SERIKALI INAPANGA WALIMU WA SAYANSI KATIKA MOJA KWA MOJA BADALA YA KUPITIA HALMASHAURI
Na Beatrice Lyimo-MAELEZO, Dodoma
………………………………………………..
Serikali imeanza kupanga walimu 
wa sayansi moja kwa moja katika shule badala ya Halmashauri kama 
ilivyokuwa awali ili kuleta uwiano sawa wa walimu katika shule 
mbalimbali nchini.
Hayo yamebainishwa na Naibu 
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Suleman Jaffo alipokuwa akijibu
 swali la Mbunge wa Muleba Prof. Anna Tibaijuka lililohusu mkakati wa 
Serikali katika kukabiliana na tatizo la upungufu wa walimu.
Naibu Waziri Jaffo amesema kuwa 
Serikali imeandaa mkakati wa kuwaajiri wahitimu wa shahada za sayansi 
ambazo siyo za ualimu baada ya kuwapa mafunzo ya muda mfupi kuhusu mbinu
 za ufundishaji na maadili ya ualimu ili kukabiliana na changamoto ya 
walimu wa sayansi nchini.
Naibu Waziri Jaffo amesema kuwa 
tayari kibali kimeombwa katika Ofisi ya Rais Utumishi kwa ajili ya 
utekelezaji huo, ambapo Serikali imepanga kuajiri walimu wastaafu wenye 
uwezo wa kufundisha waliokuwa wanafundisha masomo ya sayansi kwa mkataba
 ili kupunguza pengo lililopo.
Aidha, Naibu Waziri Jaffo 
amebainisha kuwa Serikali inafanya tathimini ya mahitaji ya walimu wa 
masomo ya sanaa kwa kila Halmashauri ili kubaini maeneo yenye ziada na 
yenye upungufu ili kusawazisha.
“Mpango wa Serikali uliopo ni 
kuwahamasisha walimu wa ziada wa masomo ya sanaa kwenda kufundisha 
katika shule za msingi ndani ya Halmashauri husika, ambapo kabla ya 
kuanza utekelezaji wa mabadiliko haya Serikali itatoa waraka maalumu 
kwenda katika Halmashauri zote nchini” amefafanua Naibu Waziri huyo.
Akizungumzia kuhusu utaratibu wa
 mafunzo ya walimu Mhe. Jaffo amesema kuwa Halmashauri moja haiwezi kuwa
 na mfumo wa peke yake wa kuandaa walimu hali ambayo iltakuwa ni vigumu 
kuthibiti ubora wa mafunzo hayo kwa walimu.
Hata hivyo amesema kuwa Serikali
 itaendelea kuongeza udahili wa walimu wa sayansi katika vyuo vya ualimu
 kadri watakavyojitokeza ili kukidhi mahitaji yaliyopo
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni