Jumamosi, 17 Septemba 2016

HOTUBA YA MGENI RASMI
WAZIRI WA NCHI – OFISI YA RAISI TAMISEMI
Mh. GEORGE SIMBACHAWENE
KATIKA UFUNGUZI WA SIKU YA USOMAJI DUNIANI
TAREHE 16 SEPTEMBA 2016
UKUMBI WA KARIMJEE – DAR ES SALAAM.

Waheshimiwa mabalozi,
Muwakilishi wa UNESCO
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,
Wakuu wa wilaya
Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri
Maafisa elimu
Makampuni washirika
Mashirika ya kimataifa
Mashirika wahisani
Mashirika yasiyo ya kiserikali
Waalimu wa shule mbalimbali
Waandishi wa habari
Wanafunzi
Ndugu waalikwa
Mabibi na Mabwana

Kwanza napenda kuchukua nafasi kutoa shukrani kwa kuniarika katika siku muhimu ya kujipima hali yetu ya usomaji na kunipa jukumu kubwa la kuwa mgeni rasmi katika sherehe hizi za Siku ya Kimataifa ya Usomaji. Binafsi nimefarijika kuona ushirikiano uliopo miongoni mwa mashirika na taasisi zinazojishughulisha na kuboresha elimu hapa nchini. Kama mnavyojua, hiki ni kipindi cha Bunge, lakini kutokana na umuhimu wa tukio hili la leo, nimeamua kushiriki nanyi.

Mnamo mwaka 1965, mkutano wa dunia wa mawaziri wa elimu ulikutana huko Tehran nchini Iran kuzungumzia jinsi ya kufuta ujinga duniani. Moja ya mapendekezo ya Tehran ni kuanzishwa kwa siku ya Usomaji duniani, kuendeleza dhana ya usomaji endelevu. Mwaka 1966, Siku ya Usomaji Duniani ilisheherekewa chini ya usaidizi wa UNESCO na washirika wake.

Mwaka 2015, viongozi wa nchi mbalimbali duniani walikubaliana na kupitisha malengo endelevu ya maendeleo, na lengo la nne limejikita katika kuhakikisha tunafuta ujinga kabisa ifikapo mwaka 2030. Safari hii si nyepesi na serikali pekee haiwezi kuitembea peke yake, bado ushirikiano wa wadau wote wa elimu utahitajika, na tayari tunaona taasisi nyingi zimeianza safari hii, na hii imetupa changamoto kwa upande wetu wa serikali.

Ndugu zangu wadau, kama wote tunavyojua, moja ya malengo katika ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, ni kuhakikisha kila mtoto nchini anapata nafasi ya elimu tena bure kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne. Kongamano mtakalofanya leo, limekuja kwa muda muafaka, wakati serikali tunatafakari tutawezaje kuboresha mfumo mzima wa elimu nchini na kuhakikisha kila mtoto anaweza kusoma na kuandika vizuri afikapo darasa la tatu.

Ninajua shirika kama Room to Read limekuwa likichangia sana kuboresha hali ya usomaji hapa nchin, kwa kutujengea maktaba katika shule za msingi, na kuweka vitabu vyote stahiki, wanawafundisha waalimu wetu wa darasa la kwanza na la pili mbinu na stadi za ufundishaji, na kuhakikisha vitabu vya kufundishia vipo shuleni na vitabu vya wanafunzi vya kujifunzia kwa kitabu kimoja kwa mwanafunzi mmoja. Mchango wao umeweza kuonyesha njia kuwa wanafunzi wanaweza kujua kusoma na kuandika vizuri wanapoingia darasa la tatu.

Ndugu zangu wadau, pia wote tunajua kuwa Raisi wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Magufuli ameongeza mkakati katika kuboresha elimu kwa kuhakikisha kila mtoto aliyeko shuleni anakaa kwenye dawati, juhudi zake zimezaa matunda mazuri sana na kupunguza uhaba mkubwa sana wa madawati, nipende kutumia fursa hii kuwashukuru nyote na hususani mashirika na taasisi zilizojitoa kwa dhati kuchangia juhudi hizi. Hata hivyo, juhudi hizi zimeibua changamoto ya vyumba vya madarasa, tunaendelea na juhudi za kupunguza uhaba huu kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwemo taasisi za wengi wenu mliopo hapa, wananchi wa maeneo ya shule zilipo na wafadhili mbalimbali.  

Takwimu za kitaifa za sensa ya makazi na watu ya mwaka 2012, inaonyesha asilimia 22 ya watanzania hawawezi kusoma na kuandika kwa ufasaha, asilimia 81.7 ya wantanzania wana elimu ya msingi, asilimia 14.4 elimu ya sekondari na asilimia 2.3 tu ndio walio na elimu ya chuo kikuu. Kiwango hiki kidogo kwa kadiri elimu inavyoenda juu kinasababishwa na kutokuwa na msingi imara kipindi cha mwanzo wa kuanza safari ya elimu. Hakuna mzazi anayempeleka mtoto wake shule ili amalize akiwa hajui kusoma na kuandika, kila mzazi anapomuandikisha mtoto shule mtoto wake, anakuwa na matumaini makubwa juu yake, lakini matumaini hayo hufifia pale dalili za wazi zinapoonekana za kutojua kusoma na kuandika kwa ufasaha.

Kwa mfumo na juhudi zinazofanywa na Room to Read, katika kuhakikisha wanafunzi wanajua kusoma na kuandika wafikapo darasa la tatu, kuna jambo tunalotakiwa kujifunza sisi kama serikali kutoka kwao, mie binafsi nazijua kazi zao na matokeo ya kazi zao nayajua, ni wazi kwa mfumo huo uwezekano wa kuwa na asilimia 0 ya wasiojua kusoma na kuandika ifikapo mwaka 2030 ni mkubwa sana kwa Tanzania. Tayari wizara yangu tumeanza kufanya kazi kwa ukaribu sana na wadau mbalimbali wanaotusaidia katika elimu kuhakikisha lengo hili tunarifikia.

Ndugu zangu wadau, Serikali yetu ya awamu ya Tano ipo tayari kuunga mkono juhudi kama zenu za kuboresha elimu kwa manufaa ya watoto wetu, napenda kuwahakikishia kuwa mlango wa Wizara yangu upo wazi kwa wote walio tayari kushirikiana nasi katika kuutokomeza ujinga na sisi tutatoa ushirikiano mkubwa kwenye hilo.  

Ndugu zangu wadau, filosofia ya Room to Read ni ‘Mabadiliko ya Dunia Yanaaza na Watoto Walioelimika’ Filosofia hii inatugongea kengele ya kuamka kutoka usingizini, na kuchangia katika mabadiliko ya Tanzania kwa kuwa na watoto watakaojua kusoma na kuandika kwa ufasaha wafikapo darasa la Tatu.

Mwaka huu kauli mbiu ya Siku ya Usomaji ni “Kusoma yaliyopita, Kuandika Yajayo” (Reading the Past, Writing the Future). Wakati ni huu sana wa kuhakikisha tunatafakari safari yetu ya kufuta ujinga kabisa ifikapo mwaka 2030, ninatamani siku kama hii kila mwaka tuwe tunakutana na kupeana mrejesho wa wapi tumefika, ninajua mashirika kama Hakielimu, Twaweza na wengine wanaweza kutusaidia sana kwenye hili. Hata mijadala tutakayofanya hapo baadae, itakuwa inatusaidia katika juhudi za kuandaa yajayo.

Kwa mara nyingine tena, nawashukuruni sana kwa kunipa nafasi hii, na nina Imani kwa kushirikiana nanyi Tanzania tutaweza kufikia lengo la kufuta kabisa ujinga ifkapo mwaka 2030.


Asanteni.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni