SERIKALI YAENDELEA KUHAKIKI MADAI YA WATUMISHI WA UMMA
………………………………………………
Serikali imeendelea kupokea na kuhakiki madai ya watumishi wa umma yanayohusu mshahara na kuyalipa kadri ya uwezo wake kifedha.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa 
Nchi, Ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora 
Angellah Kairuki alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Singida Mjini Mhe.
 Mussa Sima lililohusu mpango wa Serikali kulipa madeni ya watumishi.
Waziri Kairuki amesema kuwa 
katika mwaka wa fedha 2014/2015 Serikali ililipa madai ya malimbikizo ya
 mshahara wa shilingi 56,293,372,627.37 ambapo yalilipwa kwa watumishi 
55,688 waliokuwa na madai yatokanayo na kupandishwa vyeo, ajira mpya na 
sababu nyinginezo.
Aidha, Waziri Kairuki amesema 
kuwa kwa mwaka 2015/2016 Serikali imeendelea kulipa madai ya malimbikizo
 ya mshahara wa watumishi wa umma ambapo hadi kufika mwezi Juni, 2016 
watumishi 31,032 walilipwa jumla ya shilingi 28,929,095,373.89.
Pia ameongeza kuwa madai ya 
mishahara ya watumishi 7,871 yenye jumla ya shilingi 13,754,462,429.29 
yameshahakikiwa na kuingizwa kwenye mfumo wa taarifa za kitumishi za 
mshahara yakisubiri kulipwa na madai ya watumishi 8,776 yanaendelea 
kuhakikiwa ili yaingizwe kwenye mfumo tayari kwa kulipwa.
Akijibu swali la Mhe. Zubeda 
Sakuru (Viti Maalum) lililohusu changamoto ya maslahi kwa watumishi wa 
sekta ya afya Waziri Kairuki amesema kuwa Serikali inatambua na 
kudhamini mchango unaotolewa na madaktari, matabibu na wauguzi nchini.
Hivyo, Serikali imeendelea na 
jitihada za kuboresha mishahara ya watumishi wake mwaka hadi mwaka 
ikiwemo ya wataalamu wa sekta hiyo kwa kuzingatia uwezo wa Serikali wa 
kulipa.
Waziri Kairuki amesema kuwa 
Serikali inaendelea na utafiti wa tathmini ya kazi, punde 
itakapokamilika itapanga mishahara na motisha upya kwa watumishi wote wa
 umma wakiwemo wa sekta ya afya.
Aidha, amebainisha kuwa Serikali
 itaendelea kuboresha maslahi ya watumishi kadri ya uwezo wake wa kulipa
 utakavyoimarika ambapo katika shughuli za kila siku madeni huzalishwa 
lakini ni azma yake kuhakikisha madeni hayo yanalipwa mara 
yanapojitokea.
Mbali na hayo, Waziri Kairuki 
ametoa wito kwa wataalamu wa afya na watumishi wote kwa ujumla kufanya 
kazi kwa bidii na kwa kuzingatia viapo na maadili ya kazi zao.
 
 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni