu ya bajeti nzima kwa mwaka.
“Kwa kuanzia msimu huu tu, FIFA 
imeongeza na sasa itafika asilimia 6 kwa mwaka,” alisema Malinzi jambo 
ambalo lilimshangaza Nape ambaye leo Septemba 10, 2016 alifanya ziara ya
 kutembelea TFF kujionea hali halisi na kushangazwa na taarifa za vyanzo
 mbalimbali zinazotuhumu shirikisho.
Nape alisema: “Serikali inasapoti maendeleo, lakini lazima yafuate taratibu, kanuni na sheria za soka.”
Katika eneo la kufuata taratibu, 
kanuni na sheria za soka hatua nyingine, Nape alitaka Malinzi na kamati 
zake kuwa wakali kwa kuwa huwa hawachui hatua mapema, inatokea wadau 
kutaka kuipanda kichwani TFF.
“Naagiza mchukue hatua mapema 
kukamua majipu kabla hajajaiva. Sasa ninyi mnasubiri kwa muda mrefu 
kabla ya kuchukua hatua, ndiyo maana wanawasumbua. Washughulikieni 
mapema, mkiwabana mapema watakaa kimya, kanuni mnazo, sheria mnazo, 
wabaneni,” alisema Nape.
Katika hatua nyingine, Nape 
alisema kwamba kuna mchakato unaendelea kwa sasa ndani ya Chama Cha 
Mapinduzi (CCM) kuhakikisha kwamba wanarejesha mamlaka ya kumiliki 
baadhi ya viwanja vya soka Makao Makuu ya chama badala mikoa ambako 
wamegundua kuwa kuna matatizo makubwa katika menejimenti.
NA HIZI NDIZO SALAMU ZA RAIS WA 
TFF, JAMAL EMIL MALINZI KWA MHESHIMIWA NAPE NNAUYE WAZIRI WA HABARI, 
UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO UWANJA WA KARUME TAREHE 10 SEPTEMBA 2016
Mheshimiwa Waziri,
Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutukutanisha hapa leo.
Ni jambo la heshima na furaha 
kubwa sana  kwetu sisi wanafamilia ya mpira wa miguu Tanzania kwa 
kutembelewa na wewe Mheshimiwa Waziri na ujumbe wako. Mheshimiwa ahsante
 sana kwa tukio hili adhimu na karibu sana kwenye makazi ya mpira “home 
of football”.
Mheshimiwa Waziri tunashukuru 
kwamba umeweza kutembelea eneo letu na kujionea wapi huwa tunafanyia 
shughuli zetu mbali mbali za kuendeleza michezo.
Shirikisho la mpira wa miguu 
Tanzania TFF limesajiliwa chini ya sheria ya baraza ya mwaka 1967 na 
marekebisho yake ya mwaka 1971  na madhumuni yake makuu  ni kuendeleza 
na kusimamia mpira wa miguu Tanzania. Katika kutekeleza azma hii 
shughuli zetu tumezigawanya katika maeneo makuu matano:
- Utawala
Shughuli za kila siku za 
uendeshaji wa mpira wetu zinasimamiwa na Sekretariet ya TFF inayoongozwa
 na Katibu Mkuu Ndugu Mwesigwa Selestine. Chini yake ana vitengo vikuu 
vitano: Ufundi ambacho kinasimamia maendeleo ya mpira, Mashindano 
ambacho kinasimamia mashindano mbali mbali, Fedha na utawala, Sheria na 
vyama wanachama na cha tano ni cha biashara na masoko. Vitengo hivi kwa 
pamoja vinashirikiana kuhakikisha mpira unafundishwa, unachezwa na 
unasimamiwa vyema. Aidha zipo Kamati mbali mbali zinazotusaidia 
kutushauri kwenye mambo ya kitaalam na kutoa maamuzi vikiwa vyombo huru.
 Pia tunacho chombo chetu kinachoitwa Bodi ya Ligi kinachosimamia 
uendeshaji wa ligi zetu kuu tatu Ligi kuu ya daraja la kwanza na ya 
daraja la pili. Ligi kuu ya vilabu vya wanawake  inaendeshwa na kamati 
ya mpira wa wanawake.
- Mashindano
Ili mpira uchezwe inabidi kuwepo 
na mashindano. Wakati wote TFF inafanya jitihada za kubuni mashindano 
mapya na kuhakikisha yaliyopo yanafanyika kwa mujibu wa kalenda. Kwa 
sasa TFF tunaendesha mashindano makuu ya kitaifa saba: Ligi kuu, Ligi 
daraja la kwanza, Ligi daraja la pili, Ligi ya mikoa, Kombe la 
Shirikisho, Ligi ya vijana na Ligi ya vilabu vya wanawake. Ukiondoa ligi
 daraja la pili na ligi ya mikoa mashindano yaliyobakia yote yanaonekana
 moja kwa moja kwenye (live) kwenye Televisheni. Shirikisho liko mbioni 
kuanzisha mashindano ya vilabu nane bora vya ligi kuu (Super 8). TFF pia
 huwa inasimamia mechi mbali mbali za kimataifa za mashindano na za 
kirafiki kwa timu za Taifa za rika mbali mbali za   wanawake na wanaume.
- Masoko na Biashara
Kuendesha mpira ni gharama kubwa. 
 Wastani wa bajeti ya Shirikisho ni  shilingi bilioni kumi na tano kwa 
mwaka.Tunawashukuru FIFA ambao hadi mwaka jana walikuwa wanachangia 
asilimia 3% ya bajeti hii na kuanzia mwaka huu wanachangia asilimi 6% ya
 bajeti hii.  Jitihada kubwa zimekuwa zikifanyika kuhakikisha shughuli 
za uendeshaji wa mpira hazikwamishwi na ukosefu wa fedha. Kitengo cha 
biashara na masoko kinafanya jitihada kubwa kuhakikisha kila shindano 
letu linakuwa na udhamini hata kama sio wa kukidhi mahitaji yote.
- Miundombinu
Ni muhimu sana kuwa na miundo 
mbinu ya kutosha na yenye sifa ya kuchezewa mpira. Kwa kushirikiana na 
wamiliki mbali mbali wa viwanja vya mpira  TFF tumekuwa tukitoa ushauri 
wa namna ya kuendeleza na kutunza viwanja vyetu vya mpira ili vifae 
kuchezewa mpira wa kisasa. Aidha tunashukuru Halmashauri ya jiji la 
Tanga kwa kuiipatia TFF miliki ya eneo la ekari 18 jijini Tanga, kwa 
kushirikiana na FIFA eneo hilo litajengwa kituo cha kukuza na kuendeleza
 vipaji vya mpira cha TFF. Michoro yake  iko katika hatua za mwisho za 
maandalizi.
- Maendeleo ya mpira wa miguu.
TFF tumejiwekea malengo mawili 
makuu: Kucheza fainali za dunia mpira wa miguu wa wanawake Paris mwaka 
2019 na kucheza fainali za kombe la dunia wanaume mwaka 2026.
Kwa upande wa mpira wa wanawake 
katika kufikia azma hii mwaka huu tunaanzisha ligi kuu ya vilabu vya 
mpira wa wanawake (Tanzania Women Premier League). Kutokana na ligi hii 
vipaji vitaibuliwa kwa ajili ya kuimarisha kikosi cha timu yetu ya Taifa
 Twiga stars. Kikosi hiki mwakani kitakuwa kikikusanywa mara kwa mara, 
kufanya mazoezi na kucheza mechi za kirafiki  za kimataifa ili kujiandaa
 na hatua za awali za kombe la dunia mwaka 2018.
Kwa upande wa maandalizi ya Taifa 
stars kuelekea mwaka 2026 tayari program yetu imeanza kwa kuwa na 
Serengeti Boys ambayo inapambana kucheza fainali za vijana za Afrika 
mwakani umri chini ya miaka 17. Kwa sasa kikosi hiki kiko kambini 
Seychelles kujiandaa na mechi dhidi ya Kongo tarehe 18 Septemba . Timu 
hii pia ndiyo itapambana kucheza fainali za Afrika za vijana umri chini 
ya miaka 20 mwaka 2019. Aidha kwenye shule ya Alliance huko Mwanza 
tayari tuna kikosi cha awali cha timu ya  Taifa cha vijana umri chini ya
 miaka 15 ambacho kinaandaliwa kucheza fainali za Afrika umri chini ya 
miaka 17 mwaka 2019. Tanzania tutakuwa wenyeji wa fainali hizi kwa mara 
ya kwanza katika historia ya nchi yetu.
Pia mwaka huu tunaanzisha ligi ya 
Taifa ya vijana umri chini ya miaka 20. Kutokana na ligi hii mwakani 
itaundwa timu ya Taifa ya awali ya vijana  umri chini ya miaka 23 
itakayopambana mwaka 2019 kutafuta fursa ya kucheza fainali za Olimpiki 
 Tokyo mwaka 2020. Kutokana na makundi haya makuu matatu kuanzia mwaka 
2021 walimu wetu wa mpira wataweza kuanza kutengeneza kikosi imara cha 
Taifa stars kuelekea Fainali za Kombe la dunia 2026. Gharama kubwa 
zinahitajika kugharimia program hizi na tunaomba Serikali na wadau 
wengine mtushike mkono ili tufikie azma yetu ya kucheza World Cup 2026.
Mheshimiwa Waziri ninaomba nigusie
 uendeshaji wa ligi yetu kuu na utoaji wa leseni za vilabu.Kama 
nilivyosema hapo awali Ligi kuu inasimamiwa na bodi ya ligi kwa 
maelekezo ya kanuni za mashindano kama zinavyopitishwa na kamati ya 
Utendaji kila mwaka. Mheshimiwa Waziri kinacholiongoza Shirikisho katika
 uendeshaji wa ligi kuanzia usajili, upangaji wa ratiba,upangaji wa 
waamuzi na utoaji wa adhabu ni kwa mujibu wa kanuni tulizojiwekea na 
kauli mbiu ya #fairplay,haki mchezoni.
Ninaomba nieleze pia kuwa kufuatia
 maagizo ya FIFA sasa tupo hatua za awali za  kutoa leseni kwa vilabu 
zinazohalalisha vilabu kushiriki katika ligi. Mahitaji makuu ya leseni 
hizi ni klabu kuwa na menejimenti na kumbukumbu za mahesabu yake ya 
fedha ,kuwa na maeneo ya kufanyia mazoezi na kucheza mechi,kuwa na 
program za maendeleo ya mpira wa vijana na mwisho kueleza kinagaubaga 
nani anamiliki na kuendesha shughuli za kila siku za za klabu (ownership
 and control). Katika hili la umiliki ni marufuku klabu zaidi ya moja 
katika ligi moja kumilikiwa na mtu au mamlaka moja. Pia kanuni ya leseni
 za vilabu ina kipengele cha kipimo cha sifa cha nani anaruhusiwa 
kumiliki au kuendesha klabu ya mpira wa miguu , mipaka ya mamlaka yake 
na mahusiano na Shirikisho na mamlaka nyingine za juu zikiwemo 
Serikali,FIFA,CAF na CECAFA.
Mheshimiwa Waziri, ninaomba 
nimalizie kwa kukushukuru tena kwa kuchukua muda wako kuwa na sisi leo. 
Familia ya mpira wa miguu Tanzania inafarijika sana unapokuwa karibu na 
sisi na tunaahidi kuendelea kudumisha nidhamu katika utendaji wetu na 
kutoa ushirikiano wa karibu kwa Serikali yetu, vyombo na mamlaka 
nyingine.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni