TETEMEKO: MALINZI AWAPA POLE KANDA YA ZIWA, BURUNDI NA UGANDA
Rais wa Shirikisho la Soka 
Tanzania (TFF), Jamal Malinzi ameshitushwa na taarifa za tukio la 
tetemeko kubwa ardhi lenye mtikisiko wa kipimo cha Ritcher 5.7 
lililotokea jana Septemba 10, 2016 katika mikoa mitatu ya Kanda ya Ziwa 
kadhalika nchi za Burundi na Uganda.
Mikoa ya Kanda ya Ziwa iliyopata 
athari kwa mujibu wa taarifa ni Mwanza, Mara na Kagera nchini na 
kuripotiwa kuua zaidi ya watu 10 na wengine zaidi ya 120 kujeruhiwa 
sambamba na kubomoa majengo mbalimbali.
Rais Malinzi mara moja 
anaungana na Serikali katika kusubiri tathmini na kisha kuangalia namna 
TFF itakavyoweza kusaidia kama sehemu ya wadau katika jamii. TFF 
inaamini kuwa baadhi ya waliopata maafa ni familia ya mpira wa miguu si 
ndani tu ya nchi, bali pia nje ya mipaka ya Tanzania.
Hivyo, Rais Malinzi ametutuma 
salamu za rambirambi kwa familia zote zilizopoteza ndugu, jamaa na 
marafiki na anawaombea marehemu wapumzishwe mahali pema peponi. Amina. 
Na amewaombea kwa Mwenyezi Mungu awape moyo wa subira na uvumilivu 
katika kipindi hiki kigumu.
Katika salamu hizo, pia Rais 
Malinzi amemtumia Rais Shirikisho la Mpira wa Miguu Burundi (BFF), 
Marlon Kuylen kwa sababu sehemu ya Bujumbura imeguswa na tetemeko hilo 
kadhalika ametuma salamu za rambirambi kwa Rais wa Shirikisho la Mpira 
wa Miguu Uganda (FUFA), Moses Magogo baada ya ripoti kuonesha kuwa 
tetemeko hilo limeukumba mji wa Kampala na Rakai nchini Uganda. 
Wataalamu wa elimu ya miamba – Jiolojia wanasema kwamba lilikuwa ni 
kubwa kwa mujibu wa vipimo.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni