MAANDAMANO NI LAZIMA YAFUATE SHERIA”- KAMANDA MSTAAFU TIBAIGANA
Kamanda Mstaafu Tibaigana
……………………………………..
          Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO
Kamanda Mstaafu Kanda Maalumu ya 
Dar es Salaam kuanzia mwaka 2001 hadi 2008, Alfred Tibaigana amesema 
kuwa maandamano ya aina yoyote ni haki ya mwananchi na yanaruhusiwa 
kisheria lakini maandamano hayo lazima yafuate sheria na taratibu 
zilizobainishwa katika Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kamanda Tibaigana alitoa kauli 
hiyo hivi karibuni katika mahojiano maalum na mwandishi wa habari hizi 
kwa njia ya simu akisisitiza kuwa kila jambo linalofanyika hapa duniani 
ni lazima liongozwe kwa Sheria na Kanuni.
Ingawa sheria nyingi za nchi 
mbalimbali duniani zinafanana lakini kila nchi imejiwekea sheria na 
kanuni za kufuata katika kufanya jambo lolote au katika kutafuta suluhu 
ya migogoro mbalimbali ikiwemo ya kisiasa, kidini, kijamii pamoja na ya 
kiuchumi.
Tanzania ni nchi mojawapo 
inayoongozwa kwa Sheria na Kanuni mbalimbali na ndio sababu hata katika 
Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa nchi imeeleza wazi kuwa hakuna aliye 
juu ya sheria wala hakuna anayeruhusiwa kuzivunja sheria hizo.
Anasema kuwa ili Taifa litengemae 
ni lazima wananchi wafuate Sheria na Kanuni zilizowekwa kwa sababu 
kutofuata sheria ni kosa kubwa.
Tibaigana anaongeza kuwa Sheria ni
 msumeno, ni vema kila pande ikaheshimu sheria na kanuni hasa kwa 
kutambua madaraka ya kila mmoja yanaanzia wapi na yanaishia wapi ili 
kuzuia tatizo la muingiliano wa majukumu ambao unaweza kusababisha 
uvunjifu wa sheria na kanuni zilizowekwa na nchi husika.
Aidha, Katiba ya Jamuhuri ya 
Muungano wa Tanzania imeelezea kwa undani pamoja na kuweka sheria na 
kanuni zinazohusu maandamano ya aina yoyote ,yawe ya kisiasa, kidini, 
kijamii au ya kiuchumi.
“Sheria inamtaka mwananchi au 
kundi la wananchi wanaohitaji kufanya maandamano kutoa taarifa kwa 
maandishi kwa Mkuu wa Polisi wa eneo husika kabla ya masaa 48 ya kuanza 
kwa maandamano hayo ikieleza dhumuni la maandamano hayo, pia wahusika 
wanatakiwa wawe tayari kwa jibu lolote kutoka kwa mkuu huyo kwa kuwa 
chochote watakachojibiwa  lazima kiwe na sababu”, anasema Tibaigana.
Tibaigana anafafanua kuwa kama 
wahusika watakataliwa kufanya maandamano na hawatoridhishwa na sababu 
zilizotolewa na Mkuu wa Polisi kuna hatua mbili muhimu zinazotakiwa 
zifuatwe na sio wahusika kujiamulia kuandamana kilazima kwa kuwa kufanya
 hivyo ni kosa.
Hatua hizo muhimu zinazotakiwa 
kufuatwa ni kuandika barua kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na 
kumueleza kuwa hawajaridhika na sababu zilizotolewa na  Mkuu wa Polisi 
ili waziri naye kwa upande wake aamue kuruhusu au kukataza, endapo 
wahusika hawatoridhika na majibu ya waziri, watatakiwa kwenda Mahakamani
 ambapo ndipo uamuzi wa mwisho utatolewa.
Anasisitiza kuwa hakuna sheria 
inayotambua maandamano ya nchi nzima kufanyika kwa siku moja kwa sababu 
kila eneo lina Mkuu wa Polisi mwenye haki ya kukubali au kukataa ombi la
 kufanya maandamano kulingana na hali halisi ya eneo lake.
Kila jambo lina faida na hasara 
zake lakini kuna mambo ambayo faida huwa chache kuliko hasara, 
maandamano yana athari kubwa kiuchumi na kijamii kwa sababu maandamano 
yoyote ni lazima Jeshi la Polisi liwajibike katika kuongoza na kulinda 
maandamano hayo, hivyo kupelekea wanajeshi wengi kusitisha kazi zingine 
kwa ajili ya kuzuia vurugu zisitokee.
Athari zingine ni kusitishwa kwa 
shughuli mbalimbali zikiwemo za usafiri , kufungwa kwa maduka na masoko 
pamoja na athari zitokanazo na vurugu zinazoweza kutokea kwa sababu ya 
maandamano hayo.
Aidha, Kamanda Tibaigana anatoa 
ushauri kwa vyama vya siasa vinavyotumia maandamano kama njia ya kupata 
usuluhishi wa migogoro yao kufata sheria na kanuni zilizowekwa kwani 
maandamano mengi ya aina hiyo yanasababishwa na kutaka nafasi ya 
kuongoza nchi kwahiyo kama chama hakitoheshimu sheria za nchi lazima 
kiwe mfano mbaya kwa wananchi watakaowaongoza.
Watanzania wanatakiwa kuelewa kuwa
 maandamano sio njia pekee ya kusuluhisha migogoro yao bali njia bora ni
 kukaa chini na kuelewana kwa njia ya mazungumzo, huo ndio utamaduni wa 
nchi yetu kwani hali hiyo ya kutii sheria na kanuni umepelekea nchi 
kuendelea kuwa na amani wakati wote.
“Sisi ndio walinzi wa amani hiyo kwahiyo yatupasa kuzitii sheria zetu ili kuitunza amani yetu daima”.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni