WAKALA WA UFUNDI NA UMEME TEMESA PWANI WATUPIWA LAWAMA
Mkuu wa mkoa wa Pwani mhandisi 
Evarist Ndikilo wa katikati,akizungumza na viongozi mbalimbali wa mkoa 
wakiwemo wakurugenzi na wenyeviti wa halmashauri, wakuu wa wilaya na 
baadhi ya wabunge kuhusu hoja waliyoiibua kuhusu wakala wa ufundi na 
umeme TEMESA ,wa kwanza ma mwenyekiti wa wabunge wa mkoa wa Pwani 
Ridhiwani  Kikwete.
Meneja wa wakala wa ufundi na 
umeme(TEMESA )Mkoani Pwani ,Richard Mutagulwa wa tatu kutoka kushoto 
aliyefungata mikono akifuatilia kwa makini  malalamiko yanayotolewa na 
viongozi mbalimbali mkoani hapo juu ya wakala huo kuzorota katika kazi 
zake na kutoza gharama kubwa za matengenezo ya magari ya serikali.
(Picha na Mwamvua Mwinyi)
…………………………….
Na Mwamvua Mwinyi
 WAKALA wa ufundi na umeme (TEMESA)mkoani Pwani,umelalamikiwa 
kuwa na mafundi wa mitaani lukuki na kuzorota katika kufanyakazi zake 
ipasavyo huku ikitoza gharama kubwa za matengenezo katika magari ya 
serikali.
Wakala huo unatupiwa lawama za 
kutengeneza kwa gharama kubwa kuanzia 500,000 hadi mil.11 kwa gari moja 
wakati magari hayo yangepelekwa kwa mafundi wa kawaida gharama zingekuwa
 nafuu.
Licha ya hayo magari ya mkuu wa 
mkoa huo sambamba na katibu tawala wa mkoa bado yapo kimatengenezo kwa 
zaidi ya miezi mitatu sasa . kutokana na kushindwa kukidhi vigezo vya 
ufundi licha ya gharama zao kuwa juu.
Hayo yalisemwa na baadhi ya 
wabunge,wenyeviti wa halmashauri,wakuu wa wilaya na viongozi wengine wa 
serikali ya mkoa wa Pwani kufuatia kero kubwa wanayoipata mara 
wanapopeleka magari kutengenezwa na TEMESA.
Waliiomba serikali iangalie njia 
nyingine ya kutengeneza magari yake ya serikali badala ya kutumia wakala
 huo ambao hauwasaidii zaidi ya kupoteza fedha nyingi.
Changamoto hiyo pia imemkuta mkuu 
wa mkoa wa Pwani,mhandisi Evarist Ndikilo ambae anasema hata yeye gari 
lake liko linatengenezwa huko,hivyo kuna haja ya sheria ya utengenezaji 
magari kuangaliwa upya.
Nae mwenyekiti wa halmashauri ya 
wilaya ya Kibaha Mansoor Kisebengo ,alisema  wamepeleka magari yao 
matatu kwa ajili ya matengenezo na kila gari limetakiwa gharama ya 
mil.11.
Alisema badala ya kutengenezwa kwa
 magari hayo lakini baada ya matengenezo yamerudishwa yakiwa na hali 
mbaya zaidi hivyo kuwapa hasara.
Kisebengo alisema serikali 
inawajibu wa kuliangalia jambo hilo kwani fedha hizo zingeweza kutumiwa 
na mambo mengine ya kijamii kuliko kuzipoteza .
Mwenyekiti wa halmashauri ya 
Chalinze,Saidi Zikatimu alieleza kwamba ni vyema serikali ikaawamini 
kama wanavyowaamini katika matumizi mengine ya fedha kwa kuwaruhusu 
kutengeneza magari kwa mafundi wa nje.
Alisema walipeleka magari yao TEMESA lakini magari hayo bado ni mabovu hayafanyi kazi na hela imepotea.
Zikatimu alisema wakala huo 
wamekuwa wakitengeneza magari hayo kwa fedha nyingi huku yakiwa chini ya
 kiwango na kusababisha magari hayo kutofanya kazi baada ya 
kutengenezwa.
Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Kibiti, Alvera Ndabagoye alisema serikali inapaswa kuliangalia jambo hilo kwa umakini.
Alisema kwasasa hakuna haja ya kuwa na Temesa kwani wamekuwa wakifanyakazi kwa kutokuwa na umakini .
Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini
 Hamoud Jumaa alisema wamefanya utafiti juu yao na kugundua kuwa uwezo 
wao ni mdogo ,na siku chache zilizopita walitengeneza gari la wagonjwa 
la Kwala ambapo gharama zilikuwa ni mil.5 lakini baada ya muda mfupi 
limeharibika na sasa liko sokoni wakitaka kuliuza.
 Kamanda wa kikosi cha usalama barabarani mkoa wa Pwani Abdi 
Isango alisema kuwa gharama za wakala hao ni kubwa na hazikidhi lakini 
kwa mafundi wengine toka nje wanatengeneza kwa uhakika .
Akijibu malalamiko hayo, meneja wa Temesa mkoa wa Pwani,Richard Mutagulwa, alisema ni vema walalamikaji wakafanya utafiti .
Alisema huwa wakitengeneza magari hayo bila matatizo na lengo lao ni kutoa huduma bora kwa wateja wao.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni