Jumapili, 29 Machi 2015

SITTA AKAMILISHA MPANGO WA RELI MPYA (STANDARD GAUGE)

NA TINA RUBEN,
Waziri wa Uchukuzi,Samuel Sitta amesema  kuwa RAHCO (Kampuni ya Rasimali za Reli)wamekamilisha utaratibu  wa kumpata Mshauri wa Mradi  ambaye  ni Kampuni ya  Roths child ambayo  itawezesha kupata fedha za ujenzi wa Reli Mpya ya kati kwa Kiwango cha "Standard  Gauge "ambayo gharama yake ya ujenzi  ni Dola za Kimarekani Bilioni 7.6.
 
Alisema hayo leo jijini Dar es Salaam alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari,amesema fedha hiyo ni  ni sawa na shilingi  za Kitanzania  Trilioni 14 reli hiyo  itakuwa na urefu wa Kilomita 2561.

Sitta alisema mradi huo utakuwa  mkubwa kutekelezwa  na serikali  toka tupate Uhuru,na Serikali  haitatoa hata dola Moja kutoka Hazina bali utagharamiwa na mabenki ambayo ndiyo yatakayotoa fedha.

 Reli hiyo Mpya kabisa tofauti  na  iliyopo itakuwa  yenye uwezo mkubwa wa Kimataifa "Standard Gauge railway " itaanzia Dar es Salaam Mpaka Kigoma, kupitia Tabora, Mwanza,Isaka hadi Rusumo; Kaliua -Mpanda -Karema na Uvinza -Musongati nchini Burundi.

 Pia alisema  reli hiyo itasaidia kukidhi mahitaji  makubwa ya ubebaji mizigo kwenda nchi jirani za DRC, Rwanda, Burundi,  na Uganda na itasaidia  Wananchi  kwenda mikoani kwa wingi na kwa kasi zaidi.

  "Wengi watajiuliza kwa nini tumeamua kujenga reli Mpya?
  Ni kutokana na sababu  kwamba reli  iliyopo sasa ambayo ni ya Kiwango cha "meter Gauge " uwezo wake  wa kubeba mizigo hata baada ya ukarabati kwa mwaka ni tani Milioni 5,ambazo haziwezi  kukabili mahitaji ya mizigo ya Kanda hii ambayo itafikia tani Milioni 30 ifikapo mwaka 2025".Alisema Sitta.

  
Mradi huu wa kujenga reli ya kati utaajiri watanzania takribani 300,000 watakaohusika na ujenzi  wa reli hiyo itakayojengwa kwa muda wa miaka 5 .Reli hiyo itafanya upelekaji wa mizigo kutoka bandari ya Dar es Salaam  Mpaka nchini DRC kuchukua muda wa takribani saa 12.

 "Tumejipanga ili Uzinduzi  wa ujenzi wa reli hii ya kihistoria  ufanywe na Mheshimiwa  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete  kwa kuweka jiwe la msingi ifikapo tarehe 30 Juni , 2015 yaani Mwaka huu tulionao kule Mpiji Kituo cha stesheni Mkoa wa Pwani ambako ndiko reli itaanzia". Alisema

   Kwa ujumla reli zote  zitagharimu jumla ya kiasi cha Dola za kimarekani Bilioni 14.2 ambazo ni  sawa na shilingi za Kitanzania  Trilioni 26 zitaajiri  zaidi  ya watanzania  Milioni  Moja kwa miaka  yote zitakapokuwa zinajengwa.
 Waziri wa Uchukuzi Samuel Sitta akizungumza na waandishi leo ofisini kwake jijini Dar Es Salaam.
Baadhi ya Waandishi wa habari

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni